“Himizeni watoto wasome seminari” mapadri waaswa




Askofu wa jimbo Katoliki Kahama, Mhashamu Ludovick Minde amewataka mapadri kuhakikisha wanawasaidia watoto kutoka kila parokia wajiunge katika seminari ya Ushirombo iliyopo jimboni hapa kwa lengo la kukuza miito ndani ya Kanisa.
Askofu Minde ametoa wito huo alipokuwa akibariki na kufungua rasmi shule na nyumba ya watawa katika parokia ya Mtakatifu Fransisko wa Sale, Isaka jimboni hapa na kutoa wito kwa mapadri kuwasaidia watoto wenye nia wasome seminari.
Amesema katika kila parokia wamekuwepo watoto wenye nia ya kujiunga kusoma seminari lakini wamekuwa wakikosa msaada hivyo amewataka mapadri kwa kushirikiana na wazazi na walezi kuwasaidia kuhakikisha wanakwenda kusoma seminarini hapo.
 Askofu Minde amesema parokia zote 23 zilizopo jimboni Kahama zihakikishe zinakuwa na watoto wanaojiunga kusoma katika Seminari hiyo iliyopo katika Parokia ya Mama Bikira Msaada wa Daima, Ushirombo kwa kuwasaidia mapadri.
“Elimu ni moja ya zawadi  kubwa  kutoka kwa Mungu, hivyo lazima wazazi na walezi kwa kushirikiana na Kanisa kuhakikisha watoto wanapewa elimu  na malezi bora na kuwasaidia wakue katika maadili mema,” amefafanua
 Askofu Minde amesema elimu ni sehemu ya uchungaji, ni lazima mapadri wawasaidie watoto katika kila parokia wenye nia ya kwenda kujiunga katika shule hiyo ya seminari kusoma hapo kwa lengo la kukuza miito mbalimbali ndani ya Kanisa.
Parokia ya Fransisko wa Sale, Isaka imepata watawa wa shirika  la Masista wainjilishaji wa Bikira Maria watakaofanya kazi ya utume hapo baada ya kukamilika kwa nyumba yao na pia watakuwa walezi na kuwafundisha watoto katika shule ya mwenye heri Askofu Fulton Sheen English Medium Primary School.
Katika mahubiri yake aliyoyatoa wakati wa misa baada ya kubariki  na  kufungua  rasmi shule na nyumba ya watawa, Askofu Minde amewataka watawa watakaofanya kazi ya utume wao hapo kufanya kazi  kwa furaha na matumaini  huku wakimkazia macho Yesu Kristo kwa upendo na jamii yote.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU