NINI KIFANYIKE WANANDOA WANAPOSHINDWA KUVUMILIANA?



                                    
                            Nini kifanyike wanandoa wanaposhindwa kabisa kuvumiliana?

Na Philip Komba,
0754 054 004
     Ni kweli, kwamba ndoa iliyofikia mwungano na mshikamano kwa mujibu wa Sheria ya Kanisa Na. 1141 haiwezi kuvunjwa au kutanguliwa na mtu yeyote wala na serikali wala na Kanisa isipokuwa na kifo tu. Sheria hii ya Kanisa Na 1141 inasema wazi kabisa kuwa ndoa iliyothibitishwa au iliyoidhinishwa na iliyopata ridhaa na kutiliwa sahini na wahusika, na halafu ndoa hiyo ikakamilishwa kwa tendo la ndoa haiwezi kamwe kutanguliwa kwa uwezo wowote ule wa binadamu au  kwa sababu iwayo  yoyote isipokuwa kifo.
     Swali la kujiuliza ni hilo lililo hapo juu. Nini basi kifanyike pale wanandoa walio katika mwungano usioweza kutanguliwa wanapofikia kiwango cha juu kabisa cha kushindwa kuvumiliana katika ndoa yao? Tuseme kwa mfano, mmoja wa wanandoa hawa ameficha silaha chini ya godoro la kitanda chao na muda wowote ule anaweza kuitumia kumdhuru mwanandoa mwenzake. Ni sawa kweli, huyu mwanandoa  mwenzake asubiri tu hadi hapo hiyo silaha iliyofichwa itumike kwa kumwua na ndipo ndoa yao ikome kama sheria ya Kanisa Na. 1141 inavyosema?
     Ni wazi kabisa, si sawa. Kutokana na ukweli huu kwamba kufanya hivyo si sawa, Kanisa Katoliki lina njia nyingine ya kuyashughulikia masuala kama haya. Njia hii ni ile ya kutengua na kamwe si ya kutangua ndoa  kama hizo kwa kuzingatia Sheria ya Kanisa Katoliki Na.1152. Sheria hii ni ile ya kuwaruhusu wanandoa hawa walio katika mwungano huu usioweza kutanguliwa, kutengana. Hata hivyo ruhusa hii ya kutengana kwa kutumia hiyo sheria ya Kanisa, inatolewa kwa shingo upande sana; na Kanisa Katoliki huitoa hiyo ruhusa  baada ya masharti mengi ya kujaribu kutafuta njia ya kuwafanya wanandoa hawa kusameheana. Kwa mfano, yule anayetakiwa kumsamehe mwenzake aonyeshe waziwazi kabisa kuwa amemsamehe huyu mwenzake au anaweza hata kutoa msamaha huo  kimyakimya tu. Kukubali kutoa msamaha kimyakimya  ni kukubali kufanya tendo la ndoa naye ingawa anajua kuwa amefanya  hilo tendo la ndoa na mwingine. Kama hali hii ya kusamehe kimyakimya ikiendelea kwa angalau miezi sita bila kupelekana kwa wakuu wa Kanisa au wakuu wa Serikali, basi mambo huwa poa na tatizo huwa limekwisha kwa kufikiriwa kuwa yule aliyekataa kusamehe sasa amesamehe. Inatakiwa pia yule anayekataa kumsamehe mwenzake, asiwe anatoa mwanya wa kumwingiza mwanandoa mwenzake katika kishawishi cha kumfanya afanye tendo la ndoa na mwingine kwa kukataa, kwa mfano, kufanya tendo la ndoa naye bila sababu za msingi. Inatakiwa pia kwamba yeye mwenyewe huyu asiyetaka kusamehe asiwe  anafanya tendo la ndoa na wengine.
     Lakini kwa upande mwingine, kama hata baada ya kipindi hicho cha kutokuwa na uhusiano wa maisha ya pamoja kama wanandoa kupita, na yule aliyekosewa bado anaendelea kuvuta kamba tu ya kukataa katakata kumsamehe mwenzake, basi yule aliyekosewa apeleke shauri lake la kutengana kwa Wakuu wa Kanisa. Wakuu hao wa Kanisa, nao watafanya uchunguzi wa kina wa mazingira yote yanayohusiana na shauri lenyewe; na bado, hata baada ya kufanya uchunguzi kama huo, wataendelea  kumshauri yule anayekataa kumsamehe mwanandoa mwenzake abadili msimamo wake, na atoe msamaha kwa huyu mwenzake na  hivyo utengano ufikie mwisho. Kama hata hilo likishindikana, shauri la kutengana kwa wanandoa hawa wabatizwa na wenye mwungano wa ndoa ya Kikristo  usioweza kutanguliwa,  linaweza kumalizwa kwa agizo la Askofu wa Jimbo au kwa hukumu ya hakimu wa Mahakama ya Kanisa kwa kuzingatia sheria husika za Kanisa Katoliki.
     Kwa kuwa mashauri ya kutengana yanaishia katika kugawanya mali iliyopatikana wakati wanandoa hawa walipokuwa wanaishi pamoja, na pia maafikiano kuhusu matunzo na huduma kwa watoto  iwapo walikuwa na watoto katika ndoa yao, Askofu wa Jimbo anaruhusiwa kwa mujibu wa sheria kutoa kibali kwa wanandoa hawa kupeleka shauri lao kwenye mahakama ya kiraia. Mahakama ya kiraia inayo, kwa kawaida, vyombo vya dola vya kuhakikisha kuwa mgawanyo wa mali iliyochumwa na wanandoa hawa kwa kushirikiana, unafanywa itakiwavyo kwa kuzingatia sheria za nchi na watoto kama wapo wanapata huduma wanayostahili.
     Wanandoa wanaofikia hatua hii, ambayo kwa kweli haipendezi, ya kutengana kwa kufuata utaratibu uliowekwa na Kanisa Katoliki, lazima waelewe kuwa ndoa yao inabaki palepale yaani inabaki ndoa ambayo ni halali na kwa mujibu wa Kanisa Katoliki hakuna anayeruhusiwa kufunga ndoa nyingine tena kanisani.

Imetayarishwa kwa msaada wa Kitabu cha Sheria za Kanisa: “The Code of Canon Law: A Text and    Commentary
Mwandishi ni Mhadhiri mstaafu,
CHUO Kikuu Huria cha Tanzania,
Dar es Salaam.




                    
                                              

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU