KUELEKEA MIAKA 100 YA UPADRI: KILOMBERO WAPATA PADRI WA KWANZA MJESUITI



Na Tuzo Nyoni, Ifakara
Wakati maandalizi ya maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 100 ya Upadri nchini yatakayofanyika katika Jimbo Kuu Katoliki Dodoma yakiendelea vizuri, wito kwa mapadri nchini umeendelea kutolewa kuwa wazingatie kuwa wametumwa kwa watu ili wawasaidie kuondokana na matatizo mbalimbali na hatimaye wajisikie kuwa wao pia ni wana wa Mungu.
Akihubiri katika adhimisho la misa takatifu ya shukrani ya Padri Patrick Ngamesha(PICHANI) iliyofanyika hivi karibuni katika Kanisa la Mtakatifu Siliakus parokiani Mang’ula  Jimbo Katoliki Ifakara, Padri Valelian Shirima aliyewahi kuwa Mkuu wa Shirika la Majesuiti  amesema kuwa Kanisa lote la Mungu lina haki ya  kusherehekea sikukuu hiyo kwa ajili ya makuu aliyoyatenda kupitia nafsi ya padri mpya Patrick Ngamesha.
Padri Shirima amesema mapadri wamepewa mamlaka ya kuwasafisha watu dhambi zao na wanapokutana na watu wenye mioyo migumu wasichoke kuwahubiria neno la Mungu, kazi ambayo mapadri wanaifanya katika maisha yao yote na wakumbuke kwa sababu yao watu wengi watakuja kumwabudu na kumshuhudia Kristo, na tuzo lao  halitakuwa dogo.
Aidha Padri Shirima amemtaka Padri Patrick Ngamesha ambaye ni mjesuiti wa kwanza wa bonde la mto Kilombero (majimbo Katoliki Ifakara na Mahenge) kuwa mtu wa  sala na kabla ya kufanya kitu chochote akumbuke kuanza kwa sala ili kazi yake iwe ya kumpendeza Mungu na aweze kuunganika naye.
“Mapadri wanatakiwa wakumbuke kuwa Mungu hakuwaita kuja kulipiza kisasi na kuwatakia mabaya watu wabaya, bali wameitwa ili wawatakatifuze watu na kuwatia moyo ili wawe watu wanaomfuata Kristo,” Amesema Padri Shirima.
Hata hivyo amewakumbusha mapadri kuwa tayari kutumwa popote kufanya utume, tegemeo lao likiwa Kristo mwenyewe atakayewawezesha katika utume wao huku wakiepuka kuwa kikwazo kwa kila watakayekutana naye.
Padri Ngamesha alipewa Daraja takatifu ya Upadri tarehe 7 Julai mwaka 2017 katika parokia ya Msimbazi Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam na Askofu Msaidizi wa Jimbo hilo Mhashamu Eusebius Nzigilwa.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU