"MIAKA 40 YA UTUME SI MCHEZO SINGIDA"



Sakramenti ni alama wazi zinazoonekana na zenye nguvu ya kuleta neema ambazo aliziliweka Yesu Kristo Mwenyewe na kuzikabidhi kwa Kanisa ili ziweze kuwaletea wanadamu uzima wa kimungu.
Sakramenti hizo za Kanisa zipo saba ambazo zimegawanyika katika makundi makuu matatu, kundi la kwanza linahusisha Sakramenti za Mwanzo ambazo zinamwingiza mwandamu katika kupokea imani kwa Ubatizo, Kipaimara na Ekaristi Takatifu.
Kundi la pili lina ni Sakramenti za Uponyaji ambazo ni Kitubio na Mpako wa Wagonjwa na kundi la tatu linaundwa na Sakramenti za Ushirika na Huduma ambazo ni sakramenti ya Ndoa na Daraja Takatifu.
Kulingana na taratibu na misingi ya Kanisa Katoliki, Sakramenti ya Daraja Takatifu ni Sakramenti ambayo utume wake ulikabidhiwa na Kristo kwa mitume wake ambao unaendelea kutekelezwa katika Kanisa hadi mwisho wa nyakati.
Hivyo, hiyo ni Sakramenti ya huduma ya Kitume ambayo inajengwa kwa ngazi kuu tatu ambazo ni Uaskofu, Upadre na Ushemasi.
Sakramenti hiyo humfanya mpokeaji afanane na Kristo ili ahudumie kama chombo cha Kristo kwa ajili ya wokovu wake na wa kundi analokabidhiwa kwa kuwekwa wakfu kwa ajili ya kuihubiri Injili, kuwachunga waamini na kuadhimisha ibada kwa Mungu.
Kwa malengo hayo ya Kristo, Padre Mhango Thomas Mangi ni miongoni mwa chombo cha Kristo kwa Sakramenti ya Upadre katika kuadhimisha makuu ya Mungu na kumtangaza Kristo duniani.
Kwa Upadre wake amefanywa kuwa walimu wa imani kwa muunganiko na Askofu wa Jimbo la mahalia kwa msaada wa waumini na kanisa zima. 
Katika Karamu ya Mwisho, Yesu akiielezea ibada ya Sakramenti hiyo wakati alipokuwa akila pamoja na Mitume wake Kumi na Wawili ikiwa ni ishara ya urafiki uliopo kati yao na kuwapa maagizo ya kufanya katika utume wao, (Mt. 26:26–28; Lk. 22:19–20).
Ni dhahiri wakati wa karamu hiyo, Yesu aliwapa Mitume mamlaka ya kuendeleza kazi ya yake ndiyo maana baada ya kutwaa mkate, alishukuru, aliumega na kuwapa wanafunzi wake akisema “Huu ndio mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu”, vivyo hivyo baada ya kula alitwaa kikombe akisema, “Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, inayomwagika kwa ajili yenu”.
Mama Kanisa anasisitiza kuwa Mitume waliyapata mafundisho hayo Siku ya Alhamis Kuu kutoka kwa Yesu Kristo mwenyewe akiwa katika ukamilifu wake na kuweka Sakramenti ya Daraja Takatifu la Upadre.
Padre ni kiongozi wa kanisa anayehitajiwa na kundi la Mungu, ndiyo maana Mwinjili Yohane anasema kwa kinywa chake anaweza kutamka maneno ya Bwana “Mimi ni njia, ukweli na uzima. Hakuna ajaye kwa Baba ila kwa njia ya mimi” (Yoh. 14:6).
Ni mwaka wa 40 sasa kwa Padre Thomas Mangi wa Jimbo Katoliki la Singida tangu apate Daraja la Upadre Agosti 01, 1976 na miaka 71 tangu alipozaliwa 1945 ndiyo maana anamshukuru Mungu kwa mema mengi aliyomjalia.
Katika maadhimisho hayo, Padre Thomas amemshukuru Mungu na kutumia fursa hiyo kuwaasa Mapadre wawe na ari zaidi katika utume na uchungaji wao ili waweze kuwatumikia watu vizuri kwa furaha na kwa kujitoa kama Yesu Kristo alivyowatumikia watu.
Wosia huo unaendana na maneno ya Yesu Kristo mwenyewe (Yoh.10:11, Marko 10:45) “Mimi ni Mchungaji Mwema, Mchungaji Mwema hutoa maisha yake kwa ajili ya kondoo, Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”
Aidha, amewataka Mapadre wawe macho na mienendo ya ulimwengu wa utandawazi na mitandao ya kijamii isije kuwachanganya katika Uchungaji wao na wawasimamie vijana wasijewakamezwa na utandawazi.
Kwa upande wa familia ambayo ndiyo msingi wa kanisa, Padre Thomas awataka wanafamilia wawe na upendo wa kweli kuanzia kwa wazazi na watoto.
“Wanafamilia wawe watu wa sala, ndio maana familia ni msingi wa kanisa, kwa sala tutapata watu wengi kwenye miito mbalimbali ikiwemo Upandre na Ndoa” alisema Padre Thomas.
Amesema kuwa wazazi waangalie watoto wao kwa karibu na kuwakinga na ulevi, madawa ya kulevya na makundi yasiyofaa ambayo yameharibu maadili ya vijana na jamii na wawajenge kulingana na hatari na changamoto maisha zinazowakabili.  
Padre Thomas alipewa Daraja hilo na Mwasisi wa Jimbo hilo Mhashamu Askofu Bernard Mabula mnamo Agosti 01, 1976 katika kanisa la Parokia ya Itamka (kwa sasa Parokia ya Ilongero) ambapo ndipo alipoanzia kufanya kazi yake ya kichungaji hadi 1977 ambapo alihamishiwa Parokia ya Chemchem na kwa ya Mungu hadi 1978.
Mwaka 1979 hadi 1980 Askofu wa Jimbo wakati huo alimpa fursa ya kwenda kusoma masomo ya Upashanaji habari katika Chuo cha Maendeleo ya Jamii Nyegezi (NSTI).
Baada ya masomo yake alirudi Jimboni Singida na kupangiwa kufanya kazi yake ya  kichungaji katika Parokia ya Ntuntu akiwa Paroko kuanzia mwaka 1980 hadi 1989 na baada ya hapo alipangiwa Parokia ya Kiomboi akiwa Paroko Msaidizi kuanzia mwaka 1989 hadi 1997.
Mbali na kutoa huduma Parokiani, mwaka 1996, Padre Thomas alipata fursa ya kwenda nchini Israel kwa kazi mbili, ya kwanza ilikuwa ni hija Takatifu na kazi ya pili ilikwenda kwa kusoma kozi ya Biblia katika Chuo cha Mtakatifu Anna kilichopo Yerusalemu.
Baada ya hija yake nchini Israel, Padre Thomasi alipangiwa kufanya kazi katika Parokia ya Itaja kuanzia Mwaka 1997 hadi 2004 akiwa Paroko.
Kulingana na mahitaji ya Jimbo, alihamishiwa katika Chuo cha Katekesi cha Jimbo kilichopo Misuna Singida akiwa mwalimu na mlezi wa chuo hicho kuanzia mwaka 2004 hadi 2009.
Kulingana na wito wake wa kuhubiri Injili popote, Padre Thomas alihamishiwa tena Parokia ya Kiomboi kuanzaia mwaka 2009 ambapo alitoa huduma ya kichungaji hadi Agosti 11, 2016. Tarehe hiyo hiyo alihamia Parokia ya Singida ambapo anaendelea na kazi yake ya Kichungaji.  
Zaidi ya hayo, amefanya kazi mbalimbali za Kitume ndani na nje ya Jimbo Katoliki la Singida ikiwemo kuwa Mkurugenzi wa Upashanaji Habari Jimbo, Katibu wa Mikutano Baraza la Kichungaji Jimbo, Mwenyekiti na Katibu wa Umoja wa Mapadre Wazalendo Tanzania (UMAWATA), Mwenyekiti Dekania ya Singida na Mkurugenzi Katekesi Jimbo.
Kwa kutimiza majukumu yake ipasavyo anamshukuru Mungu kwa mema mengi anayomjalia, ndiyo maana anasema “Kwa Neema, Upendo na Huruma ya Mungu nimefika hapa. Nimrudishie Bwana nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?” (Zab.116:12).
Hakika Padre ni Mtumishi wa Mungu anayejitoa sadaka kwa ajili ya wokovu wa watu wa Mungu, “Kila padre ni kristo mwingine”. Ni mwanadamu kama wandamu wengine, aiyetwaliwa kati ya watu kwa mambo yamuhusuyo Mungu (Ebr. 5:1-3).
Katika utume wa Upadre, wakristo wanapaswa kufahamu kuwa Padre yupo kama Wakristo katika kipindi cha kuzaliwa kama wanadamu, katika maisha ya kila siku ya furaha na wakati wa huzuni pia, katika nyakati na sehemu muhimu za maisha ya mkristo Padre yupo, ndiyo maana Mungu amempatia Padre uwezo wa kuwatakatifuza watu.
Katika mlima wa mizeituni Kristo aliwapa Mitume wake uwezo wa kuondolea watu dhambi, kubatiza na kufundisha habari njema kwa watu wote kwa msingi huo, Padre Thomas anaendeleza wajibu huo wa Kristo ambaye ni Kiongozi wa mataifa yote.
Wanajimbo Katoliki la Singida wanamshukuru Mungu kwa kuwapa zawadi ya Padre Thomas, katika miaka yake ya Kichungaji amekuwa mwalimu na kiongozi wa mfano wa kuigwa kwa tabia yake ya uchapa kazi na kuwapenda watu wote hadi kufika hatua ya kuwaita watoto na vijana “Mzalendo” na “Mwaananchi”.
Hakika, huu no upendo wa kipekee wa kuwafanya watu wote kuwa rafiki ambao wanaweza kujifunza kutoka kwake kwa upendo mkuu alionao kwao.
Upendo huo umemsaidia kufanikiwa kuwajali anaowafundisha, hasa anapotoa mahubiri kwenye ibada anayoongoza kwa kuwavutia waumini kwa uwezo aliopewa na Mungu wa kilihusisha neno la Mungu na maisha ya kawaida, hatua hiyo imewafanya waumini kujenge tabia ya kupenda mahubiri yake yenye mvuto na hivyo kufanya ibada kuwa hai.
Katika maadhimisho hayo kumshukuru Mungu, Ibada ya Misa Takatifu imeongozwa na Askofu wa Tatu Mzalendo wa Jimbo hilo Mhashamu Askofu Edward Mapunda na kuhudhuriwa na Mapandre, Masista, viongozi mbalimbali wa Serikali, waumini na wananchi waliofurika katika Kigango ch a Mvae ambapo ndipo alipozaliwa Padre Thomas Mangi.
Askofu Mapunda alitumia maadhimisho hayo kwa kutoa neno kwa Mapadre ambapo aliwaasa watumie siku hiyo ya kumpongeza Padre Thomas kama njia ya kutafakari maisha yao ya kichungaji ili waweze kuwa wapatanishi na njia ya kuwapeleka waumini kwenye maisha ya utakatifu waweze kuwamona Mungu kupitia upadre wao.
“Nilikuwa naongea na Padre Thomas nikamuuliza, nikitaka kukuhamisha unapenda nikupange Parokia gani? Yeye alinijibu, nipangie Parokia yeyote, mimi kesho yake utanikuta hapo”. Alisema Askofu Mapunda.
Askofu Mapunda aliongeza kuwa maneno hayo ya Padre Thomas ni ya hekima ya kupenda kujituma na kufanya kazi ya Mungu mahali popote.
Ndivyo ilivyotokea Askofu Mapunda amempa uhamisho Padre  huyo kutoka Parokia ya Kiomboi na kuhamia Parokia ya Singida na ametimiza ahadi aliyomwambia Askofu wakati wa mazungumzo yao.
Hakika palipo na mafanikio, hapakosekani kuwa na changamoto, Katika utume wake Padre Thomas amesema kuwa kuna uvuguvugu wa imani ambapo waumini hawachangamkii imani yao ya Kikristo kwa kutokupokea sakramenti mbalimbali ikiwemo Kitubio na Ekaristi Takatifu, maisha ya suria, badala yake wamejikita kwenye siasa na kusahau mambo ya kanisa.
Ili kukabiliana na hali hiyo, waumini na watu wenye mapenzi mema wanapaswa kuchangamkia imani yao ya Kikristo na kutimiza yanayotakiwa na mama kanisa na Mungu.
Changamoto nyingine ni kuhusu maendeleo ya kanisa, ambapo walei wanatakiwa kushirikiana na Mapadre katika kulijenga na kutegemeza kanisa katika kutoa huduma, kusimamia na kutekeleza miradi mbalimbali kwa manufaa ya kanisa.
Jubilee ya miaka 40 ya Padre Thomas imeenda sanjari na Maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa huruma ya Mungu  uliotangazwa na Baba Mtakatifu Francisko Desemba 8, 2015 ambapo kwa namna ya pekee Mwenyezi Mungu ameonesha anavyojali na kumshirikisha mwanadamu huruma na upendo wake usiokuwa na mipaka.
Ndiyo maana katika picha yake ya kumbukumbu ya miaka 40 ya Upadre wake, Padre Thomas amenukuu Barua ya Paulo kwa Wafilipi kuwa dira yake katika utumishi wake “Nayaweza mambo yote katika yeye aniniaye nguvu” (Fil. 4:13) akionesha ni kwa msaada wa Mungu tu ndiyo ameweza kufikia hatua hiyo.
Katika kipindi chote hicho, amekuwa ni Mhudumu wa Neno la Mungu, mtoa Sakramenti za Kanisa na matendo ya huruma yanayojengwa katika msingi imara wa shughuli na mikakati ya kichungaji.
Jubilei hiyo imekuwa mwaliko kwa Padre Thomas kukumbuka kuwa, yeye ameteuliwa kati ya watu kwa ajili ya mambo matakatifu na kuwekwa wakfu ili kuwa ni chombo cha huruma ya Mungu kwa watu wake, (Mathayo. 22:14).
Ni neno jema kumshukuru Mungu kwa kuwajalia Wanasingida mema mengi katika maisha yao amabayo ni zawadi kutoka kwa Mungu na kuendelea kulibariki Jimbo la Singida ambalo linaloongozwa na Askofu Edward Mapunda ambaye ni Mwanajimbo na lina jumla ya Mapadre 76.
Mapadre 69 wanatoa huduma katika Parokia ziapatazo 24 ndani ya jimbo na wengine wanafanya kazi katika Seminari Kuu mbalimbali nchini na Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) na Mapadre wengine saba wametangulia mbele ya haki “Raha ya milele uwape Ee Bwana na Mwanga wa milele uwaangazie, wapumzike kwa amani, Amina.


Na Eleuteri Mangi, MAELEZO

Padre Thomas Mangi akipongezwa na baadhi ya Masista wanaofanya kazi za kitume katika Jimbo Katoliki la Singida wakati wa Jubilei ya miaka 40 ya Upadre kwa lengo la kumshukuru Mungu kwa mema mengi aliyomjalia katika utume wake.

Padre Patern Mangi (kulia) akipongeza Padre Thomas Mangi (kushoto) kwa kulitumikia kanisa kwa miaka 40 ya Upadre wake. Lengo la jubilee hiyo ni kumshukuru Mungu kwa mema mengi aliyomjalia Padre Thomas Mangi katika utume wake.

Baadhi ya walei wakimpongeza Padre Thomas Mangi wakati wa Jubilei ya miaka 40 ya Upadre kwa lengo la kumshukuru Mungu kwa mema mengi aliyomjalia katika utume wake.

Mmoja wa Wanafamilia ya Mzee Paulo Mangi, Cassian Patrick (kulia) akitoa zawadi kwa niaba ya familia kwa Mhashamu Baba Askofu Edward Mapunda ikiwa ni mchango wa familia katika kuwahudumia Waseminari wa Seminari Ndogo ya Mt.Patris Dung’unyi.

Mhashamu Baba Askofu Edward Mapunda akimkabidhi Gombera wa Seminari Ndogo ya Mt. Patris Dung’unyi Padre Francis Limu zawadi aliyopewa na Wanafamilia ya Mzee Paulo Mangi kama mchango wa kuwahudumia Waseminari wa Seminari Ndogo ya Mt.Patris Dung’unyi.
(Picha Gilbert Filbert, Singida).


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU