Mwalimu Mkuu asakwa akituhumiwa kusababisha kifo cha mwanafunzi Mbeya

Thompson Mpanji, Mbeya

JESHI la Polisi mkoani Mbeya linamsaka Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Matwiga iliyopo katika Kijiji na Kata ya Matwiga, Tarafa ya Kipembawe, Wilaya ya Chunya Mkoa wa Mbeya  Scola Mwasaga [38] kwa tuhuma za kusababisha kifo cha mwanafunzi  wa darasa la kwanza  baada ya kudaiwa kumfungia katika kasiki ya kutunzia mitihani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Naibu Kamishna wa Polisi Dhahiri Kidavashari amesema tukio hilo limetokea Mei 8 majira ya saa 4:30 asubuhi katika Kata ya Matwiga, Tarafa ya Kipembawe, Wilaya ya Chunya Mkoa wa Mbeya ambapo mwanafunzi  aliyefahamika kwa jina la Daud Kaila [11] alifariki dunia muda mfupi baada ya kufikishwa katika Zahanati ya Matwiga.
Kamanda Kidavashari  amesema kuwa awali inadaiwa kuwa marehemu alifikishwa shuleni hapo majira ya saa 4:00 asubuhi na baba yake mzazi aitwaye Jordan Kaila [43] Mkazi wa Matwiga kutokana na kuwa mtoro kwa mwezi mmoja na nusu na ndipo Mwalimu  huyo alimuamuru Baba wa mwanafunzi huyo amchape viboko vitatu makalioni  na alitekeleza adhabu hiyo.
Kamanda huyo amefafanua kuwa mara baada ya adhabu hiyo, Mwalimu Mkuu alimfungia mwanafunzi huyo pamoja na mwanafunzi mwingine ambaye ni mtoro aliyefahamika kwa jina la Felix Samweli [13] mwanafunzi wa darasa la 4 kwenye kasiki ya kutunzia mitihani iliyopo ofisini kwake.
“Baada ya muda mfupi kupita na kasiki kufunguliwa, mwanafunzi huyo wa darasa la kwanza alikuwa hawezi kupumua vizuri pamoja na mwenzake hali iliyosababisha kukimbizwa katika Zahanati ya kijiji kwa ajili ya kupatiwa matibabu lakini ilibainika kuwa Daud  amepoteza maisha,” amefafanua Kamanda huyo.
Naibu Kamishna wa Polisi Kidavashari  amebainisha kuwa Mwanafunzi mwenzake alipata huduma ya kwanza na kurejea katika hali yake ya  kawaida ambapo kutokana na tukio hilo, Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo Scola alikimbia na msako unaendelea na kwamba chanzo cha kifo ni kukosa hewa na upelelezi unaendelea.
Kamanda Kidavashari ametoa wito kwa walimu, wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kuepuka kutoa adhabu kali kwa watoto wadogo kwani zinaweza kusababisha madhara makubwa ikiwa ni pamoja na kifo na kushauri kutoa adhabu zitakazowafundisha watoto na kuwajenga katika misingi na ustawi mzuri katika makuzi yao huku akiomba jamii kuendelea kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu ili wakamatwe na kufikishwa katika vyombo vya dola kwa hatua zaidi za kisheria.
Wakati huo huo, Jeshi  hilo limefanikiwa  kuwakamata wahamiaji haramu 43 raia kutoka nchini Ethiopia  wakiwa kwenye gari lenye namba za usajili T.155 AZU aina ya Toyota Canter, wilayani Mbarali, mkoani Mbeya na kwamba dereva wa gari lililowabeba raia hao  aliyefahamika kwa jina la Zakayo Elias, mkazi wa Makambako alikimbia baada ya tukio hilo na juhudi za kumtafuta zinaendelea
Katika tukio jingine, Jeshi hilo limefanikiwa kumkamata mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Julius Mathias [28] Mkazi wa Uyole akiwa na Bhangi kete 11 sawa na uzito wa gramu 55.
Kamanda Kidavashari  amesema  tukio hilo limetokea Mei 8 mwaka huu majira ya saa 4:00 usiku huko Stendi Kuu ya Uyole, Kata ya Igawilo, Tarafa ya Iyunga, mkoani Mbeya  baada  ya askari kufanya  msako na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo  ambaye amedai ni muuzaji na mtumiaji wa bhangi na atafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU