Watanzania wengine watunukiwa nchini Kenya

CHUO Kikuu cha Kikatoliki cha Afrika Mashariki na Kati, (AMECEA-CUEA), kimewatunuku Mapadri Watanzania wawili ambao ni wahadhiri wanaofundisha katika chuo hicho baada ya kutambua mchango wao wa kitaaluma kwa jamii.
Imekuwa ni furaha, hamasa na changamoto kwa Wahadhiri na wanafunzi hasa Watanzania wanaosoma chuoni hapo baada ya wahadhiri hao wawili kutunukiwa hadhi ya juu ya kitaaluma “Profesa” wakiwa wamekidhi vigezo na masharti vinavyomwezesha mhusika kufikia hatua hiyo.
Aliyekuwa Makamu Mkuu wa Chuo katika Utawala, ( DVC) Padri  Profesa Juvenalis Baitu,  amewatangaza rasmi katika tafrija iliyoandaliwa na Umoja wa wanafunzi Watanzania wanaosoma CUEA - UTASCU ( Union of Tanzania Students CUEA), na kuwatambulisha maprofesa wapya waliotunukiwa hadhi hiyo kuwa ni Padri Profesa Nicholaus Segeja kutoka Jimbo Kuu Katoliki Mwanza na Padri Profesa Richard Rwiza, Padri wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha.
Kama ilivyo desturi ya Umoja wa wanafunzi Watanzania wanaosoma CUEA – UTASCU kukutana kila muhula mpya wa masomo kuwakaribisha wanafunzi wapya waliojiunga chuoni hapo, kwa namna ya pekee mhula huu, wamekutana kwa lengo la kuwapongeza na kuenzi kazi njema na hatua waliofikia Wahadhiri wao wanaotoka Tanzania, pamoja na kuwaaga viongozi waliomaliza muda wao madarakani na kuwakaribisha viongozi wapya.
Akizungumza katika hafla hiyo Aliyekuwa Makamu Mkuu wa Chuo katika Utawala, ( DVC) Padri Profesa Juvenalis Baitu Mtanzania anayetoka Jimbo Katoliki Bukoba, amesema ni vema wanafunzi wakajikita katika kutumia muda vizuri wawapo masomoni na wakishamaliza warudi mara nchini Tanzania kutumia taaluma waliyoipata.
Aidha amewataka wanafunzi wawapo chuoni kutambua kuwa wamebeba dhamana ya watu wengi wakiwemo wazazi, wafadhili wao, jumuiya na mikoa watokayo nchini Tanzania na dhamana ya maisha yao wenyewe, hivyo wanapaswa kuwa mabalozi wema kila wakati katika kuiwakilisha vyema Tanzania nchini Kenya kwa uwepo wao.
 “Utanzania na Uzalendo utuunganishe bila kujali protokali tulizonazo” Amesema Profesa Baitu.
Akizungumza kwa niaba ya mwenzake kwenye hafla hiyo, Padri Nicholaus Segeja  amemshukuru Mungu aliyewawezesha kufikia hatua hiyo na pia Umoja wa Watanzania kwa kuandaa tafrija hiyo ili kutambua hatua waliyofikia, na kwa kujumuika pamoja kama familia ya Watanzania, hivyo amepongeza uongozi ulitoka madarakani kwa kazi nzuri na kuwakabidhi uongozi mpya kwa furaha.
“Tangu mlipochaguliwa mmeulinda umoja huu haukufia mikononi mwenu, kadhalika nanyi mnaopokea jitahidini umoja huu usifie mikononi mwenu” amesema Profesa Segeja.
Ili kufikia mafanikio, Profesa Segeja amesisitiza kufanya kazi kwa umoja, mshikamano na kushirikishana siri ya mafanikio bila kujali tofauti za rika na nyadhifa, huo ndiyo ukarimu unaotutambulisha Watanzania.
Katika mahojiano na KIONGOZI, Profesa Segeja amesema amekuwa Profesa katika masuala yahusuyo Teolojia ya Kichungaji.
Naye Mwenyekiti mpya wa UTASCU, Padri Onesmo Shingelwa kutoka Jimbo Kuu Katoliki Mwanza, amemshukuru Mungu na wanaumoja huo kwa kumwamini na kumchagua kuwa Mwenyekiti.

 “Umoja wa Watanzania utajengwa na Watanzania wenyewe, hivyo kila mmoja ajisikie huru kujiunga” amesema Padri Shingelwa. Padre Onesmo Shingelwa, ameahidi kuimarisha umoja zaidi na amesema furaha yake itakamilika kuona umoja huo unasonga mbele.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU