UPATANISHO: KARATU WAANDAA MISA MAALUM



Na Sophia Fundi, Karatu.

PAROKIA ya Karatu katika Jimbo Katoliki Mbulu kwa mara ya kwanza tangu ianzishwe mwaka 1946 imeadhimisha misa ya upatanisho kwa walei na mapadri waliowahi kufanya utume katika parokia hiyo akiwemo marehemu padri John Costigan wa Shirika la wapalotini ambaye ndiye mwanzilishi wa parokia hiyo.

Misa hiyo ni hitimisho la Mfungo wa Novena ya siku tisa ya kuomba Huruma ya Mungu ambapo waamini walishiriki katika Jumuiya ndogondogo za kikristo na  hatimaye kushiriki adhimisho la misa iliyohudhuriwa na mapadri zaidi ya 30, wakiwemo mapadri wote waliowahi kufanya utume katika parokia hiyo na mwakilishi wa Shirika la wapalotini ambaye ni mkuu wa Shirika hilo jimboni Mbulu, viongozi wa Serikali katika Wilaya ya Karatu, wabunge Jimbo la Karatu, viongozi wa siasa na wazee maarufu.

Akihubiri katika Misa hiyo, paroko wa parokia hiyo padri Pamphili Nada amesema kuwa tukio hilo la kuadhimisha misa ya upatanisho ni zoezi lililoibuliwa na walei wa parokia hiyo kupitia umoja wa wazee na mapadri waliowahi kufanya utume katika parokia hiyo ambapo waliamua kufanya adhimisho la misa katika adimisho la somo wa Kibawata parokia ya Karatu ya  Mtakatifu Yakobo  mtume Julai 25 ya kila mwaka.

Akizungumza kwa niaba ya wawakilishi wa walei, Mwenyekiti wa parokia Bw. Reginard Bayyo amesema kuwa parokia imeamua kufanya adhimisho la misa takatifu ya upatanisho kwa lengo la kuwaomba msamaha mapadri waliowahi kufanya utume katika parokia hiyo waliotangulia mbele ya haki na wanaofanya utume maeneo mbalimbali kwa yote waliyowakosea hasa padri Costigan ambaye anadaiwa kuondoka bila amani katika parokia hiyo na kurudi kwao  Ireland miaka ya 1972 ambapo walei wamelifikiria na kuona kuwa hakufanyiwa vizuri katika utume wake.

Katika adimisho hilo Mwenyekiti huyo ameomba msamaha kwa niaba ya walei parokia ya Karatu kwa kumpa majani kama ishara ya kuomba msamaha mwakilishi wa shirika la wapalotini padri John Onna na pia  kama ishara ya kuomba msamaha kwa niaba ya mapadri wote waliowahi kufanya utume katika parokia ya Karatu majani hayo alipewa padri John Qadwe.

Akielezea historia ya marehemu padri Costigan, Padri John Qadwe amesema kuwa marehemu alifanya kazi ya utume katika parokia ya Karatu miaka ya 1949 hadi 1972 ambapo alihamishwa kwenda kuanzisha parokia ya Endabash jimboni Mbulu lakini marehemu hakufurahishwa na uhamisho huo na kuamua kujifungia chumbani kwake siku tatu bila kula chochote na baada ya siku hizo aliondoka kwenda kwao bila kumuaga mtu yeyote.

Amesema kuwa kuondoka kimyakimya kwa marehemu padri Costigan kuliwafanya walei parokia ya Karatu kuwa na  wasiwasi kwamba hakufurahishwa na kitendo hicho, ndipo walipoamua kutafuta ndugu zake au mapadri wa Shirika lake kuwaomba msamaha kwa yote yaliyotokea miaka hiyo kwa kuwashirikisha mapadri wote waliowahi kufanya utume parokiani Karatu.

Mwakilishi wa Shirika la wapalotini padri Onna baada ya kupokea majani ya upatanisho kutoka kwa Mwenyekiti wa walei aliwashukuru kwa kutafuta upatanisho ambapo aliwaomba zoezi hilo liwe endelevu katika familia na jumuiya ndogondogo za kikristo.




Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU