Umuhimu wa kuwa na ibada kwa Mama Bikira Maria (2)

SALA: Sala ya Malaika wa Bwana ni sala ya jadi ya kimapokeo inayotumika kwa kumbukumbu ya Mama Bikira Maria Kupashwa Habari ya kuzaliwa Bwana.
Sala hii inasaliwa mara tatu kwa siku: alfajiri, mchana na magharibi. Wakati wa kipindi cha Pasaka, sala ya Malkia wa Mbingu husaliwa badala ya ile ya Malaika wa Bwana, Sala ambayo  imekuwa ikisaliwa tangu karne ya 10 au ya 11. Sala zingine za Mama Bikira Maria ni sala ya Rozari Takatifu na sala ya Litania ya Loretto. Litania ya Loretto hujulikana na kupendwa zaidi.
Maandamano: Wakristo mara nyingi wamekuwa wakiandamana kwa kuonyesha heshima zao kwa Mama Bikira Maria. Maandamano kama haya yamekuwa yakifanywa na wakatoliki na waothodoksi kuanzia karne ya 16.
Kwa mfano katika mji wa Los Angeles kule Marekani kulikuwa na utaratibu wa kuandamana kwa heshima ya Mama Bikira Maria kila mwaka kwa miaka 100 ya kwanza baada ya kuanzishwa kwa mji huo hapo mwaka 1781. Utaratibu huu uliokuwa unafanywa kwa kumbukumbu ya uanzishwaji wa mji huo ulirudishwa tena mwaka 2011 baada ya kuachwa kwa miaka mingi.
Ibada zingine: Ibada kwa Mama Bikira Maria kwa mujibu wa kanuni au mafundisho ya Kanisa Katoliki: Ibada hizi ni pamoja na zile zinazohusu mafundisho juu ya Mama Bikira Maria kuwa yeye ni Mama wa Mungu, au ile imani kwamba Mama Maria amekuwa daima Bikira na alikingiwa dhambi ya asili na kwamba alipazwa mbinguni.
Ibada zenye uhusiano kama huu zinaweza kuanza kufanywa hata kabla ya tamshi  rasmi la Kanisa la kiimani kuhusu fundisho husika kutolewa kwa kuwa ibada zingine zinaendelea polepole na hivyo kuchukua muda mrefu. Mfano mzuri wa ibada iliyokuwa inaendelea polepole ni ile ya muungano wa ibada ya Moyo Mtakatifu wa Yesu na ile ya Moyo Safi wa Bikira Maria kuwa ibada ya Mioyo Mitakatifu ya Yesu na Maria.
Hata hivyo, ibada zingine zinaweza kulaaniwa kama ilivyotokea mwaka 1677, Roma ilipolaani ile imani kuwa Mama Maria mwenyewe alishika mimba kibikira, imani iliyokuwa  imezagaa kuanzia karne ya 4.
Maisha ya Mama Bikira Maria: Matukio fulani fulani maalum katika maisha ya Mama Bikira Maria yamesababisha kuibuka kwa ibada zinazolenga hivi vipengele maalum vya maisha yake. Mfano hai ni  pamoja na ile Ibada ya Mateso Saba ya Mama Bikira Maria inayokumbusha yale mateso aliyoyapata Mama Bikira Maria kama alivyokuwa ametabiri Nabii Simeoni kuhusu kusulubishwa kwa Yesu Kristo msalabani.
Kwa upande mwingine tena, kuna yale Matendo ya Furaha ya Mama Bikira Maria yanayoanza na kupashwa kwake habari kuwa atakuwa Mama wa Mungu na kuishia na tendo la kuvikwa kwake taji huko mbinguni. Kuna ibada zingine zinazoendelea muda wote kama zile zinazohusishwa na ulipaji fidia kwa matendo ya wanadamu ya kumtukana na kumkufuru Mungu yanayoendelea muda wote bila kikomo.
Ibada zinazohusisha Matokeo ya Mama Bikira Maria: Matokeo haya ni pamoja na yale yanayojulikana sana ulimwenguni ambayo yamekubaliwa rasmi na Kanisa Katoliki. Mifano ya hayo matokeo ni kama yale ya Bibi Yetu wa Guadalupe, Bibi Yetu wa Lurdi, Bibi Yetu wa Fatima, Bibi Yetu wa Akita, Bibi Yetu wa Kibeho na lukuki ya ibada zingine za kikanda pote ulimwenguni. Ibada hizi za kikanda ni kama zile za  Bibi Yetu wa Afya Njema za kule India au zile za Bibi Yetu wa Lichen za kule Poland.
Ibada kama hizi zimesaidia sana katika ujenzi wa makanisa makubwa makubwa yaliyojengwa na kutolewa wakfu kwa Mama Yetu Bikira Maria.
Picha na Sanamu za miujiza: Picha, sanamu pamoja na ikoni za aina mbalimbali za Mama Bikira Maria zimekuwa zikihusishwa na miujiza mbalimbali kama ile ya uponyaji iliyosababisha ibada hizi za kitakatifu kufanyika katika nchi kadhaa na kuhimiza ujenzi wa vituo maalumu vya hija kwa heshima ya Mama Bikira Maria.
Vitu vya kiibada: Vitu vya uchaji Mungu vinavyohusiana na heshima kwa Mama Bikira Maria ni pamoja na skapulari za aina mbalimbali, kama ile skapulari ya Bibi Yetu wa Mlima Karmeli ambayo inajulikana zaidi. Kati ya medali zote za Mama Bikira Maria, medali inayojulikana na iliyoenea zaidi ni ile  ya Miujiza. Imani inayohusu vitu vya kiibada kama medali  imekuwepo tangu miaka ya 1830.
Kuonekana mara nyingine kuwa na msisitizo wa wazo moja katika matokeo mawili ya mahali mbalimbali na nyakati mbalimbali. Kwa mfano katika matokeo ya Lurdi, ibada iliyosisitizwa ilikuwa ni ile ya Kusali Rozari Takatifu na matokeo ya Fatima yaliripotiwa kuwa Mama Bikira Maria alikuwa ameshika Rozari na pia skapilari.
Ibada za kikanda bado zinaendelea kuungwa mkono na viongozi wa kanda hizo. Kwa mfano sikukuu ya “Bibi yetu wa Upweke wa Porta Vaga katika visiwa vya Ufilipino imekuwa ikisherehekewa kwa karne na karne na ikoni yake bado inaendelea kuheshimiwa.
Huko Uhispania, kila mwaka wakati wa Pentekoste, kwenye watu milioni moja wana sherehe zinazoitwa “Romeria De El Rocio’’ ambazo zinakuwa  sehemu ya sherehe mahalia za heshima kwa Mama Bikira Maria.
Kunakuwa pia na ibada zingine za aina mbalimbali kwa heshima ya Mama Bikira Maria kwa mfano uwepo wa altare maalum katika makanisa ya Kikatoliki, altare ambazo zimewekwa wakfu kwa heshima ya Mama Bikira Maria.
Heshima kwa Mama Bikira Maria hazitolewi na wakristo wakatoliki tu na wala si na wakristo tu bali na hata waumini wa dini ya Kiislamu. Ibada ya Sala ya Rozari Takatifu, kwa mfano, hufanywa na wakristo Waanglikana na pia na Walutheri ingawa namna yao ya kusali ni tofauti na inavyosaliwa na waamini Wakatoliki.
            
Mwandishi ni Mhadhiri Mstaafu,Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Dar es Salaam.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU