KAMUSI YA UKRISTO YAZINDULIWA



IMEELEZWA kuwa kuzinduliwa kwa Kamusi ya Ukristo nchini kutasaidia siyo tu uelewa wa imani na kukua kwa lugha ya Kiswahili, bali pia kutachochea upendo na amani nchini.
Hayo yameelezwa hivi karibuni na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Utamaduni kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Lily Beleko wakati akitoa salamu za serikali kwa niaba ya Waziri wa wizara hiyo, katika uzinduzi wa Kamusi ya Ukristo uliofanyika katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC).
“Maneno yakitafsiriwa visivyo huweza kusababisha chuki na vurugu. Uwepo wa Kamusi hii utarahisisha uelewa wa imani kwa jamii na kuleta upendo na amani. Wamisionari wa mwanzo walisaidia kukua kwa Kiswahili kupitia vitabu na machapisho yao mbalimbali. Ni imani yangu kuwa kamusi hii itachochea kukua kwa lugha ya Kiswahili” ameeleza.
Aidha kupitia hotuba hiyo, Beleko ameongeza kuwa, ni imani ya serikali kuwa watumiaji wa kamusi hiyo wataongeza maarifa huku wakiimarisha umoja, amani na uzalendo. Ameeleza kuwa serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za kukuza lugha ya Kiswahili na utamaduni wake, zinazofanywa na watu na taasisi mbalimbali.
Kwa upande wake mwandishi wa kamusi hiyo Padri Dkt. Jordan Nyenyembe ametoa wito kwa watanzania kuenzi utamaduni wa kusoma kwa kuwa unachochea hamu ya kutafuta ukweli na kuchambua mambo kwa makini.
“Dini zetu zimeletwa kwa njia ya vitabu, hivyo hatuwezi kukwepa kusoma. Anayesoma vitabu anasali tofauti, na anafikiri tofauti. Kazi ya uandishi bila ya kuwa na wasomaji wa uhakika inakua na ukakasi” ameeleza Padri Nyenyembe.
Naye Mkurugenzi wa Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) Dkt. Selemani Sewangi amesema kuwa kamusi hiyo ya kihistoria itasaidia kukidhi matumizi ya istilahi za kanisa ambazo hazipati maana kusudiwa katika kamusi ya kawaida.
“Kanisa lina msamiati wake unaopaswa kueleweka vizuri. Kamusi ya kawaida haitoshelezi maana kusudiwa. Katika uga wa ukristo, kwa mfano neno Mbingu, katika kamusi ya kawaida lina maana ya anga ya juu, lakini kwa maana ya kikristo bado haijatosheleza. Hivyo uwepo wa kamusi hii utasaidia kutoa maana halisi za istilahi za kikristo” ameeleza.
Kazi ya uandishi wa kamusi hiyo ya ukristo ilianza mwaka 2004 ambapo kupitia gazeti hili la Kiongozi, Padri Nyanyembe aliandika mfululizo wa makala isemayo ‘Kiswahili cha wanakanisa’, ambayo ndiyo imezaa wazo la kuwa na kamusi hiyo ya ukristo. 

Na: Paschal Mwanache,TEC
 








Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU