“Nguvu nyingi bila kumshirikisha Mungu ni kazi bure”

MOROGORO,Viongozi wa dini na serikali wametakiwa kutokutumia akili na nguvu zao pekee katika kusimamia majukumu mbalimbali na badala yake wamtegemee Mungu awaongoze katika majukumu hayo ya kila siku.
Hayo ameyasema Askofu wa Jimbo Katoliki Morogoro Mhashamu Telesphor  Mkude alipokuwa akihubiri katika Misa Takatifu iliyofanyika Chuo Kikuu cha Jordan, Morogoro huku akitoa daraja la kipaimara na kuwapa daraja la Usomaji na Usindikizaji maflateri.
Askofu Mkude amesema viongozi mbalimbali wanatakiwa wafanye kazi zao za kuwaongoza wengine kwa kuomba mwongozo wa Mungu kwakuwa asiposhirikishwa Mungu, kutakuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wanaowaongoza.
“Viongozi wa dini na serikali tunatakiwa tumshirikishe sana Mungu katika kuibeba dhamana ambayo tumepewa ya kuwaongoza wengine, tusipomshirikisha Mungu katika kazi zetu kuna uwezekano mkubwa wa kutokutenda haki kwa tunaowaongoza hivyo kusababisha malalamiko na hatimaye kukwama na kutokufikia malengo tuliyojiwekea ili Taifa lisonge mbele,” amesema Askofu Mkude.
Askofu Mkude amesema baadhi ya viongozi wamekuwa hawawatendei haki wengine hivyo kusababisha malalamiko huku baadhi ya viongozi wakiamini kuwa hata wasipowatendea haki wanaowaongoza hawataelewa chochote na kusahau kuwa dunia sasa hivi ni kama kijiji na kila mtu anapambana ili azijue haki zake.
“Yatupasa kuwa na hofu ya Mungu katika kuongoza vitengo tulivyokabidhiwa kwa kutenda haki, tusipotenda haki ipo siku tusiowatendea haki watachoka na kuchukua maamuzi magumu,” amesema Askofu Mkude.
Wakati huo huo Askofu Mkude amewaasa viongozi wa dini kuwaombea wafanyakazi mbalimbali ili wafanye kazi zao kwa moyo pasipo manung’uniko ili taifa lisonge mbele na kufikia malengo.
“Kuna kazi ambazo sisi hatuwezi kuingia mtaani na kuzifanya, hivyo tunapoazimisha siku hii ya wafanyakazi duniani kote ni jukumu letu kuwaombea wafanyakazi wa vitengo mbalimbali kama barabara, hospitali, maseremala na sekta zingine kwani tunategemeana katika kila jambo, tuombeane ili tusonge mbele,” amesema Askofu Mkude.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU