VIWAWA SUMBAWANGA WAMWOMBEA KARDINALI PENGO



Vijana wa Kanisa Katoliki  Jimbo Katoliki Sumbawanga wamefanya maadhimisho ya misa ya  kumuombea kwa Mwenyezi Mungu Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo azidi kuimarika katika afya yake ili aweze kuendelea na wajibu wake wa utume.

Maombi hayo yamefanyika wakati wa Kongamano la vijana Jimbo Katoliki Sumbawanga lililojumuisha jumla ya vijana 408 kutoka parokia 21 za Jimbo Katoliki Sumbawanga lililofanyika kwa siku 5 na kuhitimishwa dominika ya moyo mtakatifu wa Yesu parokiani Mwazye sehemu ambapo alizaliwa Kadinali Pengo.

Akiongoza mamia ya vijana katika Kongamano hilo, Mkurugenzi Idara ya vijana Jimbo Katoliki Sumbawanga padri Christopher Mayemba amewapongeza vijana kwa uamuzi wao huo wa kujali na kuthamini wazee na hasa viongozi wa Kanisa katika mwaka huu wa Jubilei ya miaka 100 ya upadri kwani kunaonesha kujali na kuthamini shughuli za kichungaji zinazofanywa na Askofu Mkuu huyo.

“Ninawapongeza sana wapendwa vijana katika misa hii kwa kumuombea kwa Mwenyezi Mungu Kardinali Pengo ambaye hivi karibuni amerejea nchini kutokea kwenye matibabu, hivyo Mwenyezi Mungu amjalie nguvu na afya njema ya mwili na roho aweze kuimarika na kuendeleza utume. Mmefanya kitu chema na hasa kwa mwaka huu ambapo Kanisa la Tanzania linafanya Jubilei ya miaka 100 ya upadri, basi mzidi kuwaombea mapadri na kuwasaidia waweze kufanya utume wao wa kuliongoza Kanisa kwa sifa na utukufu wa Mungu,” amesema padri Mayemba.

Akieleza malengo ya Kongamano hilo kwa vijana kwa mwaka huu wa Jubilei ya miaka 150 ya Ukristo na miaka 100 ya upadri kufanyika katika parokia ya Mwazye, Katibu Mtendaji Idara ya Vijana Jimbo Bw. Emanuel Mathias amesema kuwa parokia ya Mwazye ina historia ya pekee katika Kanisa na hasa Jimbo Sumbawanga  kwa kuzaa miito mitakatifu ya utawa na upadri na zaidi kutoa maaskofu wawili ambao wanaendelea kulitumikia Kanisa  akiwepo Askofu wa  Jimbo Katoliki Shinyanga Mhashamu Liberatus Sangu na Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Dar es Salaam ambao wamezaliwa katika parokia hiyo.

“Mbali ya zawadi hii ya miito mitakatifu jimboni Sumbawanga na Taifa kwa ujumla ni jukumu letu pia kuwaombea viongozi wetu wazawa wa parokia hii  na hasa Kadinali ambaye amerejea kutoka kwenye matibabu hivi karibuni, wito wetu pia ni kwa viwawa wenzetu Tanzania kuungana nasi katika kumuombea ili Mwenyezi Mungu aweze kumjalia afya njema azidi kuchunga kondoo wake na hasa vijana ambao ndilo Kanisa la kesho.”

Kongamano hilo la vijana hufanyika kila mwaka jimboni Sumbawanga ambapo huhusisha parokia 21 zinazounda Kanda 4 ambazo ni Kanda ya Kati inayoundwa na parokia za Kanisa Kuu, Kristo Mfalme, Roho Mtakatifu, Mt. Fransisko wa Asizi, Ipito, Izimba na parokia ya Familia Takatifu. Kanda ya Kusini inayoundwa na parokia za Tunduma, Laela, Mpui, Kaengesa na parokia ya Mwazye. Kanda ya Kalambo inayoundwa na parokia za Ulumu, Matai, Sopa na Kasanga pamoja na Kanda ya Nkasi inayoundwa na parokia za  Chala, Namanyere, Kirando na parokia ya Kala.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU