CARITAS Mbeya watakiwa kuwa mfano katika kuitumikia jamii

WAFANYAKAZI wa Idara ya Caritas na Maendeleo, Jimbo Katoliki Mbeya wametakiwa kuwa mfano wa kuigwa katika kutenda na kuyaishi maisha mema katika jamii kama wanavyoonekana katika maeneo yao ya utendaji kazi.
Ushauri huo umetolewa na Mkurugenzi wa Idara ya Caritas na Maendeleo, Jimbo Katoliki Mbeya, Edgar Mangasila wakati wa hafla fupi ya kukabidhi zawadi na kuwapongeza wafanyakazi 9 wa vitengo mbalimbali vya Caritas na maendeleo iliyofanyika katika kituo cha malezi ya vijana cha Knorr Bremse cha St.Alamano, Parokia ya Shewa jimboni Mbeya.
Mkurugenzi Mangasila amesema kuwa  maendeleo na mafanikio katika  maeneo yao ya utume yanaanzia  katika ngazi ya familia, jumuiya ndogo ndogo na hatimaye katika jamii kwa ujumla, hivyo amewaalika kuyaishi kwa vitendo yale yanayoonekana katika maeneo yao ya utume  mathalani, unyenyekevu, upendo, ushirikiano, haki na amani huku wakimtanguliza Mungu.
“Ninawapongeza kwa kuzaliwa upya leo kwa kusheherekea siku zenu za kuzaliwa, kumbukeni kufikia hapa leo siyo kwa mipango yenu bali kwa mipango ya Mwenyezi Mungu, kupitia siku hii ya leo nawaalika kutafakari kutenda yanayompendeza jirani yako,”amesema.
Ameongeza kuwa mafanikio katika utume wao kazini yanatokana  na kutekeleza  majukumu  yanayowakabili  kwa unyenyekevu, ukweli na kujituma pasipo kujibakiza kwa ajili ya jamii ya wahitaji kadri ya upendo na huruma.
Kwa upande wake mmoja wa wafanyakazi, Praxeda Killian akizungumza kwa niaba ya  watumishi walioadhimisha siku ya kuzaliwa amemshukuru Mungu kwa kufikia siku hiyo  huku shukrani za pekee zikienda kwa wazazi  waliowalea na uongozi wa Caritas  kwa kuendelea  katika makuzi mema ya kifamilia.
“Kwa niaba ya wenzangu  tuliozaliwa leo tusisahau kuomba na kusali muda wote ili Mungu aweze kutujalia kuwahudumia wahitaji kwa upendo, haki, usawa na kujituma bila kujibakisha na tusisahau kuwakumbuka na kuwatembelea wahitaji,”amesisitiza.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU