Kijana akaa kitandani miezi 9 akikisubiri kifo

 Natamani hata siku moja niweze kukaa au kutambaa hata kujigeuza mwenyewe kitandani, sina fedha ya matibabu wala ndugu wa kunisaidia, Watanzania nisaidieni.”
Ni sauti ya kijana Ayubu Julias inayoibua hisia za huzuni na masononeko juu ya maisha yake  anavyoteseka kitandani kwa kukosa matibabu  na kupoteza matumaini na ndoto zake baada ya kupatwa na ajali iliyosababisha kupooza mwili na kukosa matibabu.
Ayubu ni kijana mwenye umri wa miaka 30 anaishi katika kijiji cha Baibo, kata ya Msua Manispaa ya Sumbawanga na anapaza kilio chake kwa watanzania aweze kusaidiwa kutokana na kukosa pesa za matibabu baada ya kuteguka uti wa mgongo na amekuwa mtu wa kulala kitandani na kugeuzwa kwa zaidi ya miezi 9 sasa.
Gazeti la kiongozi limemtembelea Ayubu nyumbani kwao na kufanya nae mazungumzo ambapo kwa masikitiko makubwa  Ayubu anaeleza historia ya maisha yake na kuomba msaada kwa watanzania na watu wote walio na moyo wa kumsaidia. Na anaanza kwa kusema:
“Ndugu yangu, nasubiri miujiza ya mungu tu!! Maana kama aliweza kuyatenda haya kwa Ayubu wa nchi ya Usi niliebatizwa kwa jina lake ambaye alikuwa mkamilifu na kumcha Mungu.”
“Naitwa Ayubu Julias Simchindo, nina umri wa miaka 30 nimezaliwa wilayani Chunya mkoani Mbeya. Nimelelewa zaidi na baba yangu mzazi kwani mama yangu alifariki nikiwa na umri wa miaka miwili tu hivyo sikuweza kuyashiba mapenzi na malezi ya mama katika utoto wangu.” Anaeleza kijana huyu.
“Baba yangu alikuwa akijihusisha na ujasiliamali wa kufanya biashara ndogondogo zaidi alijishughulisha na uvuvi wa  samaki ambapo alikuja Mkoani Rukwa kuvua na kupeleka samaki Mbeya ambapo mnamo mwaka 1995 alituhamishia makazi katika mji wa Tunduma ambapo alitupangia nyumba mimi pamoja na dada yangu na tukawa wakazi wa Tunduma kwa muda ambapo  baba alikua akija kutuona kila baada ya mwezi mmoja au zaidi.
 Mnamo mwaka 1996 ilikuwa ndio ukomo wa baba yetu kuja kutuona  na ikawa ni mwisho wetu kuiona sura ya baba machoni petu maana mpaka leo hii simjui baba wala hatujui ni wapi alipopotelea, ni mzima au marehemu sijui ila limebaki ni fumbo lisilo na majibu.
Namshukuru mama mwenye nyumba tulipokuwa tukiishi ambapo alitambua kama tumetelekezwa na akaamua kutufanya ni wanae na kuanza kuishi kama watoto wa pale na si wapangaji tena ambapo mama huyu aliamua kututafutia ndugu zetu na kubaini kuwa asili ya baba yetu mzazi ni Rukwa maeneo  ya Karuko ambapo aliweza kumpata baba yetu mkubwa na kutukabidhi kwake ingawa dada yangu alibaki Tunduma kwani aliolewa huko ndipo nilipotambua ukoo wetu.
Haikupita muda mrefu baba yangu mkubwa alifariki dunia lakini mwanae mkubwa ambaye ni kaka yangu alinichukua na kuanza kuishi nae maeneo ya Majengo Manispaa ya Sumbawanga ambapo nikiwa na miaka 13 mnamo mwaka 2000 aliniandikisha shule ya msingi Jangwani ambapo baadaye waliigawa shule zikawa shule mbili nyingine ikiitwa Kiweru hivyo nilihitimu katika shule ya msingi Kiweru.
 Nilihitimu, nikafaulu na kuchaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari katika shule ya Kizwite Sekondari Manispaa ya Sumbawanga ambapo nilihitimu kidato cha nne mwaka 2010, hata hivyo sikuweza kufanya vizuri katika masomo yangu ambapo nilianza maisha mapya ya utafutaji.
Baada ya kuhitimu elimu ya sekondari, nilianza kuishi na mama yangu mkubwa ambaye baba yangu mkubwa alimuacha na kuanza kumsaidia baadhi ya kazi na mahitaji madogomadogo kwani amekuwa hajiwezi.
 Nilianza kujishughulisha na biashara ya kuuza karanga na baadaye kuuza picha kubwa za ukutani kama vile za Yesu, wasanii, timu za mpira na nyinginezo ambazo ziliweza kuniingizia kipato na kuweza kuendesha maisha yangu.
Nilianza kupeleka bidhaa zangu za picha katika maeneo ya minada mbalimbali ambapo mafanikio yalizidi kunitia faraja na nilianza kujikimu mimi na mama yangu mkubwa na nikaanza kufikiri maisha ya kutafuta mwenza wa maisha yangu.
“Looo! Mipango si matumizi na binadamu unapanga lako kumbe Mungu nae ana makusudi juu yako, ilikua ni tarehe 17/ 07 /2016 ambapo ndoto zangu za maisha zilizima na mpaka sasa najiozea huku najiona.” Anaeleza Ayubu huku machozi yakimbubujika.
Tulikuwa tukitokea kipande Sumbawanga Manispaa tunaelekea wilayani Nkasi kijiji cha Kirando tulipopatwa na ajali mbaya sana ya gari ambapo binafsi nilipoteza fahamu na baada ya kurejea katika hali ya kujitambua nikiwa hospitali ya mkoa wa Rukwa  nilijikuta siwezi kuinuka, kutembea, kutambaa, kukaa wala kujigeuza kwani sehemu ya mwili wangu  kuanzia miguuni hadi kiunoni hakukuwa na mawasiliano tena mpaka leo ambapo nasubiri miujiza ya Mungu na katika ajali ile mmoja wetu alipoteza maisha palepale na 40 tulikuwa majeruhi ingawa mimi ndio nilikuwa muathirika mkubwa zaidi.
Mganga Mkuu wa hospitali ya mkoa wa Rukwa alisema kuwa hakuna uwezekano wa kimatibabu wa kunisaidia kurejea  katika hali ya kawaida na kushauri nipelekwe Muhimbili  ambapo nawashukuru wafanyabiashara wa mnadani waliweza kunichangia nauli na kufanikisha kupelekwa Muhimbili kwa ajili ya matibabu.
Baada ya kufika kule nilipigwa xray, na sitscanner ambapo sikuweza kufanyiwa upasuaji wowote kwani kuna kidonda ambacho kipo maeneo ya uti wa mgongo na badala yake kupumzishwa wodini na kutakiwa kuponesha vidonda ndipo nifanyiwe upasuaji kwa baadaye na wakanitaka nirudi nyumbani  mpaka  tarehe 28/11/2016 kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji na matibabu mengine.
Sijaweza tena kurudi kwenye matibabu wala upasuaji kwa sababu sina fedha wala mama yangu hana fedha ya kunisafirisha kwenda Muhimbili hata masharti ya chakula niliyopewa imekuwa ni changamoto maana  hana uwezo wa kunihudumia naye anasumbuliwa na ugonjwa wa Athma kwa muda sasa wala hana uwezo wa kuzalisha anasubiri misaada ya watu na ndugu ndipo anihudumie, na wakati mwingine nadhani Mungu atende analoliweza juu yangu,” Anasema Ayubu na kuongeza kuwa;
“Natamani hata siku moja niweze kukaa au kutambaa hata kujigeuza mwenyewe kitandani lakini nahisi ni ndoto za mchana kwani gharama za matibabu na nauli ya kunifanikisha kufika Muhimbili ni zaidi ya 2,000,000 ambapo sina hata ndugu mwenye uwezo wa kunisaidia, hivyo nipo naoza bila kujua hatima ya maisha yangu ingawa najihisi vichomi sehemu ya miguu yangu tofauti na nilivyokuwa mwanzo.”
Kijana  Ayubu anahudumiwa na mama yake mkubwa ambaye naYe amekwisha kuzeeka huku naye akisumbuliwa na Athma wakishirikiana na dada yake.
Na anahitaji msaada wa hali na mali ili kuweza kumsaidia kupata matibabu angalau aweze hata kukaa au kujigeuza mwenyewe na kujihudimia katika huduma za haja, kwani kwa  zaidi ya miezi 9 sasa amekuwa ni mtu wa kulala kifudifudi tu na hajui hatima yake katika kupata matibabu.

Kwa maelezo au msaada wowote wasiliana na dada yake kwa simu namba. 0758216017


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU