Taifa kuwa na sera ya maadili

NAIBU waziri wa habari, utamaduni, sanaa na michezo Mhe. Annastazia James Wambura amesema wizara hiyo ipo mbioni kutunga sera ya maadili ya taifa ili kuliepusha taifa na athari zitokanazo na mmomonyoko mkubwa wa maadili.
Uamuzi huu unakuja baada ya wadau wa habari, utamaduni na sanaa kubainisha kuwa kwa sasa taifa linakabiliwa na changamoto nyingi katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo kutokana na baadhi ya watumishi wa umma na sekta binafsi kukosa maadili ya kiuongozi na kijamii hivyo kuhitaji kuwa na sera hiyo.
Akihitimisha mkutano wa “TUZUNGUMZE” ulioihusisha wizara hiyo na wadau mbalimbali wa utamaduni habari na sanaa uliofanyika katika uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam, naibu waziri Annastazia James Wambura amesema kwa vile maoni ya wadau yanawakilisha jamii nzima ya watanzania, wizara yake italifanyia kazi pendekezo hilo baada ya kukusanya maoni zaidi.
“Kutokana na kukithiri kwa mmomonyoko wa maadili nchini japokuwa tulikuwa hatujajiandaa, lakini tutashirikiana na sekta na wizara mbalimbali ili kutunga sera hii ambayo kimsingi itakuwa jibu sahihi la maovu mengi yanayoonekana nchini hivi sasa,” amesema
Naibu waziri amesema kuanzia ngazi ya familia, kazini, katika sekta mbalimbali matendo ya mmomonyoko wa maadili yapo wazi hali inayosababisha utekelezaji wa sera za maendeleo kuwa mgumu.
“Wapo baadhi ya wananchi ambao wana tabia za kutokuwa waaminifu kwa taifa kwa kukwepa kulipa kodi hali ambayo inairudisha serikali nyuma katika ukusanyaji wa mapato na kuwapatia wananchi huduma bora za kijamii, endapo sera hii itaundwa basi matatizo kama haya yatapungua na hatimaye kumalizika”
Ametaja baadhi ya sababu zinazosababisha mmomonyoko wa maadili kuwa ni kukua kwa utandawazi, ukosefu wa elimu ya kutosha ya maadili katika taasisi za elimu na kwenye jamii, kutokuwepo na sera ya maadili ya kitaifa ambapo kila mtu anafanya anavyotaka, kutokuwepo na ushirikiano wa kutosha kwa sekta mbalimbali, baadhi ya wasanii kuwa na tabia zisizofaa katika jamii na baadhi ya vyombo vya habari kuandaa vipindi visivyozingatia maadili.
“Hali imekuwa mbaya sasa ambapo taifa linaendeshwa kwa maelekezo ya mitandaoni, yale yanayoandikwa kwenye mitandao ya kijamii yanapewa nafasi kubwa katika maisha ya kila siku ya wananchi hasa watoto yawe mabaya ama mazuri, hali hii imelifikisha taifa hapa kwani badala watu wafanye kazi za kujenga uchumi na familia zao, wamebakia kujikita katika yale yanayoandikwa kwenye mitandao ambayo huandikwa na watu wasiokuwa na taaluma za uandishi,” amesema
Naibu waziri amebainisha kuwa athari za mmomonyoko wa maadili ni pamoja na kupoteza mwelekeo wa kitaifa ambapo kutokana na kukua kwa utandawazi  na watoto wengi kumiliki simu za kisasa na kutumiana taarifa mbalimbali hivyo kuibua kizazi chenye tabia zisizofaa, taifa kupata viongozi wasio na maadili kutokana na yaliyokithiri katika jamii na kushuka kwa uchumi kutokana na matumizi ya dawa za kulevya, ulevi, ujambazi na matumizi ya rushwa.
Hata hivyo amewaomba viongozi wa kidini nchini kuisaidia wizara kuhamasisha suala la maadili mema kutokana na wao kuwa kiungo kikubwa.
“Nawaomba viongozi wa dini wote nchini muendelee kuwafundisha waamini wenu maadili mema, hii inatokana na ukweli kuwa mnakaa nao muda mrefu, wanakiamini kile mnachowaambia pia mna ushawishi mkubwa, endapo mtatumia fursa hiyo vyema basi mtakuwa mteirahisishia wizara kazi.”
Wadau wa utamaduni, habari na sanaa walioshiriki katika kikao hicho wameitaka wizara hiyo pamoja na kutunga sera ya maadili ya taifa pia iboreshe ushirikiano na sekta mbalimbali juu ya maadili, kuwatumia wasanii kutoa taswira ya maadili ya taifa, idhibiti matumizi ya mitandao ya kijamii na kudhibiti maadili ya baadhi ya vipindi vya redio na luninga, jamii na wazazi watimize majukumu yao kulinda maadili, wizara itumie vyombo vya habari kufanya kampeni ya kuboresha maadili.
kwa kipindi kirefu kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo juu ya taifa kutokuwa na sera ya maadili itakayofuatwa na wananchi wote hali ambayo imesababisha athari mbalimbali katika mipango endelevu ya kimaendeleo.
Ili kuharakisha mchakato wa upatikanaji wa sera ya maadili ya taifa, Wizara imeweka mkakati wa kukusanya maoni ya wananchi nchi nzima kwa kuandaa mikutano na makongamano kufanikisha lengo la kuwa na taifa lenye maadili mema.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU