Hospitali ya Mt. Fransisko Ifakara yazindua jengo kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa wa nje (OPD).



Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Fransisko Ifakara inayomilikiwa na Jimbo Katoliki Ifakara imezindua jengo maalumu kwa ajili ya idara ya huduma kwa wagonjwa wa nje yaani OPD, ambalo limejengwa na serikali ya Uswisi kupitia shirika lake la maendeleo la SDC.
Jengo hilo ni moja kati ya mengi yaliyojengwa na mengine kufanyiwa ukarabati katika hospitali hiyo kuanzia mwaka 2012 na limefunguliwa na Mheshimiwa Manuel Sager ambaye ni Balozi wa Uswizi na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo na uhusiano la Uswisi (SDC).
Pamoja na ujenzi wa jengo hilo na ukarabati wa majengo mengine, Shirika la SDC linaendelea pia  kuboresha miundombinu mingine ya Hospitali hiyo ili kuwezesha utolewaji wa huduma za afya katika hospitali hii kuwa rahisi, bora na ufanisi zaidi huku ikihudmia wagonjwa wapatao milioni moja kwa mwaka kutoka katika mkoa wa Morogoro na mikoa jirani.
Akiongea katika hafla ya uzinduzi wa jengo hilo, Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara Mhashamu Salutaris Libena ameishukuru Serikali ya Uswisi na shirika lake la maendeleo pamoja na Ubalozi wa Uswisi Tanzania kwa kuwezesha ujenzi na ukarabati wa majengo mbalimbali ya hospitali hiyo.
Tunaishukuru Serikali ya Uswisi kwa kushirikiana nasi, na tunaahidi kuendeleza ushirikiano huu mpaka kizazi kijacho, tunaahidi kutekeleza na kusimamia yote tunayokubaliana kwa lengo la kuendeleza muungano huu, lakini pia kazi kubwa iliyofanyika hapa ni mchango mkubwa kutoka kwa Serikali na watu wa Uswisi hasa katika nyanja ya afya, amesema Askofu Libena.
Katika hotuba yake Mheshimiwa Balozi Sager amezipongeza juhudi za wote walioshiriki kuiboresha hospitali hiyo huku akisema ana uhakika kazi hiyo itaendelea katika maeneo mengine ya hospitali na kwamba anaona fahari kwa Serikali ya Uswisi kuweza kuboresha sekta ya afya kwa Watanzania hususani jimboni Ifakara.
“Jengo hili ni sehemu moja kati ya nyingi zinazohitajika ili kutoa huduma bora za afya kwa jamii, rasilimali watu wenye ujuzi na ufanisi wa kiutendaji wa shirika pia ni sehemu muhimu katika uboreshaji wa huduma za afya, pia nashukuru kwa heshima kubwa mliyonipa ya kuzindua jengo hili la OPD na kuwekwa kumbukumbu ya jina langu kwenye ukuta wa jengo hili. Amesema Balozi Sager.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dr Kebwe Steven Kebwe amesema anaheshimu mataifa yote yanayotoa misaada nchini na kuliomba Taifa la Uswisi kutositisha msaada na ushirikiano na Tanzania katika maeneo mbalimbali kama ilivyo katika Mkoa wa Morogoro.
Hafla hiyo imefanyika katika viwanja vya Hospitali hiyo ya Rufaa ya Mt.Fransis Ifakara na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dr Kebwe Steven Kebwe, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero Bwana James Ihunyo, Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara Mhashamu Salutaris Melchior Libena, Balozi wa Uswisi Nchini Tanzania Mheshimiwa Florence Tinguely Mattli, Mkuu wa idara ya maendeleo na ushirikiano wa ubalozi wa Uswizi  Bi, Romana Tedeschi pamoja na Mkuu wa Sekta ya Afya wa Ubalozi wa Uswisi Dr. Thomas Teuscher.
Taifa la Uswizi na Jimbo Katoliki Ifakara yana historia nzuri ya mahusiano inayokaribia karne moja kwa sasa na hospitali ya Mtakatifu Fransisko na taasisi zingine za Mafunzo na utafiti zilizopo Ifakara zimekuwa zikishirikiana na taasisi mbalimbali za Uswisi zikiwemo Swiss Tropical and Public Health Institute (Swiss TPH) pamoja na Solidar Med.
Aidha kupitia ushirikiano huo kati ya Uswisi na Tanzania  Shirika la SDC la nchini Uswisi limechangia Shilingi Bilioni 17 au Dola za Kimarekani Milioni 7.8 kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia Mwaka (2012 - 2017) ili kusaidia mpango mpana unaojumuisha ujenzi na ukarabati wa majengo ya Hospitali, ununuzi wa vifaa vya matibabu, uboreshaji wa mifumo ya teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT),  pamoja na uboreshaji wa huduma za afya utawala na usimamizi.
Kwa sasa Hospitali ya Mt. Fransisko ina uwezo wa kulaza zaidi ya wagonjwa 370 na inatoa huduma mbalimbali za afya ikiwa ni pamoja na huduma za madaktari bingwa huku ikiwa miongoni mwa hospitali 10 zinazomilikiwa na Mashirika ya Kidini ambazo zilipandishwa hadhi na Wizara ya afya maendeleo ya jamii jinsia wazee na watoto na kuwa Hospitali ya rufaa katika ngazi ya Mkoa Mwaka 2012.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU