Askofu Minde awataka mapadri kuwapa ushirikiano UWAKA Kahama



ASKOFU wa Jimbo Katoliki Kahama Mhashamu Ludovick Minde amewataka mapadri  kuwasaidia  wanaume wa Umoja wa Wanaume Katoliki (UWAKA)  kuutambua  umuhimu wao katika kazi za  utume na uinjilishaji ndani ya  Kanisa pia juu ya  kulitegemeza Kanisa kuanzia ngazi ya familia, Jumuiya na Parokia zao.
Askofu Minde ameyasema hayo  katika misa takatifu ya  kuhitimisha  semina ya mafunzo ya siku 5  ya  kiroho na sala kwa  viongozi wa  Umoja wa Wanaume Katoliki ( UWAKA )  Jimbo Katoliki Kahama.
Amesema mafunzo waliyoyapata katika semina hiyo juu ya umuhimu wao katika mambo ya kiroho, sala na utume wao kwa Kanisa yawasaidie kujitambua katika kazi za kitume juu ya kulitegemeza Kanisa.
Amesema nafasi ya UWAKA ndani ya Kanisa ni pana hivyo lazima ionekane kwa kutimiza wajibu wao kwa matendo kuanzia kwenye familia, jumuiya, vigango, kiparokia na kijimbo na kuwataka wawajibike katika kulitegemeza Kanisa kwa sara na kiroho.
Askofu Minde amesema uwepo wa UWAKA ni muhimu sana ndani ya  Kanisa  katika kazi za uinjilishaji na utume wa  sala na kiroho, hivyo  kwa nafasi hiyo wanapaswa wawe wa kuwajibika kwa Kanisa na familia  kwa kutimiza wajibu wao na uonekane wazi.
“Utume wa wanaume wakatoliki ( UWAKA ) siyo wa kisiasa, ni utume wa kiroho ndani ya Kanisa katika kazi  za uinjilishaji kwa sala na lazima uonekane kwa kuchukua nafasi waliyonayo ya  baba kuanzia kwenye familia, Kanisa, katika mambo ya imani ya Kanisa Katoliki,” amesema Askofu Minde.
Askofu Minde amewataka UWAKA kufungua ukurasa mpya katika maisha ya utume wao ndani ya Kanisa kwa sifa na utukufu wa Mungu sababu yupo pamoja nao katika kutekeleza wajibu wa nafasi waliyonayo katika mambo ya kiroho na kimwili.
Akisoma taarifa ya UWAKA ya jimbo baada ya misa Dr.Sostenes Nkombe pamoja na kumshukuru Askofu Minde kwa semina hiyo amekiri kuwa imewapatia ari na uwezo wa kutekeleza majukumu yote yawapasayo wanaume wakatoliki.
Dr.Nkombe amesema katika hitimisho la semina yao wameazimia  kutekeleza malengo 10 ambayo ni sala, uwaka na elimu, uwajibikaji, majitoleo, uaminifu, uwaka na utume wetu, vikao , uchaguzi wa viongozi, uwaka na sensa na uwaka na malezi.
Pia wameahidi kushirikiana kwa karibu na Askofu Minde, mapadri, watawa na vyama vyote vya kitume jimboni Kahama.


Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU