Kardinali Pengo: Miaka 25 iliyotukuka


n  Na Pascal Mwanache

ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo ameadhimisha Jubilei ya miaka 25 ya kuliongoza Jimbo hilo, na kusema kuwa ushirikiano kati yake na waamini ndiyo uliowezesha mafanikio mbalimbali katika utume wake ikiwa ni pamoja na kuanzisha Parokia 87.
Katika Misa hiyo ya shukrani iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Mt. Yosefu, Kardinali Pengo amewashukuru waamini kwa sala zao kwa muda wote alipokuwa akipatiwa matibabu, na kusema kuwa kwa sasa afya yake imeimarika na ameshuhudia makuu ya Mungu.
“Nilipotoka katika chumba cha upasuaji nilisema maneno haya: ‘Sitakufa bali nitaishi ili niyasimulie matendo makuu ya Mungu’. Ninawashukuru wanajimbo ambao wameifanya miaka 25 ikamalizika kwa haraka. Hii inatokana na ukweli kwamba mmoja anatoa amri na wengi wanatenda” amesema Kardinali Pengo wakati akitoa shukrani kwa waamini.
Akitoa homilia katika misa hiyo Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam Mhashamu Eusebius Nzigilwa amesema kuwa moja ya mambo makubwa yaliyofanywa na Kardinali Pengo katika kipindi cha miaka 25 ya uongozi jimboni humo ni pamoja na kusogeza huduma karibu na waamini, ambapo amefanikiwa kuanzisha Parokia 87 na parokia 3 teule.
“Siku zote katika utumishi wake huwa anaumia akiona waamini wanavuka barabara kwenda kanisani. Ndiyo maana amefanya kazi kubwa ya kuanzisha parokia 87 na parokia teule 3. Pia katika uongozi wake mapadri 73 wamepadrishwa. Hii ni changamoto kwenu waamini, hamna budi kuzalisha mapadri kwani idadi ya parokia alizozianzisha ni kubwa kuliko idadi ya vijana mliowatoa kuwa mapadri” ameeleza Askofu Nzigilwa.
Adhimisho hilo la Misa Takatifu limeoongozwa na Kardinali Pengo na kuhudhuria na waamini wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam, ikiwa ni pamoja na Rais Mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa, viongozi wa Halmashauri ya Walei Jimbo na watu wenye mapenzi mema.
Itakumbukwa kuwa Julai 22, 1992 aliyekuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam, Mwadhama Laurean Kardinali Rugambwa alistaafu na moja kwa moja nafasi hiyo ikachukuliwa na Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo ambaye kabla ya kuchukua nafasi hiyo alikuwa Askofu Mkuu mwandamizi wa Dar es salaam (kuanzia Machi, 1990 hadi Julai 22, 1992).
Pamoja na kusherehekea miaka 25 ya kuliongoza jimbo la Dar es salaam, Kardinali Pengo ameadhimisha miaka 46 ya upadri na miaka 33 ya uaskofu.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU