Waamini wa Kanisa Katoliki Malawi waandamana hadi bungeni

WAAMINI wa Kanisa Katoliki Malawi wameandama hadi bungeni kupinga kupitishwa sheria ya utoaji mimba na ndoa za jinsi moja.
Taarifa kutoka ofisi ya Mawasiliano ya Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi  (ECM) zimeeleza kuwa, maandamano hayo ya amani yamefanyika Desemba 6 mwaka huu yakiongozwa na Katibu Mkuu wa ECM  Padri Henry Saindi.
Aidha imeelezwa kuwa,  tukio hilo ni la kihistoria nchini humo kwa waamini hao kuonesha ujasiri wa kiimani na kuthamini uhai na utu wa mwanadamu.

Katibu Mkuu wa ECM  Padri Saindi ameeleza kuwa, dhamira kuu ya maandamano hayo ilikuwa ‘kuwasha mshumaa’ mshumaa wa kumulika uhai na familia ambazo chanzo chake ni Kristo.

“ Barabara zilifurika waamini kutoka wilaya 28 wanaotaka bunge letu kupitisha sheria ya kulinda uhai yaani kupinga sheria ya kuhalalisha utoaji mimba na ndoa za jinsi moja,” amesema Padri Saindi.

Akihutubia maelfu ya watu waliojitokeza katika maandamano hayo ya amani, Padri Saindi amesema kuwa, nchi ya Malawi si ya kipagani. Ni nchi inayomuamini Mungu na kumcha Mungu kupitia dini mbalimbali nchini humo, hivyo hakuna haja ya kuhalalisha utoaji mimba na ndoa za jinsi moja kwani kufanya hivyo ni kwenda kinyume na matakwa ya Mungu.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya masuala ya  Afya ya Bunge hilo Bi. Julliana Lunguzi aliyepokea mapendekezo hayo ya Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi kupitia Katibu wake Padri Saindi amewahakikishia waamini hao kuwa wamekubaliana na mapendekezo ya Kanisa Katoliki Malawi na watafanyia kazi kulingana na mapendekezo yao.
“Mimi pia ni muumini wa Kanisa Katoliki, mwanamke tena mwenye ujuzi wa utabibu. Sitakubaliana kupitisha sheria ya utoaji mimba na ndoa za jinsi moja. Ninachowasihi ni kuendelea kutuombea ili Roho Mtakatifu atuongoze tufanye maamuzi sahihi ndani ya bunge letu,” amesema Bi. Lunguzi. 

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU