Waamini Musoma waonywa juu biashara ya dawa za kulevya

Askofu wa Jimbo Katoliki Musoma Mhashamu Michael Msonganzila amewataka waamini jimboni humo kutotaka maisha mazuri ya haraka haraka kwa kutumia njia za mkato kama kilimo cha bhangi na kuuza dawa za kulevya ili kupata  mali na utajiri, bali watumie njia halali inayompendeza Mungu.
Askofu Msonganzila ameyasema hayo hivi karibuni wakati wa Misa Takatifu ambayo iliambatana na harambee ya kuchangia ujenzi wa Kanisa ambapo jumla ya fedha taslimu shilingi milioni 106 zilipatikana pamoja na kutoa sakramenti ya kipaimara kwa watoto 400, Misa iliyofanyika katika parokia ya Tarime Jimboni hapo.
Askofu Msonganzila amewaambia waamini hao kuwa mali na utajiri ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu,  kama watatumia njia iliyo halali kwani wana bahati ya kuwa na   mifugo mingi ambayo  wanaweza  kuitumia kupata mali na utajiri badala ya kuhangaika na kilimo cha bhangi na kuuza dawa za kulevya ambazo hata serikali inapiga marufuku.
“Naomba niwaambie ndugu zangu msitake maisha mazuri kwa kutumia njia ya kilimo cha bhangi, kuuza dawa za kulevya, wizi au njia nyingine yoyote ya kupata mali haraka isiyo halali, zote hizi ni njia za shetani wala hazimpendezi Mungu. Parokia ya Tarime mmejaaliwa kuwa na mifugo mingi na kila familia naamini mna mifugo ambayo mna uwezo wa kuitumia mifugo hiyo kwa ajili ya kupata mali, achaneni na njia hizo kabisa msije mkajiletea matatizo maana hata serikali inapiga marufuku kabisa njia hizo,”amesema Askofu Msonganzila.
Pia amewakumbusha waamini wa parokia hiyo kuhakikisha kila mmoja anawajibika  ndani ya familia yake kudumisha amani na upendo, sambamba na kuhakikisha vitendo vya ukatili vinakomeshwa ili amani, upendo na uvumilivu vitawale katika familia na jamii kwa ujumla, ili kusudio la Mungu liweze kutimia kwa kuwa vitendo vingi vya ukatili ambavyo vimekuwa vikitokea vinatokana na upendo, amani na uvumilivu kupungua ndani ya familia.
“Wito wangu kwenu wakristo wa Parokia ya Tarime, nawaombeni sana mshikamane, mpendane, mvumiliane pale mwenzako anapokukosea msameheane, mkifanya hivyo mtakuwa mmemshinda shetani, na ndio maana  Kanisa Katoliki halichachi kutokana na kuwa na misingi imara ya upendo,” amefafanua.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU