Mapinduzi makubwa kwenye muziki mtakatifu kufanyika



Na Pascal Mwanache, Dar


θ Katiba ya kwaya Taifa mbioni kukamilika
θ Bodi ya walimu wa muziki wa Kanisa kuundwa


Katika jitihada za kutunza hadhi ya muziki mtakatifu wa kanisa, mapinduzi makubwa yanatarajiwa kufanyika ikiwa ni pamoja na uundwaji wa katiba ya kwaya ya taifa, uundwaji wa bodi ya muziki wa Kanisa na uwepo wa tovuti maalum kwa ajili ya kukusanya nyimbo zilizopitishwa kwa ajili ya matumizi ya kiliturujia.
Hayo ni baadhi ya maazimio ya Kamati ya Taifa ya Muziki Mtakatifu kupitia Kamati ya Taifa ya Liturujia, ambapo kwa muda mrefu zimekutana kutathmini hali ya kupungua kwa hadhi ya muziki mtakatifu kutokana na watunzi na wanakwaya kuwa na uelewa mdogo wa teolojia na elimu ya muziki huo.
Katika mkutano wao hivi karibuni, wajumbe wa kamati ya muziki mtakatifu wamepitia rasimu ya katiba ya kwaya ya taifa, ambayo ndani yake inataja uundwaji wa bodi ya walimu wa muziki ya Taifa ambayo pamoja na mambo mengine itahusika kuratibu mambo yanayohusu walimu na ualimu wa muziki wa Kanisa.

Kiini cha mapinduzi hayo
Akifungua rasmi mkutano huo, Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara na Mwenyekiti wa Idara ya Liturujia ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Mhashamu Salutaris Libena amesema kuwa muziki mtakatifu kama moja ya nguzo 10 za liturujia umevamiwa kiasi cha kuhatarisha utakatifu wake, hivyo ni lazima jitihada za makusudi zifanyike kuunusuru muziki huo.
“Muziki wetu ni lazima uwe mtakatifu kwa sababu ni sehemu ya liturujia. Tangu zamani mafundisho mengi yamewekwa kwenye muziki. Hii itukumbushe kuwa sisi tumeitwa na kutumwa kuinjilisha na kutakatifuza, tuweze kuwagusa watu ili wamgeukie Mungu. Lakini kwa sasa uwanja wa muziki mtakatifu umevamiwa sana, ikiwa ni mbinu za shetani kushambulia yaliyo mema. Lazima vita hii tuishinde” amesema Askofu Libena.
Aidha Askofu Libena ambaye aliongoza mkutano huo, ametaja baadhi ya changamoto zinazoukabili muziki mtakatifu kwa sasa kuwa ni pamoja na wanakwaya kutoelewa ni nini utume wao, wanakwaya kutoshiriki kikamilifu Sakramenti mbalimbali hasa Ekaristi Takatifu, kuimba nyimbo kwa nia ya kuburudisha badala ya kuinjilisha.
“Biblia ina maneno mengi na mazuri, lakini ajabu watunzi wanatumia maneno ya mtaani, ninyi watunzi maneno yenu mnayatoa wapi? Mnatunga nyimbo zenu mkiwa katika hali gani na mkiwa wapi? Unafika muda wa kukomunika wanakwaya wamekaa tu wanaimba. Tunapomtumikia Mungu vizuri tunatekeleza kile alichotuitia, ole wetu tusipoihubiri Injili” ameongeza.

Rasimu ya Katiba ya Kwaya ya Taifa yawasilishwa
Katika jitihada za kuepukana na changamoto zinazoukabili muziki mtakatifu, Kamati ya Muziki Mtakatifu ya Taifa iliazimia kuandaa rasimu ambayo itakuwa katiba na kutumika kwa kwaya zote nchini. Mchakato wa kuandaa rasimu hiyo ulianza mwaka 2016 ambapo kamati maalum iliyojumuisha watafiti, wataalamu wa muziki wa Kanisa, Wanasheria wa Kanisa, mapadri na watawa na wataalamu wa sayansi ya jamii iliundwa na kuanza kazi yake.
“Rasimu pia inapendekeza kuundwa kwa Bodi ya walimu wa Muziki wa Kanisa, ambayo itafanya kazi ya kuratibu masuala yanayohusu walimu na ualimu. Pamoja na kazi nyingine, bodi hiyo itaamua ili mtu aitwe mwalimu wa muziki wa Kanisa anatarajiwa awe namna gani. Pia itahusika kuratibu na kuandaa madarasa ya Muziki Mtakatifu kadiri ya silabasi ya Baraza la Maaskofu” ameeleza Bernadin Mukasa, mmoja wa wajumbe walioshiriki kuaandaa rasimu hiyo.
Rasimu hiyo inapendekeza kuwa na Utume wa Kwaya Katoliki Tanzania (UKWAKATA), huku ikipendekeza somo wa utume huo akiwa ni Mtakatifu Sesilia, na salamu itakayotumika ni ‘Tumwimbie Bwana: Katika Roho na kweli’.

Swahili Music Notes kuwa mali ya Kanisa
Katika hatua nyingine ya kuendelea kuupa hadhi yake muziki mtakatifu, kamati ya muziki pia imeafikiana kuifanya tovuti yenye mkusanyiko wa nyimbo mbalimbali za kanisa inayojulikana kama Swahili music notes, kuwa chini ya usimamizi wa kanisa, ili kuboresha yanayofanywa na tovuti hiyo.
Askofu Libena ameeleza kuwa utayari wa mwanzilishi wa tovuti hiyo kuikabidhi kwa Kanisa utasaidia uhakiki wa kila wimbo utakaoingizwa katika tovuti hiyo pamoja na zile zilizopo ili kuepusha makosa ya kiteolojia yaliyomo.
Kwa upande wake mwanzilishi wa tovuti hiyo, Bw. Terence Silonda amesema kuwa analikabidhi Kanisa tovuti hiyo ili kazi ya uinjilishaji kupitia muziki mtakatifu ifuate mtiririko wa kiliturujia unaokubalika na Kanisa Katoliki.

Comments

  1. Nawapongeza sana kwa utayari huo wa kuanziasha mapinduzi katika MUZIKI MTAKATIFU,
    maana wanakwaya wengi hujiimbia tuu waonavyo inafaa.

    ReplyDelete
  2. Vyema sana. Muhimu ni kuwa maendeleo haya yasifunge milango kwa kizazi cha wanamuziki wanaojifunza kiwapa nafasi ya kukua.

    Mungu atubariki

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU