" TUVITHAMINI VYOMBO VYA HABARI VYA KANISA" ASKOFU NZIGILWA



Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam Mhashamu Eusebius Nzigilwa amekemea waamini wanaopenda kufuatilia vyombo vya habari vya kidunia kuliko vya kanisa na hivyo kufanya kazi ya uinjilishaji kuwa ngumu, kwani kanisa hutumia vyombo vyake kuinjilisha huku wakristo wengi wakipitwa na fursa hiyo.

Ameeleza hayo hivi karibuni wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya kutoa Sakramenti ya Kipaimara katika Parokia ya Teresia wa Mtoto Yesu, Mafia
Ambapo takribani vijana 30 walipokea Sakaramenti hiyo, idadi ambayo haijawahi kufikiwa katika kisiwa hicho cha Mafia, ambapo zaidi ya asilimia 90 ya wakazi wake ni waislamu.

 “Wangapi mnasikiliza redio za kanisa? Hamsikilizi kwa sababu mnapenda mambo ya kidunia” amehoji Askofu Nzigilwa.

Aidha  amesema kuwa Yesu aliwaagiza watu waende ulimwenguni kote wakatangaze Injili, hivyo hawapaswi kupinga agizo la Mungu, na kwamba atakayemuonea aibu naye atamuonea aibu mbele ya Baba yake.

Amewaasa vijana waliopata Sakramenti ya Kipaimara kuwa hata wao wanatumwa kuitangaza Injili, na kuwataka waitangaze Huruma ya Mungu bila uwoga kwai huu siyo wakati wa kujificha.

“Wazazi msiwalee watoto kwa kuzingatia usafi wa kimwili pekee, bali fanyeni hivyo pia kwenye usafi wa kiroho. Tusiwalee watoto kwa kuwafanya wapende kitu bali utu, kwani kitu huchakaa na hutupwa, ninyi mkizeeka watawakataa kwa kuwa  mtakuwa hamna kitu” amesisitiza Askofu Nzigilwa.

Baada ya Adhimisho hilo la Misa Takatifu ilifuata halfa iliyohudhuriwa na viongozi wa serikali na wa dini mbalimbali, huku kwa upande wa serikali Mkurugenzi Mtendaji Mafia Erick Chrisantus Mapunda amemuomba Askofu Nzigilwa afikishe salamu kwa Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo kuwa wapo tayari kutoa eneo ili ijengwe shule ya Sekondari  kidato cha tano na sita.

Pia ameongeza kuwa Serikali wilayani humo ipo tayari kutoa kiwanja kingine kwa Kanisa ili kuunga mkono juhudi za Kanisa katika kutoa huduma za afya.

“Tupo tayari kutoa eneo jingine ili kujenga kituo cha afya. Japo itakuwa mali ya kanisa tunafahamu kuwa watakaonufaika ni watanzania wote”

TEC

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU