“Majimbo yote yawe na tovuti”

 KURUGENZI ya Mawasiliano ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) imeshauriwa kuhimiza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano katika majimbo yote ili kuweza kuwafikia watu wengi zaidi na kupanua wigo wa Mawasiliano.
Akizungumza na wakurugenzi wa Mawasiliano Jamii kutoka baadhi ya majimbo Katoliki Tanzania katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino (SAUT) kwenye Semina juu ya matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama), pia mbinu za Mawasiliano, Mratibu wa Mawasiliano Jamii wa Umoja wa Wanachama Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati (AMECEA) Padri Chrisantus Ndaga amesema Kanisa Katoliki bado lina changamoto katika matumizi ya mitandao ya kijamii hususani tovuti za majimbo.
Padri Ndaga ameyashauri majimbo yote Katoliki nchini Tanzania kufungua tovuti na mitandao mingine ya kijamii ili kutanua wigo wa Mawasiliano ndani na nje ya majimbo wakati akiwahimiza wakurugenzi wa Idara za Mawasiliano Jamii majimboni kuwaendeleza kitaaluma wasimamizi wa Idara hizo ili waendane na teknolojia ya kisasa katika upashanaji habari.
Padri Ndaga amesema kuwa majimbo mengi ya Kanisa Katoliki Tanzania hayajazama katika matumizi ya tovuti (website) na baadhi ya majimbo yamefungua tovuti hizi lakini hayana wataalamu wenye weledi wa kuzisimamia tovuti hizo pia kuweka habari zinazoendana na muda.
Aidha amesema AMECEA na TEC wamejipanga kuwaelimisha mapadri, watawa na walei walio katika tasnia ya habari ili wapate maarifa yatakayowawezesha kutumia mitandao yote ya kijamii ikiwemo ‘whatsap’, ‘facebook’, tweeter’, ‘instagram’ na blogu ambapo kwa sasa kuna jamii kubwa ya watanzania hususani vijana ambao wanaweza kuinjilishwa katika uinjilishaji mpya.
Wakichangia maoni yao katika semina hiyo, washiriki toka majimbo mbalimbali wameipongeza AMECEA na TEC kuona hitaji la kuyahamasisha majimbo kutumia Tehama na redio kwani wapo watanzania wengi hawaendi kanisani lakini wanasikiliza sana redio na kufuatilia mitandao ya kijamii.
Semina hiyo imeandaliwa na Idara ya Mawasiliano ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) kwa udhamini wa AMECEA na kuhudhuriwa na wakurugenzi wa Mawasiliano kutoka majimbo ya Dar Es Salaam, Mwanza, Shinyanga, Geita, Njombe, Arusha, Tanga, Tabora, na baadhi ya wawezeshaji  kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi.
Aidha Mratibu wa Mawasiliano wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Bw. Bernard James ameshangazwa na baadhi ya wasimamizi wa Mawasiliano majimboni kushindwa kuandika habari zinazowagusa wakristo na wananchi na hivyo kufanya habari za jitihada mbalimbali nzuri zinazofanywa na majimbo kuisaidia serikali kutoa huduma za kijamii hasa elimu, afya, maji na ujenzi wa miundombinu kutoifikia jamii.
Bwana Bernard amewaomba wakurugenzi wa Mawasiliano kutoka majimboni kuhamasisha habari toka majimboni ziandikwe kwa wingi, na kuunda mfumo mzuri wa usambazaji ili kuliwezesha gazeti hili lifike katika kila Parokia ili waamini wengi wanufaike na gazeti hilo.


Na Salvatory Magangila na Veronica Modest, Mwanza









Comments

  1. wazo zuri sana websites hizo ziwe na matukio yote ya jimbo na pia wakumbuke ku update hizo websites kila siku maana ukiingia website ya jimkoo la dsm ni kituko yani ni kaka imekufa na wana idara ya teknolojia habari na mawasiliano

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU