Askofu Rwoma: Msitoe wala kushiriki kutoa mimba



Askofu wa jimbo katoliki Bukoba Mhashamu Desiderius Rwoma amewataka wanawake wote wakristo nchini kukataa kupokea shinikizo lolote la kutoa mimba wakiiga mfano wa Bikira Maria alivyokubali kumleta duniani Mkombozi wao Yesu Kristo.
Askofu Rwoma ametoa rai hiyo wakati wa mahubiri yake kwa niaba ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kwenye  adhimisho la misa takatifu ya Krismasi kitaifa iliyofanyika katika kanisa kuu la jimbo katoliki Bukoba.
“Kataeni aina yoyote ya ushawishi ama sababu zozote zile ambazo zinaweza kuwasukuma kukubali kutoa mimba, ukitoa mimba licha ya kumkosea Mwenyezi Mungu na kiumbe kisicho na hatia, pia umelikosesha taifa pengine mtu ambaye angechangia katika maendeleo yake,” amefafanua.
Amesema Yesu Kristo aliyezaliwa ni mkombozi wa kila mtu, hivyo kuzaliwa kwake ni furaha kubwa na wakristo hawana budi kusherehea kwa kufurahi kwani imefunuliwa neema ya Mungu inayowakomboa wote.
“Krismasi ni kipindi cha neema na fursa adhimu ya kufurahi, kubaki na neema hizi alizotuletea Yesu, basi tuwe na shukrani pia kuthamini kile ambacho Mwenyezi Mungu ametujalia katika siku hii muhimu,” amesisitiza
Askofu Rwoma amesema watoto ni zawadi pia mali ya Mungu siyo ya wanadamu, akimaanisha kwamba ni jukumu la kila mkristo kuhakikisha kuwa anaipokea na kuithamini zawadi ya mtoto aliyopewa pasipo kuidhuru ama kuipoteza akisema kuwa kufanya hivyo ni kumkufuru Mwenyezi Mungu.
“Endapo Bikira Maria angeshawishika kwa namna yoyote kutokumzaa mtoto Yesu nini kingetokea kwa dunia ya leo?, nani angekuja kutukomboa?, nani angetufariji katika mateso kadhaa tunayopitia kila siku?, nawasihi mzingatie mfano huu pia mmuishi Mama yetu Bikira Maria kwa kitendo chake cha ujasiri na upendo kwetu wote.”
Amewataka wanaume wote duniani kuwaheshimu na kuwathamini wanawake kwa mfano wa Bikira Maria wakizingatia alivyouletea ulimwengu mkombozi Yesu Kristo.
Aidha Askofu Rwoma amewakumbusha watanzania kuishi kwa amani, Baraka, upendo na rehema ili kuendelea kuilinda amani iliyopo ambayo kwa miaka kadhaa imekuwa ikitamaniwa na mataifa mengi ambayo yameteseka kwa siku nyingi kutokana na migogoro isiyokoma.
Akizungumzia baadhi ya wananchi wenye tama ya mali na mafanikio ya harakaharaka, Askofu Rwoma amekemea vikali tabia hiyo kwani husababisha kwa kiwango kikubwa kuwanyima wanyonge haki ya kupata maendeleo, huduma za kijamii na hata kuishi kwa amani.
“Tuthamini ufukara kwani utajiri na fahari vinapita tu, haya yote siyo kikwazo cha wewe kuingia mbinguni, la msingi hapa ni kupokea kwa unyenyekevu yote tunayoelekezwa kwa namna yoyote ile pia kuridhika na tukipatacho kwani kinatoka kwa Mwenyezi Mungu, kufanya hivyo kutampendeza yeye na hatimaye tutakuwa katika mazingira mazuri zaidi,” amesema Askofu Rwoma
Askofu Rwoma pia amekemea vikali tabia ya uharibifu wa mazingira iliyokithiri katika maeneo mbalimbali nchini akiitaka jamii kuacha mara moja tabia hiyo kwani isipokoma italiingiza taifa katika ukame, njaa na kusababisha vifo na migogoro isiyo ya lazima.
Ameitaka serikali kufanya jitihada za kina kukomesha hali hiyo ya uharibifu wa mazingira na ikiwezekana itoe adhabu kali kwa wote watakaoendelea na tabia hiyo inayotishia uhai wa wanadamu na viumbe hai vingine.

Na Bernard James

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU