Wataalamu Wakristo wajiimarishe kiroho

n Na Emmanuel Kamangu, Kigoma

CHama cha Wataalamu Wakristo Tanzania (CPT) Jimbo Katoliki Kigoma kimewataka wanachama wa utume huo kuishi maisha ya utakaso kiroho na kimwili ikiwemo kujiimarisha kiuchumi katika kumtumikia Mungu.
Hayo ameyasema Katibu Mtendaji wa CPT Jimbo Katoliki Kigoma (CPT) Fransis Mangu wakati akizungumza na Gazeti hili katika kujua mipango mikakati waliyonayo ndani ya utume huo ambapo ametaja kuwa wanapanga kujiimarisha kiroho sambamba na kiuchumi ndani ya Kanisa Katoliki.
Akitoa mfano kwa upande wa kiroho amesema wamepanga kujiimarisha katika mambo ya imani kama kufanya Hija, mafungo pamoja na sala na kwa upande wa kiutawala ni kueneza utume huu katika kujitanua kiuchumi.
Hata hivyo Mangu amesema kuwa katika Parokia 23 za Jimbo Katoliki Kigoma changamoto waliyonayo ni kwa upande wa Parokia moja ya Kibombo ambapo wamejipanga kuwa ifikapo Septemba 30, watakuwa na Hija katika Parokia hiyo itakayochukua siku mbili ili kuhamasisha utume huo kuwaimara jimboni hasa upande wa kiroho na kimwili.
Aidha Katibu Mangu amesema kuwa wana aina tatu za mikutano; timu ya Jimbo ambayo hukutana mara sita kwa mwaka, pamoja na Halmashauri inayochukua viongozi watatu wa kila parokia na hukutana mara mbili kwa mwaka katika kupanga mikakati juu ya kuendeleza malengo ya utume huo.
“Mbinu tunazozitumia ni tofautitofauti lakini tunaziunganisha pamoja ambazo tunaziita mkutano, kwa hiyo tunakuwa na semina, mafundisho mbalimbali ya kiimani sambamba na mafungo,” Amesema Mangu.
Kwa upande mwingine Mangu amesema kuwa wanapokutana wanakuwa na padri ambaye huongoza mambo yote ya kiroho lakini pia wanakuwepo walei mbalimbali wenye historia za kiimani ambao hupewa nafasi kufundisha.
“Mijadala mbalimbali huwepo katika mikutano yetu ili kubadilishana uzoefu wa kiimani ikiwemo wa kiutaalamu kulingana na kila taaluma ya kila mmoja wetu,” Amesema Mangu.
Katibu Mangu amedai kuwa katika utume huo kipaumbele cha kwanza ni kufundishana kuelewa kuwa Mungu ndio wa kwanza na wa mwisho katika kila jambo hapa Duniani.
“Kwahiyo taaluma na utaalamu wa mtu haumfanyi kutokushiriki mambo ya kimungu bali kila binadamu yeyote aliyeumbwa na Mungu  anatakiwa kuanza na Mungu na kumaliza na Mungu katika shughuli za roho na mwili.”


Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU