Wengi wanaopewa madaraka Tz ni dhaifu

Rais Magufuli: Vita ya uchumi ni mbaya
Askofu: Tunabadilishiwa dhahabu kwa bangili
Mwamalanga: Wabunge waliombeza Rais wasikanyage bungeni

KITENDO cha Serikali kuzuia makinikia (mchanga wa dhahabu) uliopo kwenye makontena katika Bandari ya Dar es Salaam na sehemu nyingine nchini usisafirishwe kwenda nje ya nchi na hatimaye kuchunguzwa na kubainika kuwa na madini yanayotoroshwa, ni funzo kwa Watanzania; Wamesema watu mbalimbali wakiwamo wasomi na viongozi wa dini huku Askofu Kilaini akisema, Watanzania wasishangilie kutumbuliwa kwa Profesa Muhongo.
Kutokana na hali hiyo, Rais John Magufuli, amesema Tanzania iko kwenye vita, huku akisistiza, “Vita ya uchumi ni mbaya.”
“Kwa ajili ya kazi hii muhimu ilibidi wajumbe watafutiwe ulinzi maalumu, lakini wapo watu waliojitokeza kutaka kuingilia uchunguzi huu na majina yao tunayo na wengine tunawajua,” alisema rais Magufuli muda mfupi baada ya kupokea ripoti ya kamati aliyoiunda kuchunguza makontena ya mchanga huo zaidi ya 270 yaliyokuwa yasafirishwe kwenda nje ya nchi.
Akaongeza, “Kuna mwingine anajiita profesa wakati yeye ni daktari; alipewa hela mbele ya kamera. Ninachotaka kusema kwa Watanzania ni kuwa, tupo kwenye vita na vita ya uchumi, ni mbaya sana.”
Uchunguzi wa gazeti hili kupitia mazungumzo na vyanzo mbalimbali umebaini kuwa, uchunguzi, ripoti, mapendekezo na hatua za awali zilizochukuliwa na Rais Magufuli dhidi ya walioshiriki kufanikisha hujuma hiyo dhidi ya uchumi wa Watanzania, pia vimetoa fundisho kuwa katika masuala yenye maslahi ya taifa, tofauti za itikadi za kidini na kisiasa lazima ziwekwe pembeni ili kujenga taifa imara.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, watu hao wamesema miongoni mwa mambo ambayo ni fundisho kubwa kwa Watanzania ni kuwa, umaskini wa Watanzania ni wa kujitakia kwa kuwa miongoni mwa watu wanaofanikisha utajiri wa Watanzania kuibwa na kuliwa na mkampuni ya wawekezaji wa nje,  wamo Watanzania.
Imebainika kupitia Ripoti ya Kamati aliyoiunda Rais John Magufuli kuchunguza makontena hayo ya mchanga wa dhahabu kuwa, madini mengine ya mabilioni ya fedha, yamekuwa pia yakitoroshwa kutoka Tanzania bila kujulikana.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati hiyo iliyoundwa na kufanya uchunguzi huo, Profesa Abdulkarim Mruma, madini mengine yaliyokuwa hayajulikani yenye thamani ya kati ya shilingi bilioni 129.5 na shilingi bilioni 261yalibainika katika makontena 227 yaliyokuwa yasafirishwe kwa mwezi mmoja kabla Rais hajazuia usafirishaji huo ambao baadhi ya watu waliubeza kuwa utatishia na kuwafukuza wawekezaji.
Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki Bukoba, Mhashamu Methodius Kilaini, amesema kuwa ingawa aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini kabla ya Rais kumuondoa madarakani, Profesa Sospeter Muhongo ameondoka madarakani kwa kuwajibika kwa mujibu wa nafasi yake, hapaswi kubezwa kwa kuwa naye aliikuta mikataba hiyo.
“Profesa Muhongo ametumbuliwa kuwajibika, lakini mikataba hiyo aliikuta hivyo, kutumbuliwa kwa Muhongo sio jambo la kushangilia na badala yake, tunapaswa kuibadili na hapa Rais ana kazi kubwa kuirekebisha maana tulishajifunga ipo kazi ngumu kwelikweli, lakini najua Rais yuko makini,” alisema Mhashamu Kilaini.
Alisema fundisho kubwa analoliona kwa Watanzania kutokana na sakata hili, ni kwamba Watanzania wengi wanaopewa madaraka ni dhaifu kiasi cha kudanganywa na kutumiwa kwa manufaa ya mataifa ya nje huku, wakiangamiza taifa lao jambo linalohitaji maombi zaidi kwa taifa lipate watu waadilifu na wenye uzalendo.
“Tuwe na uzalendo na tuandae watu wetu kwa ujuzi na maarifa; hii itatusaidia kuepuka watu wanaotoka Ulaya kutuletea bangili ili sisi tuwape almasi na dhahabu,” alisema.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Maadili, Amani na Haki za Binadamu kwa Jamii ya Madhehebu ya Dini Tanzania, Askofu William Mwamalanga, alisema moja ya mafunzo makubwa wanayoyapata Watanzania ni kwamba Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015, umewapa Rais ambaye ni jemadari jasiri katika kutetea wanyonge na kulinda rasilimali za nchi.
“Ndipo tunajifunza kuwa ziara nyingi za nje ya nchi kwa viongozi wakuu wa nchi sio kuwa zinaleta faida, bali mara nyingi ni hasara maana wengi wanapokwenda huko, wanakutana na magenge ya wawezekezaji wahuni yanayowapofusha na kuwafanya watumike kuroga uchumi wa nchi zao,” alisema Mwamalanga.
Ametaka Watanzania wamuunge mkono na kumtia moyo kwa kufanya maandamano ya kitaifa huku wakimwombea na kumpa tuzo.
“Rais amesisitiza kabisa na ndiyo ukweli kwamba, hii ni vita kubwa kati ya madude makubwa ya uhalifu ambayo ni zaidi ya ujambazi,” alisema.
Kiongozi huyo wa kiroho alisema kukimbiakimbia kwenda nchi za nje na kujidanganya kwa misaada, ni kuzidi kuliangamiza taifa kwa kuwa kinachotolewa na baadhi ya mataifa au wahisani, ni sehemu ndogo kati ya rasilimali wanazolipora taifa.
“Tujifunze kutokwenda nje kuomba misaada kwa kuwa ukienda, wanakupa sehemu moja kati ya 100; na 99 inayobaki, wanakupora,” alisema na kuongeza, “Huyu ni Rais wa Kwanza tangu tupate uhuru, kusimamia kwa dhati uchumi wa nchi na hapa, tunapaswa kumpa tuzo ili hata watoto wetu wajifunze maadili na kuthubutu kulitetea taifa kama anavyofanya Rais.”
Alisema kutokana na hali hiyo, mawaziri na watendaji wote waliopita katika wizara hiyo tangu mwaka 1998, wachunguzwe na kuchukuliwa hatua hususani watakaobainika kuhusika au kuzembea na kulisababishia taifa hasara.
“Hata vyama vyetu vyote vya siasa visiwe chaka la kuwaficha majambazi wanaoliangamiza taifa na ninashukuru na kumpongeza Rais Magufuli kwa kuwa ameanza kukisafisha chama chake,” alisema.
Alisema anatamani kampuni zote zilizobainika kukiuka makubaliano katika mikataba na kufanya hujuma kwa taifa, ziondolewe nchini haraka kwa kuwa ni hatari kwa taifa.
“Ninatamani kuona hata wanasiasa waliokuwa wakibeza uamuzi wa Rais wa kuzuia usafirishaji wa mchanga wa dhahabu huku wakijua wanatumikia rushwa ili kukandamiza maslahi ya taifa, wajipime wenyewe kama wanastahili kuendelea kuingia katika Bunge la Tanzania kwani wamedhihirisha walikuwa wanatetea usaliti na maangamizi kwa taifa,” alisema.
Akasema, “Wapo wabunge walikomaa kabisa kumlaumu Rais kuwa uamuzi wake kuzuia mchanga utaliathiri taifa kwa kulitia hasara na kufukuza wawekezaji… Hao, naomba hata Bunge kupitia kwa Spika, Job Ndugai, liwajadili na viundwe vyombo vya kuwachunguza walikuwa wanatetea maslahi gani kama sio kutumikia rushwa.”
“Hapa ninasema kwa nguvu kabisa kwamba, wale waliotaka kulishawishi Bunge kumuona Rais kama aliyekosea katika uamuzi wke, wajitoe au watolewe wasiendelee kuingia bungeni maana walikuwa wanafanya usaliti wanaoujua na wanaojua namna wanavyofaidi usaliti huo dhidi ya Watanzania wenzao. Nitashangaa sana kama wabunge hao wataendelea kuwa bungeni.”
Mbunge wa Kigoma Mjini, Kabwe Zitto alinukuliwa jana akiunga mkono matokeo yaliyobainishwa na kamati iliyoundwa na rais kuchunguza mchanga wa dhahabu na kusema matokeo ya utafiti huo ndio rejea sahihi kwa sasa.
“Utafiti unapingwa kwa utafiti. Kwa sasa Kamati ya Mruma (Profesa Abdulkarim Mruma- Mwenyekiti wa Kamati) ndio rejea sahihi kwenye suala la mchanga na hivyo nakubali mapendekezo yaliyomo,” alisema mbunge huyo wa upinzani aliyewahi kuwamo katika moja ya Tume za kuchunguza mikataba ya sekta ya madini nchini.
Naye Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Dk Alex Malasusa alisema ripoti hiyo inapaswa kuwafumbua macho Watanzania katika sekta mbalimbali.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana kwa upande wake anasema, funzo tunalopata Watanzania ni ukweli kwamba tumekuwa tukiwanyenyekea wawekezaji huku wakitunyonya na alichokifanya Rais ni jambo jipya na la manufaa na linalopaswa kuungwa mkono na Watanzania wote.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU