Matokeo kidato cha VI: Shule za Kanisa Katoliki

6,495 kati ya 6,840 wafaulu kwenda Vyuo Vikuu

n  Na Pascal Mwanache

WAKATI Kanisa Katoliki likiwa katika maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara, matokeo ya kidato cha sita kwa shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki zimewezesha wanafunzi 6,495 kati ya 6,840 kufaulu na kuwa na sifa za kujiunga na Vyuo Vikuu.
Taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Idara ya Elimu ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Padri Raraiya Alphonce, imeeleza kuwa jumla ya wanafunzi waliofanya mtihani wa kidato cha sita mwaka huu ilikuwa 73,692 kitaifa na kati ya hao wanafunzi wa shule za Kanisa Katoliki waliofanya mtihani huo ni 6,840 sawa sawa na asilimia 9.3%.
Padri Raraiya amesema kuwa wanafunzi waliofaulu kwa daraja la kwanza ni 1,079, daraja la pili ni 2,852, daraja la tatu ni 2,564. Ufaulu hafifu, yaani daraja la nne ni 253 na walioshindwa ni 92.
“Ni mategemeo kuwa idadi ya watakaojiunga na vyuo vikuu kutoka katika shule za Kanisa Katoliki ni 6,495 sawa na asilimia 11.09% ya wanafunzi 58,556 waliofaulu kwa daraja la kwanza mpaka la tatu. Pongezi nyingi ziwafikie Maaskofu kwa misaada mbalimbali na miongozo katika kuendesha shule zetu; pongezi kwa Makatibu Elimu Jimbo, wakuu wa shule husika na walimu wote kwa matokeo haya,” Ameeleza.
Aidha ametoa wito kwa walimu wa shule hizo kujitathimini na kuona jinsi ya kuendelea kuwasaidia wanafunzi ili wapate elimu bora. Pia amewaasa Makatibu elimu katika majimbo kuwapatia nafasi walimu ili wajiendeleza kitaaluma ili wawe walimu mahiri na wenye kuwajibika.
“Matokeo ya mitihani ni kipimo kwetu sisi walimu kuona ni kwa jinsi gani tumewajibika na kusaidia wanafunzi kusonga mbele katika kutimiza ndoto zao. Tumshukuru Mungu kwa uwezo aliotupatia wa kuondoa ujinga ndani ya vichwa na maisha ya vijana wetu. Tuombe neema ya kuwapa vijana wetu elimu bora na maadili.” 
Miongoni mwa shule zilizofanya vizuri katika matokeo hayo ni pamoja na shule tatu zilizoingia katika nafasi ya kumi bora (zenye idadi zaidi ya wanafunzi 30) ambazo ni Shule ya Sekondari ya Wavulana Marian (2), Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Marian (5), Shule ya Sekondari Maria Mtakatifu Mazinde (7).
Shule zilizofanya vizuri zilizo na idadi chini ya wanafunzi 30 ni pamoja na Seminari ya Mt Yakobo- Moshi (4), Shule ya Sekondari ya Kaisho- Kayanga (7), na Seminari ya Rubya-Bukoba (9).
Kuangalia matokeo yote ingia katika blogu ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania: www.tec1956.blogspot.com.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU