Talaka Kanisa Katoliki hapana


Na Sarah Pelaji

TUME ya Sheria za Kanisa ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) imefanya ufupisho wa Barua ya Kitume Mitis Iudex Dominus Iesus (The Gentle Judge, Our Lord Jesus) ya Baba Mtakatifu Fransisko ya Agosti 15 mwaka 2015 ambayo ilifanya mabadiliko katika kanuni zinazohusiana na mwenendo wa kesi za utangazaji batili wa ndoa
Hayo yameelezwa hivi karibuni na Katibu Mtendaji wa Tume hiyo Padri Henry Mchamungu, mwalimu katika Seminari ya Mtakatifu Karoli Lwanga Segerea jijini Dar es Salaam ambaye ni mjumbe katika Tume ya Sheria za Kanisa nchini akieleza kuwa mabadiliko katika kanuni zinazohusiana na mwenendo wa kesi za utangazaji batili wa ndoa ni vyema Maaskofu pamoja na Mavikari Hakimu (Judicial Vicars) kufahamu ili waweze kushughulikia kesi za ndoa ipasavyo.
Aidha Tume hiyo inayoongozwa na Mwenyekiti wake Askofu Rogathy Kimaryo na Makamu Mwenyekiti Askofu Michael Msonganzila, wameoanisha baadhi ya mambo ya kimsingi ya  kuzingatia katika barua hiyo kuwa ni pamoja na Hukumu moja ya ubatili wa ndoa inayotolewa na mahakama ya ngazi ya mwanzo inajitosheleza. Haihitaji tena kufanyiwa mapitio na mahakama ya ngazi ya pili na mengine.
Kutokana na Barua hii ya kitume ya Papa Fransisko, haimaanishi kuwa Baba Mtakatifu ameruhusu talaka, bali amefanya marekebisho kidogo kwenye kanoni zinazohusiana na mwenendo wa kesi za utangazaji batili wa ndoa. Kanoni ambazo Baba Mtakatifu amezifanyia marekebisho, zimekuwepo tangu Mkusanyo wa Sheria Kanoni (Code of Canon Law) ulipotangazwa na Baba Mtakatifu Yohani Paulo II mwaka 1983.
Amenipa, Kanisa linatambua waziwazi uwezekano wa kuwepo ndoa ambazo zinafungwa kibatili, na ndiyo maana limeweka kanoni zinazotawala mchakato wa kutangaza batili ndoa hizo. Ili ndoa iwe halali, lazima mambo makuu matatu yazingatiwe: a) Ubadilishanaji wa Ukubali wa Ndoa kati ya Wafunga ndoa wenyewe, b) Kutokuwepo kwa Kizuizi cha Ndoa, na c) Uzingatiaji wa Utaratibu Kanoni.
Amesema kuwa, endapo ndoa itafungwa huku mmojawapo wa wafunga ndoa hayupo au mwakilishi wake ili kubadilishana ukubali wa ndoa, au kuna kizuizi cha ndoa na hakikuondolewa na mtawala mahalia, au utaratibu kanoni hauzingatiwi, basi ndoa hiyo huwa ni batili.
Kanisa limeweka utaratibu wa kutangaza batili ndoa kama hizo. Ndoa inapotangazwa batili ina maana kuwa ndoa inatangazwa kuwa haikuwepo tangu mwanzo, na wala haimaanishi Hakimu mmoja chini ya mamlaka ya Askofu: Katika ngazi ya mwanzo, Askofu ndiye mwenye mamlaka ya kumteua hakimu ambaye anapaswa kuwa mklero.
 Mkusanyo wa Sheria Kanuni unaeleza kuwa kesi inayohusu utangazaji batili wa ndoa iamuliwe na jopo la mahakimu watatu (rejea Kan. 1425, §1 na Mitis Iudex Dominus Iesus, Kan. 1673, §3). Hakimu ambaye ni mklero lazima asimamie jopo hili, lakini mahakimu wengine wanaweza kuwa walei. Katika jopo hili la mahakimu, kura ya wengi inahitajika ili ndoa ipate kutangazwa batili.
Hata hivyo kutokana na upungufu mkubwa wa wanasheria kanuni na hivyo kuwa vigumu kuanzia mahakama yenye jopo la mahakimu watatu, Baraza la Maaskofu linaweza kumruhusu Askofu aaminishe kesi za ndoa kwa hakimu mmoja, ambaye anapaswa kuwa mklero (rejea MSK, kan. 1425, §4).
Kwa kuwa mchakato wa kesi za utangazaji ubatili wa ndoa mara nyingi umechukua muda mrefu, ndiyo maana Baba Mtakatifu Fransisko amefanyia mabadiliko kanoni husika, ili mchakato uende kwa kasi zaidi.
Kwa mfano, hukumu inayotolewa na mahakama ya ngazi ya mwanzo inajitosheleza, haihitaji tena kufanyiwa mapitio na mahakama ya ngazi ya pili. Kwa namna hii, mchakato umefupishwa.
Aidha, Baba Mtakatifu ameyataka Mabaraza ya Maaskofu yawasaidie maaskofu kuangalia ni jinsi gani ya kuchangia gharama za mahakama ili kupunguza mzigo kwa waamini wenye kesi za ndoa, na pale inapowezekana michakato ya kesi za ndoa ifanyike bila ya kuwatoza chochote wenye kesi.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU