Utukufu kwa Mungu juu Mbinguni






HAPANA shaka sote tunaufahamu utenzi huo kwani tunauimba kila Sikukuu na Dominika isipokuwa Dominika za Kipindi cha Majilio na Kwaresima. Katika tafsiri mpya ya Kanuni ya Misa kumekuwa na mabadiliko ambayo tungependa kuyaelezea katika makala haya.
Utenzi wa Doksolojia
Awali ya yote tuufahamu mfumo wa utenzi wenyewe. Huo ni utenzi wa doksolojia. Neno doksolojia nalo ni la kigeni; linatoka katika lugha ya kigiriki au  kiyunani ‘doksa’ maana yake  utukufu. Doksolojia (kwa kiingereza  doxology)  ni sala inayotoa sifa ya utukufu kwa Mwenyezi Mungu, aghalabu  kwa nafsi zote tatu.
Tunazo doksolojia mbalimbali lakini zilizo muhimu hasa ni hizi zifuatazo: Doksolojia ndogo, ambayo hutumika mara nyingi katika Liturujia na hata katika Sala za Ibada mbalimbali ni: Atukuzwe Baba, na Mwana na Roho Mtakatifu, kama mwanzo na sasa na siku zote na milele, Amina. Katika Liturujia, doksolojia hiyo  hutumika katika kuadhimisha Liturujia ya Vipindi, yaani katika kusali Sala ya Kanisa. Husemwa kila baada ya zaburi. 
Utenzi huo wa Utukufu kwa Mungu juu mbinguni huitwa doksolojia kubwa kutokana na urefu wa sala yenyewe. Pengine huitwa Utenzi wa Malaika kwa sababu maneno ya mwanzo wa utenzi huo yaliimbwa na Malaika wakati wa kutangazwa kuzaliwa kwake Bwana Yesu (Rej Lk 2:14).
Tena, tuna  doksolojia kuu ambayo inahitimisha Sala Kuu ya Ekaristi wakati wa Misa. Kuhani huinua patena yenye hostia takatifu na kalisi ya Damu takatifu na kusali: “Kwa njia yake, na pamoja naye, na ndani yake, Wewe, Mungu Baba Mwenyezi, katika umoja wa Roho Mtakatifu, unapata heshima yote na utukufu, milele na milele.” Waamini wote huitikia kwa sauti ya kushangilia: Amina.
Katika sherehe hutakiwa kuitikia mara tatu kwa kuimba: Amina, Amina, Amina. Hiyo ni doksolojia kuu kwa sababu inafungia Sala Kuu ya Ekaristi ambayo ni kiini cha Sala zote katika kuadhimisha Ekaristi.
Tukirejea kwenye utenzi wa Utukufu kwa Mungu juu mbinguni, tangu karne za mwanzo za Ukristo,  utenzi huo ni wa  kumwabudu na kumtukuza Mungu. Maneno yake  ya ufunguzi yaliimbwa na Malaika;  una maneno yenye mkazo mkubwa katika kumtukuza, kumpa Mungu sifa kuu, na heshima kubwa anayostahili, yaani kumwabaudu.
Kwamba Mungu ni Mfalme mkuu wa ulimwengu ni ukweli ambao Wakristo wanauungama katika utenzi huu pia. Mungu aliye Mfalme  mwenye enzi kuu ndiye pia Baba yetu kama Kristo alivyotufunulia na kutufundisha kusali:  “Basi ninyi salini  hivi: Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje ...” (Mt 6:9).
Yesu anapoweka mkazo kuhusu kusameheana, anasisitiza pia kwamba Mungu ni Baba yetu aliye mbinguni: “Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe makosa yenu(Mt 6:14-15). Mungu Baba yetu wa mbinguni atatutendea sisi kama sisi tunavyowatendea wenzetu.
Sehemu kubwa inayofuata ya utenzi huo hutoa sifa na utukufu kwa nafsi ya pili, Bwana wetu Yesu Kristo. Wakristo humpa sifa na utukufu Bwana Yesu kama Mungu anayeokoa kama jina lake Yesu linavyomaanisha. Hukiri imani kuhusu nafsi ya Yesu kwamba ni Mwana pekee wa Baba, na kwamba siyo tu  Mwana wa Mungu bali yeye mwenyewe pia ni Mungu.
Utenzi huo umetungwa katika msingi wa Maandiko Matakatifu ambayo humtaja Yesu kuwa ni Mwanakondoo wa Mungu. Mtunzi ametumia jina Mwanakondoo ambalo Yohane Mbatizaji alilitumia alipomwonesha Yesu kwa watu kama tunavyosoma  katika Injili ya Yohane kwamba Yesu ni Mwanakondoo anayeondoa dhambi za ulimwengu( Rej Yn 1:29).
Jina hilo kwamba Yesu ni Mwanakondoo wa Mungu hudokeza fumbo la Pasaka. Amekuwa Mwanakondoo halisi wa Pasaka kwa sababu,  kwa kufa kwake msalabani ameondoa dhambi za ulimwengu wote. Katika  kitabu cha Ufunuo, mwandishi hulitumia mara nyingi sana jina hilo, Mwanakondoo, hasa katika sura ya 5, 7,14 na 21.
Baada ya kukiri imani hiyo kwamba Yesu ni Mungu anayeokoa, ni Mwanakondoo wa Mungu, ndipo huja maombi kwamba atuonee huruma na atuondolee dhambi zetu.  Tunakumbushwa kwamba katika Liturujia yatupasa kwanza kukiri imani halafu kutoa maombi yanayojengwa  juu ya imani tunayoikiri.
Kabla ya kutoa sifa kwa Roho Mtakatifu, utenzi hutoa tena sifa na utukufu kwa Yesu kama zile  alizopata Baba. Sifa hizo ni kwamba yeye ni Mtakatifu na  ana enzi kuu. Yesu anatawala mbinguni pamoja na Roho Mtakatifu  katika utukufu uleule  wa Mungu Baba.
Tafsiri mpya
Katika tafsiri mpya tunapaswa kuwa makini sehemu zifuatazo: sehemu ya mwanzo kabisa; na amani duniani kwa watu aliowaridhia. Katika tafsiri ya zamani tulizoea kusema: na amani duniani kwa watu wenye mapenzi mema. Kwa vile mwanzo wa utenzi huo ni wimbo wa Malaika, uamuzi umekuwa kutumia neno aliowaridhia kama ilivyo katika Biblia.
Hapo tukumbuke kwamba kuna tafsiri kadhaa za Biblia katika lugha ya Kiswahili. Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania liliamua kutumia katika Maadhimisho ya Liturujia tafsiri ile  iliyotolewa na Chama cha Biblia Kenya na Tanzania mwaka 2004 na ikachapwa tena na Jimbo la Bologna, Italia kwa niaba ya Baraza la Maaskofu Tanzania, 1997; Jimbo Katoliki la Iringa lilipewa dhamana ya kuwasiliana na wachapaji. Kwa sababu hiyo pengine toleo hilo huitwa Biblia ya Iringa.
Katika kutoa sifa na utukufu kwa Bwana wetu Yesu Kristo tafsiri ya zamani ilisema: mwenye kuondoa dhambi za dunia... kumbe katika tafsiri mpya sasa tunasali: mwenye kuondoa dhambi za ulimwengu, utuhurumie; mwenye kuondoa dhambi za ulimwengu, pokea ombi letu.  Neno ulimwengu limetafsiriwa kutoka neno la kilatini: ‘mundus -i’ kumbe  katika tafsiri mpya neno dunia linabaki kama tafsiri ya neno la kilatini ‘terra  -ae’.  
Mwishoni mwa utenzi kuna tofauti ndogo ambayo tunapaswa kuitambua. Katika kutoa sifa za utukufu na enzi kwa Yesu Kristo tafsiri mpya inasema: Peke yako Uliye juu kabisa, Yesu Kristo...Kutokana na tofauti hizo Baraza la Maaskofu limechapa Kanuni ya Misa ndogo kwa ajili ya waamini ili waweze kufuata tafsiri mpya ya Sala hizo za Misa bila kupishana.
Tafadhali, tafadhali

Tafadhali sana, tunawahimiza wachungaji kuwahamasisha Wakristo kujinunulia vijibu hivyo vidogo vya Kanuni ya Misa ili wavitumie katika kushiriki Misa vizuri. Vinapatikana katika maduka ya vitabu na hasa katika ofisi zetu za Baraza la Maaskofu Katoliki.

Wengi wameuliza kwa nini kutafsiri upya sala hizo? Tafsiri hiyo mpya inatolewa kukidhi agizo la Vatikano  kwa  Mabaraza ya Maaskofu Katoliki duniani, kuwataka kutafsiri Sala za Liturujia kwa makini kama tulivyoeleza katika makala nyingine huko nyuma. Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania halina budi kutekeleza maagizo hayo ya Vatikano.

Comments

  1. Asante sana Mababa kwa ufafanuzi huu mzuri mno.

    Nina swali kidogo tu, kwamba ni kwanini huwa tunainama tunaposali sala hiyo ya Doxolojia ndogo yaan Atukuzwe Baba na Mwana na Roho Mtakatifu?

    Na pia ni kwa nin tunainama pale tunaposali sala iyo ya Malaika pale tunapotamka Neno Yesu Kristo "peke yako Bwana, peke yako uliye juu kabisa YESU KRISTO)?

    Na piano pale tunaposali sala ya kanuni ya Imani ya Nicea tukifika kwenye maneno AKATWAA MWILI KWA UWEZO WA ROHO MT KWAKE YEYE BIKIRA MARIA AKAWA MWANADAMU" tunainamisha vichwa, KWA NINI?

    Naomba kupata ufafanuzi kitoka kwenu mababa.

    Nitashukuru sana na Mungu awabariki.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Hii ya tatu ni agizo limeandikwa kwa Misale kubwa ya Altare. Maanake, ni unyenyekevu wa Yesu

      Ya kwanza na ya pili pia ni kwa heshima ya utatu ila haijaandikwa

      Delete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU