YUBILEI YA MIAKA MIA MOJA YA UPADRI TANZANIA

 
Waamini Wawaombee  Makuhani

Waamini wachache wamepata kuuliza: Katika kuadhimisha Mwaka wa Yubilei ya Upadri, kuna nafasi ya Mapadri kufanya mazoezi mbalimbali ya kiroho. Je, waamini wanatakiwa  wafanye kitu gani hasa? Tunapozungumza kuhusu Mapadri tunamaanisha wale wote waliopata Sakramenti ya Daraja takatifu: Ushemasi, Upadri na Uaskofu ambayo ni  Daraja ya Upadri katika ukamilifu wake. Tuone uzito wa madaraka waliyopewa wakati wa Liturujia ya Daraja Takatifu, halafu tutaona nini kinachotakiwa.

Daraja Takatifu ya Ushemasi
Kanisa Katoliki lina utaratibu madhubuti wa kuwaweka wakfu makuhani wa  kuadhimisha Liturujia takatifu na  kuwatumikia waamini katika yale yamhusuyo Mwenyezi Mungu (Rej. Ebr 5:1). Kanisa linatoa malezi kwa muda wa kutosha ili  kuwaandaa  kitaaluma na kuwajenga kimaadili vijana wale wanaotaka kuwa makuhani. Kisha hutoa Daraja takatifu katika Liturujia maalum. 

Daraja kubwa ya kwanza ni Ushemasi. Katika Liturujia ya Ushemasi Wakristo hukumbushwa wajibu wa Shemasi kwamba: “humsaidia Askofu na Mapadri katika huduma ya Neno la Mungu, Altare na ya upendo”(Liturujia ya Ushemasi).  Shemasi anapaswa kuhubiri Injili, kuandaa vipaji kwa ajili ya sadaka ya Ekaristi na kuwagawia waamini Mwili na Damu ya Bwana.Kama anaagizwa na Askofu, anakuwa na wajibu wa kuwaonya na kuwafunza katika mafundisho ya Kristo waamini na wasio waamini, kuongoza sala, kuadhimisha Sakramenti ya Ubatizo, Ndoa na kuwapelekea waliopo kufani Komunyopamba, kuongoza Liturujia ya mazishi.

Katika Liturujia ya kutoa Daraja takatifu, kabla ya kuwekewa mikono kijana anaulizwa maswali kadhaa na hujibu: Nataka. Swali la mwisho katika mfululizo wa maswali hayo linasema: “Je, wataka kulinganisha bila kukoma maisha yako na mfano wa Kristo, ambaye Mwili na Damu yake utavigusa altareni?” Kujibu swali hili  Mteule hutanguliza kuomba msaada wa Mungu hivi: “Kwa msaada wa Mungu, nataka.” Kwa kuulizwa vile  Liturujia inaweka wazi kwamba mtu halazimishwi bali mbele ya waamini anaamua mwenyewe kuitika wito wa Mungu na kupata Daraja takatifu ya Ushemasi.

Baada ya kumpa  Daraja ya Ushemasi, Askofu humkabidhi Shemasi mpya Kitabu cha Injili na kumwambia hivi: “Pokea Injili ya Kristo, ambayo umewekwa kuwa mhubiri wake; angalia, usadiki hayo utakayosoma, ukafundishe hayo utakayosadiki na ukashike hayo utakayofundisha.”
Basi, ili waweze kuishi kadiri ya wito wao  Mashemasi wanahitaji msaada wa Mungu. Kwa namna  ya pekee mwaka huu wa Yubilei ya Upadri hapa Tanzania, waamini wanatakiwa kuwaombea Mashemasi na Makuhani wao.

Daraja Takatifu ya Upadri
Kama inavyokuwa katika Liturujia ya kupata Ushemasi, Liturujia ya Daraja Takatifu ya Upadri hufuata utaratibu uleule. Shemasi  akishaitwa na kuitika, Askofu anayetoa Daraja Takatifu anamjulisha rasmi kwa waamini na kuwaeleza hadhi ya Upadri na wajibu wake. Sehemu ya mafundisho hayo ya utambulisho inasema: “Na ndugu huyu baada ya kufikiriwa sana anawekwa sasa katika Daraja ya Upadri ili naye apate kuwa mhudumu wa Kristo Mwalimu, Kuhani na Mchungaji. ...Naye atafananishwa na Kristo aliye Kuhani mkuu na wa milele, na ataunganishwa na ukuhani wa Maaskofu; yaani atawekwa wakfu kuwa kuhani halisi wa Agano Jipya ili aihubiri Injili, alichunge taifa la Mungu na kuziadhimisha Ibada takatifu, hasa sadaka ya Bwana.”

Kisha utambulisho kwa waamini, Askofu humwelekea Shemasi na kumwambia wajibu wake atakaotekeleza baada ya kuwekewa mikono na kuwa Padri. Sehemu ya mafundisho hayo  inasomeka hivi: “Hivyo uwagawie  wote lile Neno la Mungu ambalo nawe ulilipokea kwa furaha. Unapotafakari sheria ya Bwana angalia usadiki kile unachokisoma, na kufundisha kile unachokisadiki, na kufuasa kile unachokifundisha. ...ili kusudi kwa neno na kwa mfano upate kuijenga nyumba yaani Kanisa la Mungu.” Hayo yanahusu wajibu wa Padri wa kufundisha na kuhubri Neno la Mungu. Anatakiwa kuhubiri siyo tu kwa maneno bali pia kwa mfano wa maisha yake.

Kuhusu wajibu wa kutakasa kwa kuadhimisha Sadaka ya Bwana anaangalishwa hivi: “Kwa hiyo elewa vizuri unachokifanya, na iga unachokitenda;  na kwa kuwa unaadhimisha fumbo la kifo na ufufuko wa Bwana, jitahidi kutiisha viungo vyako kwa kukomesha vilema vyote na kuenenda katika upya wa uzima”. Mafundisho hayo ni mazito; Padri inampasa kuadhimisha Ekaristi kwa ibada na uchaji, kwani anaadhimisha tendo takatifu sana. Anatakiwa kujitahidi kuishi katika maadili mema. Katika mfululizo wa maswali ya kumhoji, hujibu daima: Nataka.  Swali la mwisho, lakini linasema hivi:

“Je, wataka kujiunga zaidi siku hadi siku na Kristo Kuhani Mkuu ambaye alijitoa mwenyewe kwa Baba kuwa sadaka safi kwa ajili yetu na pamoja naye kujiweka wakfu kwa Mungu kwa ajili ya wokovu wa watu?”
Hapo Padri-mteule anahitaji sana msaada wa Mungu na hujibu: “Kwa msaada wa Mungu, nataka”. Swali hili linahusu jitihada ya Padri mpya kujiunga na Kristo na kujiweka wakfu kwa Mungu siku kwa siku.  Jitihada ya kuwa mwadilifu na kufanana na Yesu Kristo ni jambo la kila siku. Katika mwaka huu maalum Wakristo wanatakiwa kuwaombea Mapadri ili Mwenyezi Mungu awawezeshe kuishi kadiri ya wito wao. Mara nyingi baadhi ya waamini hupenda kuwasengenya na kuongea kuhusu  mapungufu ya Makuhani; lakini kwa wito maalum wa Yubilei ya  Miaka 100 ya Upadri  waamini wafanye bidii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya miito ya Upadri na kuwaombea Makuhani wao.

Daraja Takatifu ya Uaskofu
Daraja Takatifu ya Uaskofu ni kilele cha Sakramenti  ya Daraja Takatifu, kwani ni Urika wa Mitume. Mafundisho anayopewa Askofu-mteule ni mazito zaidi ya yale ya Upadri. Anakumbushwa kwamba kuwa Askofu ni kuwa mtumishi, wala siyo adhama. Askofu anatakiwa kutumikia na siyo kutawala. Katika mahojiano kuhusu     
                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                      kupokea utumishi huo anaulizwa maswali tisa. Swali la tisa linasimama hivi: “Je, wataka kumwomba bila kukoma Mungu Mwenyezi kwa ajili ya taifa lake takatifu na kutekeleza utume wa ukuhani mkuu pasipo lawama?” Askofu-mteule hujibu: “Naam, kwa msaada wa Mungu, nataka.”

Katika Liturujia ya kumweka wakfu Askofu-mteule, mashemasi wawili hushikilia Kitabu cha Injili kinachowekwa juu ya kichwa chake, ishara ya madaraka  ya kuwa Kuhani mkuu na wajibu wa kwanza wa kuhubiri na kutetea imani. Mteule yampasa kujibu  kwa dhati ya moyo wake  Nataka” au Kwa msaada wa Mungu, nataka”, mbele ya Mwenyezi Mungu;  kutekeleza  hayo yote  anahitaji  sana msaada wa Mwenyezi Mungu. Kwa hiyo kabla ya kupewa Daraja takatifu Liturujia imeweka nafasi muhimu kwa waamini wote kumwombea  kwa Maombi makuu ya Litania  wakati huo Mteule anakuwa amelala kifudifudi ili kujinyenyekea kwa Mwenyezi Mungu na kumuomba kwa dhati neema zake.

Hatima
Tumeona kwa kifupi Liturujia ya Daraja takatifu. Kwa kuzingatia madaraka mazito wanayotwishwa katika kupata Daraja takatifu, katika mwaka huu wa Yubilei ya miaka 100 ya Upadri hapana budi Wakristo kuwaombea Makuhani kwa bidii ili hayo waliyoahidi wakati wa kupewa Daraja Takatifu waweze kuyaishi.  Umuhimu huo wa kuomba siyo tu kwa nafasi hii ya Yubilei, bali kila siku Wakristo wanatakiwa kuwaombea Makuhani wao. Nao Makuhani wanatakiwa pia kuwaombea waamini wao kama  wanavyoahidi katika Liturujia ya Daraja takatifu.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU