‘Kanisa haliwezi kuendelea bila matumizi sahihi ya rasilimali’


MWENYEKITI wa Mawasiliano Jamii AMECEA Askofu Charles Kasonde amesema kuwa, utaalamu juu ya matumizi sahihi ya rasilimali watu na fedha ndiyo chanzo cha maendeleo endelevu katika Kanisa.
Askofu Kasonde amezungumza hayo wakati akifungua Warsha ya siku nne ya wakurugenzi wa Kichungaji na Mawasiliano pamoja na wanahabari wa AMECEA juu ya uratibu madhubuti wa rasilimali fedha na watu iliyofanyika katika Baraza la Maaskofu Katoliki Ethiopia (Addis Ababa Ethiopia).
Warsha hii ya kujifunza namna ya kuandika miradi bora yenye vigezo ni muhimu katika Kanisa kwani wakati huu ujuzi wa kuandika miradi umekuwa na changamoto mbalimbali ambazo bila kuzifanyia kazi hatutaweza kuendelea.
Ni wazi kwamba tunategemea wafadhili kupitia miradi. Wafadhili kwa sasa wamepungua na sisi waombaji tumeongezeka. Hivyo kwa namna moja ama nyingine vigezo na masharti vimeongezeka  ndiyo maana lazima tuwe na utaalamu na ubunifu katika kuandika miradi.
Ninaamini kila mmoja akipata ujuzi huu kama wanahabari na waratibu wa Kichungaji katika nchi zetu za AMECEA tutapunguza mzigo wa kuendesha taasisi katika Mabaraza yetu ya Maaskofu. Utaalamu huu hatuwezi kuukwepa kwani bado nchi zetu ni masikini hatuwezi kujiendesha bila wafadhili wetu,” amesema Askofu Kasonde.
Aidha amesisitiza kuwa makini na wafadhili ambao wanatuma fedha kwamba lazima baada ya kupokea fedha na kuzitumia, anayetekeleza mradi lazima aandike ripoti iliyo na utaalamu, kwa uwazi na uaminifu ili kuondoa maswali na mashaka kwa wafadhili.
“Kuchelewesha ripoti, kuandika ripoti isiyoeleweka, iliyo na maswali mengi kumesababisha wafadhili kupungua kwasababu wanaona baadhi si waaminifu wa rasilimali fedha. Ninawasihi kutumia akili zetu kujitoa kabisa kusikiliza warsha hii ili kuleta mabadiliko katika nchi zetu na majimbo yetu,” amesema Askofu Kasonde.
Amepongeza Ofisi ya Mawasiliano AMECEA pamoja na ya Kichungaji kwa kuwaunganisha wanachama wa AMECEA pamoja ili kupata elimu ya namna ya kuratibu rasilimali fedha na watu. Amesema kuwa inaonesha uhai wa AMECEA na kuleta umoja na mshikamano kati yao kwani wote wanakabiliwa na changamoto zinazofanana na ni vyema kushirikishana changamoto hizo ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi.
Askofu Kasonde ambaye pia ni  Askofu wa Jimbo Katoliki Solwezi  nchini Zambia amesisitiza uwajibikaji, uwazi, ukweli na uadilifu katika kutekeleza miradi kwakuwa hayo yanasaidia kujenga fursa zaidi ya kufadhiliwa tena siku za mbeleni.
Akizungumza katika warsha hiyo, Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ethiopia Padri Abba Hagos Hayish amesema kuwa, Baraza hilo limefarijika kupokea mkutano huo (warsha) ya namna ya kuratibu rasilimali fedha na watu hususani miradi kwani hata Kanisa la Ethiopia lina changamoto hizo za kutafuta fedha kwa ajili ya kujiendesha.
“Ninawashukuru kwa kuichagua Ethiopia kufanyia warsha hii. Maaskofu, mapadri pamoja na waamini wanawapokea kwa mikono miwili kama ndugu zao.
Mfahamu kuwa wakristo wakatoliki hapa Ethiopia ni wachache. Hata hivyo pamoja na uchache wetu jamii ya hapa inalitegemea Kanisa Katoliki kutoa huduma za kijamii hususani elimu na huduma za afya.
Tunatoa huduma kwa watu zaidi ya milioni 50, hivyo namna ya kupata rasilimali fedha ni changamoto. Kumbe Warsha hii itawaongezea ujuzi wanahabari wetu, waratibu wetu Katika ofisi ya Kichungaji namna ya kuandika miradi ili wapate ujuzi huo. Huu umekuwa ni muda mwafaka kwetu,”amesema Padri Abba Hayish.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU