‘TUSIPOKUWA IMARA SAKRAMENTI YA KITUBIO ITAPOTEZA MAANA YAKE’



IMEELEZWA kuwa changamoto nyingi zinazoikumba Sakramenti ya Kitubio katika ulimwengu wa leo zinazweza kuwatikisa waamini kiimani iwapo hawatasimama imara.
Hayo yamebainishwa na Sista Magdalena Laurent, katika Kongamano la Ekaristi Takatifu Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam, lililofanyika Oktoba 8 katika viwanja vya Msimbazi Center, na kuhudhuriwa na waamini kutoka parokia mbalimbali za jimbo hilo.
Akielezea juu ya changamoto kadhaa zinazoikumba imani ya ukristo katika ulimwengu wa leo, Sista Magdalena amesema kuwa kila Sakramenti  ina changamoto zake, lakini Sakramenti  ya kitubio ina changamoto nyingi kwani watu wengi katika ulimwengu wa leo wanashindwa kuipokea. 
“Katika uhalisia wa maisha tunazungukwa na imani mbalimbali, tunasoma vitabu na vijarida, mitandao pia inarusha mafundisho mbalimbali yenye uzushi pia juu ya Sakramenti ya Kitubio. Tusipokuwa imara changamoto hizi zinaweza kututikisa katika imani hasa katika kupokea kitubio. Pia kuna mbinu na mitego mbalimbali ya shetani kutufanya tuone dhambi ni kitu cha kawaida katika ulimwengu wa leo” ameeleza Sista Magdalena.
Aidha Sista Magdalena ameonya kuwa kuna hatari ya watu kupuuzia dhambi na neno dhambi kuonekana kupitwa na wakati, huku wakijaribu kuhalalisha kila kitu.
“Maadili yanamomonyoka kwa kigezo cha kwenda na wakati. Amri za Mungu tunazirahisisha;  Amri ya 1 inageuzwa na kuwa abudu miungu wengine upate heri duniani, ndiyo maana tunashuhudia kuibuka kwa dini za ajabu, dini za shetani, na nguvu za shetani katika ushirikina. Amri ya pili inageuzwa kuwa taja jina la Mungu katika kuficha uovu na kusema uongo. Mungu anatumika katika kuficha ukweli” ameongeza.
Akitaja hatari nyingine za kiroho katika ulimwengu wa leo Sista Magdalena ametahadharisha juu ya watu kukwepa kitubio kwa hofu ya kupoteza uhuru wa kufanya starehe, kutokuamini huruma ya Mungu ya milele, kutoamini uwepo wa maisha ya baadaye, yaani ponda mali kufa kwaja.
“Wengi wetu tuna aibu ya kitubio, tunajihoji kuwa padri atanionaje na siyo Mungu atanionaje. Pia tuna tabia ya kuziunganisha dhambi ‘najuta na zile nilizosahau’ na kwa kufanya hivyo tunatenda dhambi nyingine katika kitubio yaani kusema uongo. Kama hatuna aibu katika kutenda dhambi, kwa nini tunaona aibu kwenda kwenye kitubio” amesema.

Akijibu baadhi ya maswali kutoka kwa waamini, hasa juu ya changamoto ya wakristo kutetereka kiimani, Padri John Kulwa amewataka wazazi kuwarithisha watoto wao imani Katoliki wakiwa bado wadogo ili kuwaimarisha na harati za kiroho.
 “Anza na mtoto wako, tangu akiwa tumboni mfundishe imani, kwa kuishi kiaminifu miguu miwili ndani ya kanisa katoliki. Ukifanya hivyo, tamaa yako ya kupenda kanisa itatiririka kwa mtoto, na itampa imani wakati wa majaribu. Mkiona watoto wenu wanalega katika imani jichunguzeni” ameeleza.
Ekaristi Takatifu na huruma ya Mungu ndani ya familia
Kwa upande wake Padri Novatus Mbaula amesema kuwa familia ni jumuiya ya watu wanaounganishwa kwa upendo wa kiagano, asili ya huruma kati ya mume na mke, na hivyo kuzitaka familia kuwa  chombo cha huruma ya Mungu kwa wanadamu, kwa kuwa sakramenti zote za Kanisa huanzia nyumbani.
“Ekaristi Takatifu inatupa changamoto ya kuhurumiana ndani ya familia, yaani kumkaribisha Kristo katika mahusiano ya wana familia. Kama hakuna umoja na mawsiliano ya kifamilia hakutakuwa na huruma. Vijana wengi wanaoitwa katika wito wa upadri, hatuwahurumii badala yake tunawakimbiza katika mambo mengine, hii ni kwa sababu hatutambui na kuthamini malengo yao na wito wao” amesema Padri Mbaula.
Aidha ameongeza kuwa familia zinaweza kuwaonea wengine huruma ikiwa tu watayatambua mahitaji yao ya msingi, ya kimwili na kiroho.
“Upendo na huruma tunaouonyesha nje ya familia, ni changamoto inayotutaka tufanye hivyo hivyo ndani ya familia, kadhalika ukarimu wa ndani ni changamoto ya kutoa ukarimu huo nje” ameongeza.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU