RAIS MAGUFULI KUMALIZA TATIZO LA MAJI SEKONDARI GEITA



WANAFUNZI wa Sekondari ya Kristo Mfalme Nyantakubwa katika Jimbo Katoliki Geita wameandamana hadi mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Magufuli wakidai huduma ya maji.

Wanafunzi hao ambao walifika mbele ya Rais Magufuli eneo la Katunguru akiwa katika msafara wake kwenda kuzindua mradi mkubwa wa maji Wilayani Sengerema katika kijiji cha Nyamazugo, waliambatana na walimu wao na mapadri walezi wa shule hiyo huku wakiwa na bango lenye maandishi “Mhe. Rais Magufuli tunaomba utoe tamko kuhusu kilio chetu cha maji kijiji cha Nyantakubwa.”

Akizungumza na blog hii, Mkuu wa shule hiyo ya Sekondari ya wasichana ya Nyantakubwa padri George Nkombolwa amesema wamefikia uamuzi wa kwenda mbele ya Rais kufuatia kutelekezwa kwa Mradi wa maji wa vijiji vya Chamabanda Nyantakubwa, Nyamtelela na Kasungamile huku viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema wakikaa kimya.

“Tatizo la maji ni kubwa sana kijijini Nyantakubwa na hasa kuendesha shule bila maji ni gharama kubwa sana. Tunasikitika hatuoni hatua zozote na mradi una karibuni miaka 5, hakuna matumaini,” amesema padri George.

Awali Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Sengerema Magesa Mafuru alipotembelea shuleni hapo alisema kuwa mradi huo wa maji ulikwama baada ya Mkandarasi aliyekuwepo kushindwa kazi na hivyo wamemuuzia mkandarasi mwingine atakayekamilisha kazi hiyo, lakini hakuna kinachofanyika.

Akizungumzia tatizo hilo Rais John Magufuli wakati wa hotuba yake kijijini Katunguru ameomba wananchi kuwa na subira kwani Serikali inafanyia kazi miradi mingi ya maji na kwamba yote haiwezi kuisha kwa siku moja.

“Tunafanyia kazi miradi mingi sana ya maji na tunafanikiwa. Lakini hatuwezi kukamilisha yote kwa siku moja...kwani hata Mungu aliumba hatua kwa hatua kwa siku sita na ya saba akapumzika.”

Wakati huo huo, Raisi John Magufuli amempongeza Paroko wa Parokia ya Nyantakubwa Jimboni Geita, padri George Nkombolwa kwa kutoa huduma nzuri ya elimu kwa wasichana.

Raisi amempongeza padri George wakati akiongea na wananchi wa Kijiji cha Katunguru akiwa njiani kwenda kuzindua mradi wa maji wilayani Sengerema.

“Nakupongeza sana Baba Paroko kwa kuelimisha wasichana. Ninyi wasichana someni kwa bidii na muache kudanganywa eti ËŠnakupenda`, acheni mambo hayo hadi mhitimu masomo. Naendelea kukazia tena..mtoto wa kike awe shule ya Msingi au Sekondari akipata mimba ndiyo basi hatarudi tena shuleni.  Ataenda huko awe mzazi na wazazi wenzake.” Rais amesema.

Mhe. Rais amesema pia kuwa kwa upande wa wavulana au wanaume watakaowapa mimba wanafunzi wajue kuwa miaka 30 inawasubiri jela.

Habari ambazo zimeifikia blog hii ni kuwa baada ya ziara ya Rais Magufuli kukamilika na kuelekea Wilayani Chato, Mhandisi wa maji Wilaya ya Sengerema Bw. Blaise amefika katika Shule ya Sekondari Yesu Kristo Mfalme Nyantakubwa siku ya Jumatano na kuahidi kuwa mkandarasi mpya amekwishapatikana na akaahidi kuwa maji yataanza kutoka baada ya miezi 6.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU