"WANYONGE WAPEWE KIPAUMBELE" ASKOFU KASSALA



                                    
       

Na Sarah Pelaji, Dar es Salaam
SERIKALI na taasisi za kidini zisipomgusa mnyonge zina ubaridi na kasoro katika utendaji wake.

Askofu wa Jimbo Katoliki Geita Mhashamu Flavian Kassala ametoa rai hiyo wakati akifafanua juu ya kikundi cha watu nchini Marekani kilivyotaka kuharibu sherehe ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni pamoja na kuzungumzia suala la Mama Thereza wa Kalkuta kutangazwa Mtakatifu Septemba mwaka huu.

“Huo ni mmomonyoko wa maadili na kukosa imani ya hali ya juu kwa kumdhihaki Mama Mtakatifu. Jitihada zifanyike kuwazuia vijana wetu wasiingie katika uanachama wa kuabudu shetani.” Amesisitiza

Askofu Kassala ameeleza kuwa, Si nchini Marekani tu ambapo baadhi ya watu wanajaribu kuchafua Sherehe ya Bikira Maria bali hata baadhi ya wananchi nchini Italia wamekosa mwelekeo wa kiimani kwa kugeuza sherehe za Bikira Maria kuwa sherehe za kutatapanya mali kwa kufunga kipindi cha kiangazi na kujiandaa na kipindi cha baridi.

“Sherehe ya Bikira Maria katika mazingira ya Italia inachukuliwa katika sehemu mbili, kwanza ni sherehe ya Kanisa pili ni sherehe ya mazingira ya kidunia.
Huwa wanasherehekea mazingira yao ya kufunga kipindi cha joto kwa kufanya sherehe kubwa za kutapanya mali na kufanya kila aina ya starehe.

Huwa wanawapeleka wazee kwenye nyumba za kutunzia wazee ili wapate nafasi ya kustarehe na kutapanya mali ili baada ya hapo wakusanye kwa ajili ya kipindi kingine cha joto kinachoanza Juni mpaka August.
Hivyo ukiangalia hawa ni kinyume na maisha ya Mama Thereza kwamba wanatumia mali kwa kumtenga maskini na wasiojiweza. Mama Thereza alitumia muda na nguvu zake kuwasaidia masikini.
Aligusa maisha ya mnyonge ambaye amekosa matumaini. Ndio maana anaenda kutangazwa Mtakatifu kwa maisha yake ya kumfanya mnyonge kujisikia huru na binadamu mwenye furaha na matumaini.”
Ameiasa serikali kugusa maisha ya mnyonge kwa kumuinua kutoka majalalani, kukaa barabarani na kumpeleka katika mazingira bora. Isimuinue mtu ambaye tayari ameshainuka bali imuinue yule ambaye anatamani kuinuka lakini hana uwezo.
“Kiongozi bora anagusa maisha ya watu, anajibu changamoto za watu wake hususani wasiojiweza na masikini. Kanisa kadhalika lisiwe baridi kujibu changamoto za waamini wake ambao wanahitaji faraja na kupata matumaini kupitia kwake”.

Askofu Kassala anaongeza. “Kiongozi bora ni yule anayesoma alama za nyakati. Haishi kwa kushika kanuni tu bali analinganisha kanuni na mazingira ya watu wake. Kanisa pia lisome ishara za nyakati kwa kutafsiri kanuni na changamoto za sasa ili waamini wake wasiweke kasoro na maswali mengi dhidi yake. Kumbe utendaji ni uleule lakini kwa mfumo tofauti,”
Mwito wake kwa jamii ni kuzingatia maadili na kufanya mambo ya msingi yanayomuinua mwingine badala ya kumkandamiza.
“Wengi wetu tunaweza kuwa Mama Thereza kama tunafanya kazi kama inavyopaswa kwa furaha na matumaini, kumuangalia aliyeko dhaifu miongoni mwetu na kumtetea pale anapokandamizwa”.

“ Ukiangalia utendaji wa serikali utaona ubinafsi katika baadhi ya watendaji. Wanafunzi wanaketi chini hakuna madawati, watu wanakufa kwa kiu bila maji, njaa na mengine lakini kila mwaka bajeti inapitishwa. Je, bajeti hiyo ni kwa ajili ya nani? Serikali ijipange kuwainua wanyonge ambao wanahitaji nguvu yake ili wainuke badala ya kuinua wale ambao tayari wameshainuka.” Amesisitiza.

Hivi karibuni Baba Mtakatifu Fransisko wakati wa Malaika wa Bwana mjini Vatikani amesema kuwa, Kanisa halihitaji kuwa na utendaji wenye urasimu kutumikia kwa upendo na huruma katika  kujali  mahitaji ya watu hasa waliosahaulika pembezoni katika  umaskini na upweke.

Papa alionya kwamba, waamini wa Kanisa  bila kuwa na mioyo iliyojaa huruma na upendo , kuna hatari kwa Kanisa kuwa baridi katika utendaji wake. 

Alitaja ubaridi huo  au imani ya uvuguuvugu tu, maana yake , ni kuwa na utendaji  usioonyesha dhahiri  utambulisho wa Kanisa katika maisha ya kijamii.
Ifahamike kuwa, huko Marekani katika mji wa Oklahoma, Maaskofu wa Kanisa Katoliki waliwaasa waamini duniani kusali sala maalumukupinga ibada ya mashetani iliyokuwa imepangwa na wanachama wake ili kumkejeli Bikira Maria siku ya Sherehe ya Kupalizwa kwake Mbinguni August 15 mwaka huu.

Kufuru hiyo dhidi ya Bikira Maria ilipangwa ifanyike katika mji huo huku wafuasi wa kikundi hicho wakiwa wameshika sanamu ya Bikira Maria wakiidhihaki.

Askofu Mkuu wa Oklahoma Mhashamu  Paul Coakley aliitisha sala maalumu ili kuungana na waamini kusali kama familia kuzuia jambo hilo ovu.
Hata hivyo alilaumu serikali za mitaa kushindwa kuzuia ama kushughulikia nia ya kufanya dhihaka hiyo.

                  

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU