Hija nchi Takatifu 2017 yafana







θ Mapadri wahamasishwa kushiriki kwa wingi

ASKOFU, mapadri 51, watawa na walei wamefanya safari ya Hija katika nchi Takatifu, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Jubilei ya miaka 100 tangu Padri mzalendo wa kwanza kupewa daraja hilo Tanzania Bara.
Kundi hilo lililokuwa na mahujaji zaidi ya 90 kutoka majimbo 15 nchini lilianzia safari yake nchini Misri likiwa limedhamiria kuifuata njia ya Wana wa Israel kutoka Misri kwenda nchi ya ahadi.
Kundi hilo liliambatana na Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa Mhashamu Bernadini Mfumbusa ambaye pamoja na mapadri wengine 19 mwaka huu wanaadhimisha Jubilei ya miaka 25 ya utumishi katika shamba la Bwana.
Mahujaji hao waliowasili nchini Misri tarehe 9 April 2017 waliweza kutembelea Kanisa la Familia Takatifu ambapo kwa mujibu wa mapokeo Yesu, Bikira Maria, na Mtakatifu Yosefu waliishi hapo kwa miaka 3 kama wakimbizi kufuatia tishio la Mfalme Herode kutaka kumwua mtoto Yesu.
Aidha mahujaji hao waliweza kubadilishana mawazo na wakristo wa madhehebu ya Kikoptic ambao wamekuwa ni kielelezo cha mateso ya wakristo karne hii katika nchi yao yanayotokana na imani yao. Mahujaji hao waliweza kutembelea piramidi za mjini Kairo zilizo Gaza nchini humo ikiwa ni moja ya vielelezo juu ya mateso waliyoyapata Waana wa Israeli wakati wakiwa utumwani Misri.
Kundi hilo la Mahujaji lilisafiri kuelekea Mlima Sinai ikiwa ni hatua ya pili katika safari hiyo ambapo pamoja na kupanda Mlima Sinai waliweza kutembelea Monastery ya Mtakatifu Katarina.
Mapokeo yanaeleza kuwa hapo ni mahali ambapo Musa aliweza kushuhudia kichaka kinachowaka moto bila kuteketea. Wakiwa njiani waliweza kusimama mahali ambapo pia kwa kadri ya mapokeo ndipo ambapo Mungu aliwavusha Waisrael katika bahari ya Shamu.
Pamoja na kutembelea mji wa kihistoria wa Petra nchini Yordani mahujaji waliweza kuona mlima Nebo mahali ambapo Musa kadri ya maandiko alionyeshwa Nchi Takatifu, nchi ya ahadi kabla ya kufa.
Nchini Israel mahujaji hao walipiga kambi katika mji mdogo wa Bethlehemu, mahali ambapo Kristo alizaliwa. Sehemu hiyo ya tatu ya ziara iliwafikisha sehemu zote kuu katika historia ya maisha ya Yesu kadri ya maandiko tangu kuzaliwa, kufundisha, kufanya miujiza, kuteswa hadi kifo chake.
 Padri Wenceslaus Kayera wa Jimbo Katoliki Ifakara, mmoja wa Wajubilei wa miaka 25 ya utumishi anakumbuka jinsi alivyoweza kusubiri kwa zaidi ya masaa matatu ili aweze kulifikia Kaburi la Yesu kutokana na uwingi wa watu kwenye foleni.
Mahujaji hao walipata bahati ya kuadhimisha sadaka ya Misa Takatifu katika mlima ujulikanao sasa kama Mlima wa Heri (Beatitudes –Mt 5:1-12) na baadhi ya mahujaji walipata pia nafasi ya kurudia ahadi zao za ndoa mjini Kana mahali ambapo Kristo alifanya muujiza wake wa kwanza.
Siku ya mwisho kabla ya kurudi nyumbani mahujaji hao waliweza kutembelea mlima Sayuni, mahali ambapo panaaminika kuwa ndipo Hekalu la kwanza lilijengwa.
Hekalu hilo kwa sasa halipo na mahali pake pamejengwa Msikiti ujulikanao kama Dome of the Rock. Wayahudi hujikusanya na kusali wakielekea moja ya kuta za uzio wa Hekalu zilizosalia wakisali na wakiamini kuwa siku moja Hekalu lao litajengwa tena.
Baadhi ya mahujaji walizungumza na gazeti hili walionyesha furaha yao hasa kutokana na mlinganisho wa yale waliyokuwa wakisoma katika maandiko na uhalisia wake waliouona katika safari hiyo. Aidha waliomba kuwa iwepo mipango maalumu kwa Wakatoliki kuwa wanatembelea maeneo hayo mara kwa mara kadri ya nafasi.
Naye Askofu Bernadini Mfumbusa katika kuhitimisha ziara hiyo alisema kuwa ingekuwa ni jambo jema kama mapadri wengi wanapata nafasi ya kutembelea nchi hizo tatu, ikiwa ni kukamilisha yale ambayo wamejifunza wakiwa mashuleni.
 Safari hii iliandaliwa vyema na kampuni ya Cordial Tours ya mjini Dar es Salaam na kuratibiwa na Mapadri Wanajubilei wa miaka 25  nchini.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU