UJUMBE WA BABA MTAKATIFU PAPA FRANSISKO MAADHIMISHO YA 50 YA SIKU YA MAWASILIANO DUNIANI



UJUMBE WA BABA MTAKATIFU PAPA FRANSISKO MAADHIMISHO YA 50 YA SIKU YA MAWASILIANO DUNIANI

Mawasiliano na Huruma: Makutano yenye Tija

Wapendwa dada na kaka zangu,
Mwaka Mtakatifu wa Huruma unatualika sote kwa pamoja kutafakari uhusiano uliopo baina  ya mawasiliano na huruma. Kanisa, katika umoja na Kristo, aliye umwiliko hai wa Baba wa huruma, linakumbushwa kutekeleza huruma kama tofauti bainishi ya uwepo wake na kwa kila kitu litendalo. Kile tunachokisema na jinsi tunavyokisema, kila neno na tendo letu linapaswa kuwa kielelezo cha huruma, ukarimu na msamaha wa Mungu kwa wote. Upendo, kwa asili yake, ni mawasiliano; na huongoza kwenye uwazi na ushirikiano. Kama mioyo na matendo yanaongozwa na upendo wa Mungu, basi mawasiliano yetu yatakuwa yameguswa na nguvu za Mungu mwenyewe.
Kama watoto wa Mungu, tunakumbushwa kuwasiliana na kila mtu, pasipo kubagua. Kimsingi, maneno na matendo ya Kanisa yanalenga kufikisha huruma, kugusa mioyo ya watu na kuisaidia katika safari ya kuelekea ukamilifu wa maisha ambao Yesu Kristo alitumwa na Baba kuuleta kwa wote. Hii inamaanisha kwamba sisi wenyewe lazima tuwe tayari kulikubali joto la Mama Kanisa na kuwagawia wengine joto hilo, ili Yesu ajulikane na apendwe. Joto hilo ndilo linalolipatia neno la imani maana yake; kwa mahubiri yetu na ushuhuda, na kutoa cheche ambazo huwapatia watu uhai.
Mawasiliano yana nguvu ya kujenga madaraja, kuwezesha kukutana na kushirikishwa, na hivyo kuimarisha jamii. Hupendeza kiasi gani pindi watu wakichagua maneno yao na matendo kwa uangalifu, katika jitihada za kuepusha kutokuelewana, kutibu kumbukumbu za majeraha na kujenga amani na maelewano. Maneno yanaweza kujenga madaraja kati ya watu binafsi na katika familia, makundi ya kijamii na watu. Hii inawezekana katika dunia ya vitu na dunia ya utandawazi. Maneno na matendo yetu lazima yaweze kutusaidia sote kukwepa hali isiyokatika ya kuhukumu na kulipiza kisasi ambavyo huendelea kuwanasa watu binafsi na mataifa, ikihimiza hisia za chuki. Maneno ya wakristo yanapaswa kuwa faraja ya kudumu katika kujenga ushirika, hata katika matukio ambapo ni lazima kuulaani uovu bila hofu, ili kamwe yasijaribu kuvunja mahusiano na mawasiliano.
Kwa sababu hiyo, nawaalika watu wote wenye mapenzi mema kuivumbua upya nguvu ya huruma inayoponya mahusiano yaliyojeruhiwa na kuleta amani na maelewano kwa familia na jamii mbalimbali. Sisi sote tunajua ni namna gani majeraha ya zamani na chuki vinavyoweza kuwanasa watu na kuweka kizingiti katika njia ya mawasiliano na maridhiano. Hali hii inajidhihirisha pia katika mahusiano baina ya watu. Katika kila tukio, huruma inaweza kuanzisha aina mpya ya hotuba na mijadala. Shakespeare aliongea kwa ufasaha aliposema; “Ubora wa huruma hautetereshwi. Unashuka kama mvua mwanana toka mbinguni mpaka chini ardhini. Imebarikiwa mara mbili: inambariki inayeitoa na yeye anayeipokea” (Mabepari wa Venisi 4,I).
Lugha yetu ya kisiasa na kidiplomasia ingeboreka kama ingesukumwa na huruma, ambayo kamwe haikosi tumaini. Natoa rai kwa wenye majukumu ya kitaasisi na kisiasa, na wale wenye jukumu la kuunda maoni ya umma, kuweka tahadhari katika namna wanavyoongea dhidi ya wale wanaofikiri au kutenda tofauti nao au wale ambao watakuwa wametenda makosa. Ni rahisi kushawishika kutumia hali hizo na kuwasha moto wa kutokuaminiana, hofu na chuki. Badala yake, ujasiri unahitajika kuwaongoza watu kuelekea kwenye mchakato wa maridhiano. Ni ujasiri wa ubunifu chanya ambao hutoa suluhu ya ukweli kwa migogoro ya zamani na fursa ya kujenga  amani ya kudumu. “Heri wapatanishi, maana hao wataitwa wana wa Mungu.” (Mt 5:7-9).
Jinsi ninavyotamani namna yetu ya kuwasiliana, pia huduma yetu kama wachungaji wa Kanisa isiwe kamwe ya kiburi na kujivuna dhidi ya adui, au kuwatafsiri vibaya wale ambao dunia inawachukulia kuwa wapotevu na kuwapuuzia. Huruma yaweza kusaidia kupunguza mikasa ya maisha na kutoa joto kwa wale waliojua ubaridi tu wa hukumu. Namna yetu ya kuwasiliana isaidie kuondokana na fikra zinazowatenganisha wadhambi na wenye haki. Tunaweza na lazima tuhukumu hali za dhambi - kama vile ukatili, rushwa na unyonyaji - lakini hatuwezi kuhukumu watu, kwani ni Mungu pekee anayeweza kuona undani wa mioyo yao. Ni kazi yetu kuwaonya wale wenye kufanya makosa kuupinga uovu na udhalimu kwa namna fulani, kwa ajili ya kuwaacha huru waathirika na kuwanyanyua wale walioanguka. Injili ya Yohane inatuambia kuwa “ukweli utawaweka huru”(Yn 8:32). Ukweli muhimu zaidi ni Yesu mwenyewe, ambaye ukarimu wake wa huruma ni kipimo cha kupimia namna tunavyoonyesha wazi ukweli na kuupinga udhalimu. Kazi yetu kuu ni kuunga mkono ukweli kwa upendo (rej. Eph 4:15). Maneno pekee yanayosemwa kwa upendo na kwenda sambamba na ukarimu na huruma yanaweza kugusa mioyo yetu yenye dhambi. Maneno, matendo na misimamo mikali ya kimaadili inahatarisha kuwatenga zaidi wale tunaotamani kuwaongoza kwenye uongofu na uhuru, kwa kuzifanya hisia zao ziwe za kukataa na kujihami.
 Baadhi hufikiri kuwa maono ya jamii iliyo na mizizi yake katika huruma hayana maana. Lakini hebu tujaribu na tukumbuke uzoefu wetu wa kwanza wa mahusiano, ndani ya familia zetu. Wazazi wetu walitupenda na kututhamini kwa jinsi tulivyo zaidi kuliko kujali uwezo na mafanikio yetu. Wazazi kwa asili hutaka mafanikio kwa watoto wao, lakini upendo huo kamwe hautegemei watoto kutimiza masharti fulani. Nyumba ya familia ni mahali ambapo muda wote tunakaribishwa (rej.Lk 15:11-32). Nataka kumhamasisha kila mtu kuiona jamii siyo kama jukwaa ambapo wageni hushindana na kujaribu kuibuka washindi, bali kama nyumbani au familia, ambapo mlango upo wazi muda wote na kila mtu anajisikia kukaribishwa.
Ili jambo lipate kutokea,ni lazima kwanza tusikilize.Kuwasiliana kunamaanisha kushirikishana, na kushirikishana kunahitaji kusikiliza na kupokea. Kusikiliza ni zaidi ya kusikia. Kusikia ni kupokea taarifa, wakati kusikiliza ni kuwasiliana ambako kunadai ukaribu. Kusikiliza huturuhusu kuelewa kwa usahihi, na siyo kuwa watazamaji tu au watumiaji. Kusikiliza pia kunamaanisha  kuwa tayari kushirikishana  maswali na mashaka, kusafiri sambamba, kukomesha madai yote ya mamlaka ya kiimla na kuweka uwezo wetu na vipawa katika huduma ya manufaa ya wote.
Kusikiliza siyo rahisi. Mara nyingi ni rahisi kujifanya viziwi. Kusikiliza humaanisha kuwa na umakini, kutaka kuelewa, kuthamini, kuheshimu anachosema mtu mwingine. Huhusisha aina ya kifodini au kujitoa sadaka, tukijaribu kumuiga Musa mbele ya kichaka kinachoteketea: inabidi tuvue viatu vyetu tunaposimama “ mahali patakatifu” katika kukutana kwetu na yule aongeaye name (rej.Kut 3:5).Kujua jinsi ya kusikiliza ni neema kubwa, ni zawadi tunayotakiwa kuiomba na kufanya kila juhudi kuitekeleza.
Barua pepe, ujumbe mfupi, mitandao ya kijamii na kuchati vyaweza pia kuwa mbinu kamili za mawasiliano ya wanadamu. Siyo teknolojia inayoamua kama mawasiliano ni sahihi ama siyo, bali moyo wa mwanadamu na uwezo wetu wa kutumia kwa busara mbinu tulizonazo. Mitandao ya kijamii yaweza kuwezesha mahusiano na kutangaza mazuri ya jamii, lakini pia yanaweza kusababisha ubaguzi na mtengano kati ya watu binafsi na makundi. Dunia ya kisasa ni duara la wazi, eneo la kukutana ambapo twaweza kuhamasisha ama kutenganisha, kushiriki katika mijadala yenye mantiki ama mashambulizi yasiyo na usawa. Nasali ili Jubilei hii, tukiishi kwa huruma, “itufungue zaidi kuwa na bidii katika mazungumzano ili tuweze kujuana na kuelewana vizuri zaidi; na iweze kuondoa namna zozote za fikra zilizofungwa na zisizo na nidhamu, na kuondoa kila namna ya ukatili na ubaguzi” (Misericordiae Vultus, “Uso wa Huruma”, 23). Mtandao wa intaneti waweza kutusaidia kuwa raia wema. Upatikanaji wa mitandao ya kisasa unahusu wajibu kwa jirani yetu ambaye hatumwoni, ambaye lakini ni mtu halisi na mwenye hadhi ya utu ambayo ni lazima iheshimiwe. Mtandao wa intaneti waweza kutumika kiungwana kujenga jamii yenye afya na iliyo wazi katika kushirikishana.
 Mawasiliano, popote na kwa namna yoyote yanapofanyika, yamefungua upeo mpana zaidi kwa watu wengi. Hii ni zawadi ya Mungu inayodai uwajibikaji mkubwa. Napenda kurejea kwenye hii nguvu ya mawasiliano kama “ukaribu”. Kutano kati ya mawasiliano na huruma litazaa matunda endapo litaleta ukaribu unaojali, kufariji, kutibu, kusaidia na kusherehekea. Katika dunia iliyomeguka vipande vipande, kuwasiliana kwa huruma humaanisha kusaidia kutengeneza ukaribu wenye nguvu, huru na undugu zaidi kati ya watoto wa Mungu na dada na kaka zetu wote  katika familia moja ya kibinadamu.
 Kutoka Vatikani, 24 Januari 2016


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU