Sinodi ya Maaskofu kwa vijana kufanyika 2018

MAADHIMISHO ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya vijana yanatarajiwa kufanyika Oktoba 2018 na kuongozwa na kauli mbiu “Vijana, Imani na mang’amuzi ya Miito”. Maandalizi ya sinodi hiyo yameanza kwa Sekretarieti kuu ya Sinodi za Maaskofu kutoa Hati ya Maandalizi ya Sinodi ya XV ya Maaskofu kwa ajili ya vijana. Hati hiyo inatoa mwaliko wa kumfuata Yohane, mwanafunzi aliyependwa zaidi na Yesu.
Hati hiyo pia inaangalia hali ya vijana duniani: utambulisho na ushiriki wao, mambo rejea binafsi na taasisi pamoja na mchakato wa kuunda vijana wa kizazi kipya wanaoshikamana zaidi. Sura ya pili ya hati hiyo inajikita katika imani, mang’amuzi na wito kwa kuzingatia umuhimu wa imani na wito katika maisha ya vijana; zawadi ya kufanya mang’amuzi ya miito ili kutambua, kutafsiri na kuchukua maamuzi ya maisha.
Sura ya tatu inapembua kwa kina shughuli za kichungaji kuhusu miito kwa kuwataka viongozi wa Kanisa kufanya hija na vijana katika maisha yao, ili hatimaye waweze kutoka, kuona na kuitikia wito wa kumfuata Kristo Yesu. Walengwa wakuu ni vijana wote bila ya ubaguzi; Jumuiya inayojihusisha na malezi ya miito pamoja na kuwa na watu ambao ni mfano bora wa kuigwa.
Shughuli za kichungaji kwa ajili ya miito zinatekelezwa katika maisha ya kila siku sanjari na ushiriki mkamilifu katika masuala ya kijamii. Hati inachambua maeneo maalum ya shughuli za kichungaji bila kusahau ulimwengu wa mitandao ya kijamii, ambamo vijana wengi wanapenda kuogelea huko.
Mwishoni, Hati hii inamwangalia Bikira Maria aliyehifadhi, akatafakari na kumwilisha Neno la Mungu katika maisha yake, ili aweze kuwasindikiza vijana katika safari ya maisha ya miito yao. Kuna maswali dodoso yatakayosaidia kuandaa Hati ya Kutendea Kazi, maarufu kama “Instrumentum Laboris”, kwa kuangalia hali ya kila bara. Namna ya kukusanya takwimu, kuzitafsiri na kuzifanyia kazi.
Hati yenyewe
Katika utangulizi wake, Hati ya Maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya vijana, inatoa mwaliko kwa vijana wote ili waweze kupata utimilifu wa furaha ya maisha, kwani Kanisa limekabidhiwa dhamana ya kutangaza na kushuhudia Furaha ya Injili.
Huu ni mwaliko wa kuwasaidia vijana ili kupata mang’amuzi kuhusu miito mbali mbali ndani ya Kanisa kama: watu wa ndoa, watawa na mapadri, ili kwa njia ya mwanga wa imani, wawe tayari kushuhudia utimilifu wa furaha katika miito yao.
Sura ya kwanza: Hali ya Vijana Duniani! Sura hii inapembua hali ya vijana duniani ili kugusa undani wa maisha ya vijana kimaadili na kiroho, tayari kufanya mang’amuzi ya maisha na wito wao. Kuna hali ya kutojaliana, idadi ndogo ya watoto wanaozaliwa; tamaduni na mapokeo ya imani ya Kanisa toka nchi moja hadi nchi nyingine.
Bado kuna ubaguzi kati ya watoto wa kike na kiume. Vijana wanaojadiliwa ni wale wenye umri kati ya miaka 16- 29 lakini pia umri huu unategemea na mahali walipo vijana.
Dunia inabadilika kwa kasi kubwa jambo ambalo linahitaji kuwa na sera na mikakati ya shughuli za kichungaji kwa muda mrefu. Hii inatokana na ukweli kwamba, kuna idadi kubwa ya vijana ambao hawana fursa za ajira; kuna athari za mabadiliko ya tabianchi; wimbi kubwa la wakimbizi na wahamiaji lakini pia wapo vijana wachache wanaofaidika na ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Pamoja na maendeleo yote haya lakini kuna vijana wengi bado wanajikuta wakiwa wametumbukia katika upweke hasi na hali ya kukata tamaa kutokana na utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu. Rasilimali ya dunia inatumika kwa ajili ya mahitaji ya watu wachache na kwamba, kuna uharibifu mkubwa wa mazingira hali inayotishia usalama na maisha ya kizazi kijacho!
Sura ya pili: Imani, Mang’amuzi na Miito. Mama Kanisa katika mchakato wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya vijana anataka kukutana, kuwasindikiza na kuwasaidia vijana bila ubaguzi ili kweli vijana waweze kupata utimilifu wa maisha kwa kutambua kwamba maisha na imani ni zawadi ya Mungu.
Ili kuwahudumia vyema vijana, anasema Baba Mtakatifu Fransisko kunahitajika wema, upole na majitoleo ya dhati kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Yosefu, mtu mwenye haki, jasiri na mchapakazi; aliyeonesha huruma na upendo. Kuna uhusiano wa pekee kati ya imani  na wito, kwani hapa vijana wanajisikia kupendwa na kuthaminiwa.
Imani inawasaidia vijana kujenga na kudumisha umoja, udugu na mshikamano wa dhati, tayari kushuhudia tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu, matokeo ya majadiliano ya kina katika dhamiri nyofu. Wito na mwaliko kutoka kwa Kristo Yesu, umesheheni furaha na majitoleo ya dhati ambayo yanapaswa kutakaswa, kuwekwa huru ili kutambua jambo jema na kulitenda.
Vijana wanapaswa kufanya maamuzi magumu katika maisha yao, kwa kusoma alama za nyakati na kutambua uwepo wa Roho Mtakatifu katika historia; kwa kung’amua kilicho chema na kukifuata, ili kupata utimilifu wa maisha. Mkazo ni kutambua, kutafsiri na kuchagua kile ambacho Mwenyezi Mungu anataka katika maisha ya kijana.
Sura ya Tatu: Mikakati ya shughuli za kichungaji: Sera na mikakati ya shughuli za kichungaji kwa vijana inapaswa kujielekeza mahali waliko vijana katika maisha yao ya kila siku, ili kuwasaidia kujenga historia ya maisha yao. Yesu apewe nafasi ya kuweza kutembea na vijana hatua kwa hatua ili aweze kusimama na kuwaangalia kwa jicho lenye huruma na upendo, ili kwa kufunga safari na vijana, Jumuiya nzima ya waamini iweze kujengwa na kuimarishwa.
Vijana wapewe nafasi ya kuonesha na kushirikisha kipaji chao cha ugunduzi; kwa kuwa na mwono na mwelekeo mpya na mpana zaidi katika sera na mikakati ya shughuli za kichungaji.
Hapa, Mama Kanisa anakazia mambo makuu matatu: kutoka, kuona na kuitwa. Utume kwa vijana ni mchakato unaopaswa kuwashirikisha vijana wote pasi na ubaguzi kwa kutambua kwamba, Jumuiya ya waamini nayo inawajibika barabara katika malezi, makuzi na majiundo ya vijana wa kizazi kipya.
Jambo la msingi ni ushuhuda wenye mvuto na mashiko kwa vijana kwa kuwashirikisha vijana katika maisha na utume wa Kanisa. Kanisa linawataka wazazi, walezi na familia; viongozi wa Kanisa pamoja na walimu kuwa kweli ni mfano bora wa kuigwa na vijana wa kizazi kipya.
Mwishoni, Hati ya Maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya vijana kwa Mwaka 2018 inatoa maswali dodoso ya jinsi ya kukusanya takwimu; kusoma na kutafasiri takwimu za vijana wanaohudhuria maeneo ya Kanisa, wale ambao wako nje au wale wanaojisikia kuwa ni wageni kabisa katika maeneo ya Kanisa.
Maswali ya utume kwa vijana kuhusu miito; walezi na waalimu na mwishoni maswali msingi kwa kila bara pamoja na kushirikisha wengine takwimu zilizopatikana yamekaziwa kwa wote.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU