Simanzi yatawala mazishi ya Pardi Andrew Lupondya



Maaskofu wa majimbo manne , mapadri , watawa na mamia ya waamini  wameshiriki misa ya mazishi ya Padri Andrew  Lupondya (33)  na watoto watano wa  shirika rafiki wa utoto wa Yesu (VIFRA)  na mlezi wao Mama Judith  Kajwahula (63 )  wa jimbo Katoliki Kahama waliofariki  katika ajali ya gari.

Ajali hiyo ilitokana na gari walilokuwemo kugongana uso kwa uso na roli aina ya fuso Disemba 24  na marehemu wamezikwa katika eneo la kiwanja cha  kanisa kuu la Mtakatifu Karoli Lwanga parokia ya Kahama mjini.

Misa ya mazishi  imefanyika katika kanisa kuu la jimbo na  imeongozwa na Askofu Fravian Kasala wa jimbo Katoliki Geita, pamoja  na  Maaskofu  Liberatus  Sangu wa Shinyanga, Joseph Mlola wa Kigoma  na mwenyeji Askofu Ludovick Minde wa Kahama.

Akihubiri katika misa hiyo Askofu wa jimbo Katoliki Shinyanga Liberatus Sangu amesema “Kifo ni fumbo la Kristo, alishinda  mauti kwa kufa na kufufuka kwa imani tumeshirikishwa  toka tulipobatizwa  ndani yake, hivyo kutokea kwa msiba huo mkubwa uliowapata  wana jimbo la Kahama uzidi kuwaimarisha  katika imani  yetu kwa upendo na mshikamano.”

Askofu Sangu ameongeza “Huruma ya Mungu haina mpaka, tuikimbilie siku zote katika mateso, furaha na kudumu kwenye imani yetu  kwa kuongozwa na Yesu Kristo na Roho Mtakatifu na tuwaombee Padri Lupondya na watoto na mlezi wao waliofariki  katika ajali hiyo wakiwa kwenye utume wa  sala ndani ya kanisa Mungu aweze kuwapokea kwake mbinguni.”

Aidha katika salamu za  rambirambi  zilizotolewa na Askofu Joseph Mlola wa Kigoma amesema  kamwe wasimruhusu shetani japo msiba huo ni mkubwa  ndani ya kanisa na inauma sana na kuwataka waumini wawe na imani  kwa kuwa kifo siyo mwisho wa maisha bali ndiyo mwanzo wa maisha ya milele  huko mbinguni huku akiwaalika wakristo  kuwaombea.

Naye Askofu Flavian Kasala wa jimbo Katoliki Geita amesema “Kwa kuwa kifo kimewapata wakiwa katika harakati za sala katika kupokea  kuzaliwa kwa Masiha Yesu Kristo mkombozi wetu  pamoja na masikitiko yetu tuwe na matumaini Bwana hatatuacha, tuwaombee Mungu aweze kuwapokea katika makao ya milele.”

Katika  salamu zake za pole Askofu mkuu wa jimbo kuu Katoliki Dar-es-Salaam, Mwadhama Polyicarp Kardinali Pengo alizomtumia Askofu wa jimbo Katoliki Kahama Ludovick Minde na waamini wote, amewataka kupokea msiba huo kwa matumaini ya kipasaka kwa kuwa wamepata waombezi wao huko mbinguni.

Mkurugenzi wa mashirika ya kipapa Padri Jovitus Mwijage ametoa pole kwa kifo cha Padri na kuwapoteza wamisionari hao wadogo na kusema kwa kuwa wamefariki wakiwa katika utume huo  mashirika yataendelea kuwaombea  kwa sala wapumzike kwa amani.

Askofu wa jimbo Katoliki Kahama Mhashamu Ludovick Minde Katika shukrani zake, amewashukuru Maaskofu, mapadri na  watawa  wote kwa pole na faraja walizompatia yeye na waamini wote jimboni hapa na kuwa hilo limekuwa kumbukumbu ya Huruma ya Mungu na kwa Krismasi ya mwaka huu na kuwataka wana shirika kuendelea kukua na kuongeza siku zote Katika imani.

Marehemu Padri Lupondya aliyekuwa paroko msaidizi katika kanisa  kuu la jimbo la Mtakatifu Karoli Lwanga parokia ya Kahama mjini amezaliwa mwaka 1983 akapewa daraja la ushemasi 17/ 11/ 2014 na kupewa  daraja ya Upadri 25/7/2015 jimboni hapa .

Padri Lupondya alifariki dunia jumamosi Disemba 24 alasiri  kwa ajali ya gari yake aliyokuwa akiendesha aina ya Toyota Hilux  akiwa amewabeba watoto wa shirika rafiki wa Yesu VIFRA  na mlezi wao walipokuwa wakitoka parokia ya Ekaristi Takatifu Kabuhima kwenda Karoli Lwanga Kahama mjini walipogongana uso kwa uso na roli aina ya fuso na kusababisha vifo vya watoto watano na mlezi wao Mama Kajwahula.

Watoto waliofariki wa VIFRA ni Carolina Zacharia (11) Emiliana Boniphace (12) Anisia Marco (14) Eva John (9) Paschal Bwile ( 16) na mlezi wao wa jimbo la Kahama Mama Judith Kajwahula (63), kwa pamoja na Padri Lupondya  wamezikwa jumatano Disemba 28 katika eneo  la kiwanja cha kanisa kuu la Mtakatifu Karoli Lwanga parokia yao ya Kahama mjini.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU