Wakazi Ngorongoro waiomba serikali kuwanusuru njaa

WANANCHI wanaoishi katika Tarafa ya Ngorongoro wilayani Ngorongoro mkoani Arusha wameiomba serikali kwa kushirikiana na Mamlaka ya Hifadhi ya Taifa Ngorongoro (NCAA) kuweka utaratibu mbadala wa kuwalipa kiasi cha fedha kinachotokana na utalii ili kuwanusuru na njaa kali inayowakabili.
Tarafa hiyo yenye zaidi ya wakazi 82,000 kati yao ni asilimia tatu tu ndio wenye uwezo wa kufuga, huku asilimia 97 wakiwa hawana uwezo wa kufanya chochote kutokana na wananchi hao kuzuiwa kufanya shughuli zozote za kilimo ndani ya hifadhi hiyo.
Mwenyekiti wa Baraza la Wafugaji Ngorongoro ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Nainokanoka, Edward Maura akizungumza katika kikao cha kuwanusuru wananchi hao na baa la njaa, amesema wananchi wa tarafa hiyo wapo katika hali ngumu kimaisha kutokana na kutokuwa na njia yoyote mbadala ya kuwaingizia kipato huku wakitegemea  chakula cha msaada kutoka NCAA ambacho hakiwatoshelezi.
“Pamoja na kuahidiwa kuletewa chakula wakati mwingine hakifiki kabisa na hakitoshi, tunaiomba sana serikali kwa kushirikiana na NCAA waweke utaratibu wa kutulipa fedha zinazotokana na utalii kila mwezi angalau Sh 300,000 kwa kila kaya ili waweze kujikimu kimaisha, vinginevyo maisha yanazidi kuwa hatarini,” alieleza.
Naye Meneja mipangowa Baraza la Wafugaji Wanawake (PWC), Alais Melau amesema wamekuwa wakivijengea uwezo vikundi vya wakina mama kwa kuwapatia mikopo na kuwaanzishia miradi midogo midogo ya kujikwamua kiuchumi.
Melau amesema wamewagawia wananchi hao mbuzi 900 na kuwasaidia kuanzisha maboma ya kiutamaduni ambayo wamekuwa wakifanya shughuli za utalii na kujipatia kipato cha kuendeleza familia zao.
NayeNaibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro, William ole Nasha amesema matatizo  yanayowakabili wananchi wa tarafa hiyo ni kutokana na kuwepo kwa sheria ya ardhi inayowanyima uhuru ndani ya hifadhi hiyo.
Amesema katika kuhakikisha kuwa wananchi hao wanaondokana na njaa, wameandaa utaratibu wa kuwaletea wananchi chakula na kuwauzia kwa bei nafuu ya soko ili kila mwananchi amudu gharama za kununua chakula hicho.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU