TANZIA: MAMA MKUU WA KWANZA WA SHIRIKA LA MT. AGNES CHIPOLE AFARIKI DUNIA




Waamini wametakiwa kutokata tamaa wanapopatwa na magonjwa, dhiki, mateso na misiba katika maisha. Hayo yamesemwa hivi karibuni na Padre Camilius Haule naibu wa Askofu mkuu wa jimbo kuu Katoliki Songea wakati wa adhimisho la misa takatifu ya mazishi ya Sista Ester Mwali OSB aliyekuwa mama mkuu wa kwanza wa shirika la Mtakatifu Agnes Chipole.
Padre Camilius amesema kuwa,” tunaguswa na mateso na misiba kwa sababu sisi ni binadamu tunaonja maumivu, na mateso kwa sababu kifo hakizoeleki na mtu yoyote kati yetu”.  Amesema kutokana na hali hiyo waamini hawana budi kushikamana na Mungu ili wapate nguvu ya kumwendea Yesu kwa pamoja.  Amesema  Mungu ndiye anayejua kwa nini ametuumba na kutupa uzima na kuutwaa tena na Mungu peke yake ndiye mwenye uwezo wa kumrejeshea mtu maisha yake tena kama alivyofanya kwa kumfufua Lazaro.
Padre Camilius amesema, “imani yetu itufanye tuamini kuwa, mateso na misiba  tunayopata hapa duniani yatufanye tutambue kwamba tunapomaliza maisha yetu hapa duniani tunapokufa na kuzikwa   bado  kuna uzima, na Yesu Kristu anatufufua kwani ndiye anayeshika uzima wakila mmoja wetu”.
Amesema Sister Ester  alikuwa kielelezo thabiti cha ukomavu wa imani katika kanisa mahalia, hususani katika jimbo kuu Songea na  amekuwa moja ya mafanikio ya kazi ya uinjilishaji ya wamisionari Wabenediktini toka Ujerumani  katika ukanda wa Kusini mwa Tanzania.  Sista Ester alikuwa mtu wa mang”amuzi na muhimili katika shirika la Mtakatifu Agnes Chipole.
Amesema kanisa linamzika mtawa aliyekubali kudhihirisha imani yake kwa kuishi mashauri ya injili, aliyeyatolea maisha yake ya imani katika mikono ya Yesu Kristu na utume kadiri ya roho ya kibeneiktini. Ameongeza kuwa, Sister Ester  alikubali kuwa kiongozi kwa miaka tisa {9} aliyekuja kutumikia na kutoa maisha yake kwa ajili ya kanisa.
Ameongeza kuwa,  kanisa na shirika limeondokewa na mmoja aliyekuwa kiungo katika mwili wa fumbo la Yesu Kristu katika nafsi ya Sister Ester , amewataka waamini kumwombea Sister Ester kwa mwenyezi Mungu ili aweze kusamehewa makosa yake na apokelewe katika uzima wa milele.
Sista Ester Mwali alizaliwa mnamo mwaka 1934, amefariki akiwa na umri wa miaka 82 ya kuzaliwa na miaka  55 ya nadhiri za kitawa, Aidha alikuwa mtu mwenye mapendo kwa Mungu na watu, mwaminifu, mvumilivu, mnyenyekevu, hodari mpenda kupokea na kutoa ushauri.

Sister Tuzo Nyoni, Songea




Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU