Ujumbe wa Papa Fransisko kwa Siku ya Wakimbizi na Wahamiaji 2017

‘WAHAMIAJI wadogo ni wahanga wasio na sauti’ ndiyo kauli mbiu inayoongoza maadhimisho ya Siku ya 103 ya Wakimbizi na Wahamiaji Duniani itakayoadhimishwa na Kanisa hapo Januari 15, 2017. Baba Mtakatifu Fransisko katika ujumbe wake kwa siku hii, anaangalia kwa jicho la masikitiko mateso na mahangaiko ya watoto wadogo wanaolazimika kukimbia nchi zao na kujikuta wakiwa wanaishi ugenini.
Watoto hawa ambao “hawaonekani” na wala hawana sauti wamejikuta wakiishi katika mazingira magumu na hatarishi yanayowatumbukiza kwa urahisi katika ukahaba na biashara ya ngono; ni kundi linalofanyishwa kazi za suluba pamoja na kupelekwa mstari wa mbele kama askari.
Watoto hawa wamekuwa wakibebeshwa mzigo wa biashara haramu ya dawa za kulevya na hatimaye kutumbukizwa katika magenge ya kihalifu. Ni watoto wanaolazimika kuyakimbia makazi yao kutokana na vita, manyanyaso, dhuluma na matokeo yake wanajikuta wakiwa peke yao bila msaada wa wazazi na walezi wao. Maandiko Matakatifu yanaonya kwa ukali wale wote wanaosababisha makwazo kwa watoto wadogo.
Baba Mtakatifu amesema kuwa katika maadhimisho ya Siku ya Wakimbizi na Wahamiaji Duniani kwa Mwaka 2017, anapenda kuweka mkazo juu ya matendo na mahangaiko ya watoto wakimbizi na wahamiaji, hasa wale ambao wako pweke. Takwimu zinaonesha kwamba, kuna idadi kubwa ya watoto wanaoishi nje ya mazingira ya familia na nchi zao na hivyo kujikuta wakiwa kama wakimbizi na wahamiaji, changamoto kubwa katika ulimwengu mamboleo.
Wakimbizi na wahamiaji na watu wanaotafuta fursa za ajira, maisha bora zaidi lakini kuna watu wanaolazimika kuyakimbia makazi na nchi zao kwa matumaini ya kupata amani na usalama wa maisha.
Baba Mtakatifu anasema, waathirika wakubwa zaidi ni kundi la watoto wadogo wanaokumbana na majanga ya maisha, umaskini pamoja na matukio ambayo yanajikita katika ulimwengu wa utandawazi hasi, kiasi cha kuwatumbukiza katika biashara haramu ya binadamu.
Hili ni kundi linalohitaji mazingira ya kifamilia, ili kulindwa na kuendelezwa na wazazi pamoja na walezi wake. Watoto wana haki ya kupata elimu bora kutoka ndani ya familia na shule, ili waweze kukua na kukomaa, tayari kuwajibika barabara katika ustawi na maendeleo ya nchi zao kwa siku za usoni.
Baba Mtakatifu anasema, ili kukabiliana na changamoto hizi zote kuna haja ya kutambua kwamba, wakimbizi na wahamiaji ni sehemu ya historia ya ukombozi hata Waisraeli wanakumbushwa katika Agano la Kale kwamba, kuna wakati hata wao walikuwa ni watumwa katika nchi ya kigeni, changamoto ya kusoma alama za nyakati, ili kujenga na kudumisha umoja na mshikamano na watu wanaolazimika kuzikimbia au kuzihama nchi zao.
Watu watambue na kuguswa na mahangaiko ya wakimbizi, ili kuwaonesha ukarimu, tayari kutambua mpango wa Mungu hata katika mazingira kama haya kwani Jumuiya ya Kikristo inawaambata watu wote kutoka katika lugha, jamaa na taifa. Kila mtu ana thamani kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu na kwamba, utu na heshima ya binadamu kamwe hauwezi kulinganishwa na vitu. Ubora wa taasisi yoyote ile unapimwa kutokana na jinsi inavyotoa kipaumbele chake kwa utu na heshima ya binadamu, lakini zaidi jinsi inavyowahudumia wanyonge ndani ya jamii na katika mazingira kama haya watoto wakimbizi na wahamiaji.
Baba Mtakatifu anaitaka Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba inajikita katika sera ambazo zitasaidia kuwalinda, kuwaingiza watoto katika maisha ya kijamii sanjari na kuivalia njuga changamoto ya wakimbizi na wahamiaji duniani, ili watoto hawa wasitumbukie mikononi mwa watu waliofilisika kiroho, kimaadili na kiutu.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU