Ajali ya wanafunzi Arusha

Mapadri, Masheikh, wachungaji watahadharisha
θ Waongoza ibada katika eneo la ajali


Na Sophia Fundi, Karatu.
MAELFU ya wananchi wa wilaya ya Karatu mkoani Arusha wamejitokeza katika ibada maalumu iliyofanyika katika eneo ilipotokea ajali na kuua wanafunzi 33, walimu 2 na dereva mmoja.
Ibada hiyo ilishirikisha waamini wa dini mbalimbali wilayani Karatu ikijumuisha mapadri wa Kanisa Katoliki, masheikh na wachungaji, wote wakiwa na lengo la kumwomba Mungu azipokee roho za marehemu na kuondoa balaa la ajali kama iliyotokea katika eneo hilo na katika wilaya nzima.
 Mkuu wa wilaya ya Karatu ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya Bi. Theresia Mahongo amewashukuru viongozi wa dini na waamini kwa pamoja kwa kushirikiana katika ajali iliyotokea kwa kuwasaidia majeruhi pamoja na marehemu kuwapeleka wanapostahili.
Amesema serikali inatoa shukrani zake kwa wote walioshiriki kwa hali na mali katika tukio zima, wakati ilipotokea ajali hadi kusafirisha majeruhi na maiti.
Akizungumza katika ibada hiyo mwakilishi wa Askofu Jimbo Katoliki Mbulu ambaye ni Makamu Msimamizi wa Kitume wa Jimbo Katoliki Mbulu Padri Urbano Sulle amewaomba waamini kuwa na ushirikiano bila kuangalia itikadi za dini kwani watu wote ni wana wa Mungu.
Amelaani vitendo vya madereva kutofuata alama za barabarani na kusababisha ajali ambapo Malaika wa Mungu ambao ni taifa la kesho na waliokuwa na ndoto zao za baadaye wamekatishwa ndoto hizo.
Kwa upande wake mwakilishi wa Kanisa la KKKT jimbo la Karatu Mchungaji John Safari amewaomba waamini kwa ujumla wao kuwa na roho ya toba kila wakati wakiinua macho yao kwa Mungu na pia kukemea roho ya ajali iliyotawala katika maeneo yote na kumwomba Mungu kutakasa eneo ilipotokea ajali   kwa damu ya Yesu aliyekufa msalabani.
Ajali hiyo ilitokea Mei 6 mwaka huu katika eneo la Marera kijiji cha Rhotia wilayani Karatu ambapo wanafunzi 33 wafariki, walimu 2 pamoja na dereva wa gari baada ya gari NO.T.871BYS COSTA kupinduka na kutumbukia kwenye korongo.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU