Tanzania inapoteza asilimia 1 ya pato la Taifa kutokana na uduni wa mazingira

IMEELEZWA kuwa ili kuendana na uchumi wa kati ambao nchi imedhamiria kufikia ifikapo mwaka 2025 upo umuhimu mkubwa wa kuwa na miundombinu ya usafi inayoakisi hali ya uchumi wa kati.
Hayo yameelezwa hivi karibuni mkoani hapa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii ,Jinsia,Wazee na Watoto Mh.Ummy Mwalimu pamoja na wadau wa masuala ya usafi wa mazingira, ambapo kwa pamoja wamepitisha azimio la kutambulisha awamu ya pili ya kampeni ya kitaifa ya usafi wa mazingira.
Pamoja na mambo mengine kampeni hiyo inahusisha maboresho ya vyoo vya kisasa, kunawa mikono kwa kutumia sabuni, kutibu maji ya kunywa, usafi mashuleni, usafi kando ya barabara kuu na kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.
Akitilia mkazo suala la usafi wa mazingira Mwalimu amesema kujisaidia hovyo imekuwa ni tatizo kubwa kwa zaidi ya miaka 25 ambapo kulingana na ripoti ya mwaka 1990 inaonyesha jumla ya asilimia 10 ya watu waishio vijijini hawakuwa na vyoo huku zaidi ya asilimia 55 ya watanzania walikuwa wakitumia vyoo duni vyenye madhara kiafya na uchumi.
“Taifa kwa ujumla linahitaji kupiga vita matumizi ya vyoo duni pamoja na tabia ya kujisaidia hovyo ili kuondokana na magonjwa ya kuhara, kipindupindu, minyoo na nimonia,” amesema.
Mbali na hayo amesema kuwa hali duni ya usafi, huigharimu nchi asilimia moja ya pato la taifa kila mwaka na kwamba uchafu huchangia kwa kiasi kikubwa kudumaa kwa watoto nchini kunakosababishwa na kuhara ambapo jumla ya watoto milioni 2.7 huathirika.
Hata hivyo kulingana na ripoti ya Benki ya dunia inaonyesha kuwa Tanzania inapoteza asilimia 1 ya pato la ndani ya taifa kutokana na hali duni ya usafi wa mazingira.
Ripoti inazidi kueleza kuwa kiasi hiki ni kikubwa sana kwa taifa linalotarajia kuwa na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 na hivyo wizara kutoa wito kwa wananchi wote kuunga mkono serikali kuhakikisha upatikanaji wa vyoo bora.
Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na shirika la umoja wa mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) takwimu zinaonesha kuwa dunia inapoteza watoto milioni 1.7 kila mwaka kutokana na magonjwa ya kuhara na nimonia.
Hata hivyo ripoti hiyo inaeleza kuwa vifo hivyo vinaweza kuzuilika kwa kunawa mikono kwa sabuni kila baada ya kutoka chooni ikiwa ni pamoja na serikali kuelekeza bajeti ya mapato katika masuala ya mazingira kwa ujumla.
Kampeni ya kitaifa ya usafi wa mazingira ilizinduliwa mwaka 2012 ili kuongeza kasi ya kuboresha hali ya usafi wa mazingira nchini ikiwa ni pamoja na kuunganisha nguvu ya pamoja na wadau wote kuhamasisha jamii kuwa na vyoo bora.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU