Historia ya Epifania

Makanisa ya Kikristo ya nchi ya Magharibi na Sherehe ya Epifania:
HATA kabla ya mwaka wa 354, Makanisa ya nchi za Magharibi yalikwishaiweka sherehe ya Kuzaliwa kwa Kristo kama sikukuu ya Krismasi na kuipangia siku ya kuisherehekea kwake kuwa ni tarehe ya 25 ya mwezi wa Desemba.
Tarehe ya 6 ya mwezi wa Januari ilikuwa imetengwa kwa kusherehekea sikukuu ya Epifania ya Kristo hasa ule ujio wa Mamajusi lakini pia kwa kusherehekea ubatizo na harusi ya Kana. Ilipofika mwaka wa 1955 ilianzishswa sikukuu ya pekee ya kusherehekea ubatizo wa Bwana.
Uanzishwaji wa hiyo sikukuu ya pekee ya kusherehekea ubatizo wa Bwana kwa makanisa ya nchi za Magharibi ulidhoofisha zaidi ule uhusiano uliokuwepo hapo awali kati ya sherehe ya Epifania na ile ya Kuzaliwa kwake Kristo.
Desturi za Kiliturujia zinazozingatiwa na Makanisa ya nchi za Magharibi.
Wakristo walio wengi wa nchi za Magharibi wanakuwa na siku 12 za sherehe zikianzia tarehe ya 25 ya mwezi wa Desemba na kumalizika tarehe ya 5 ya mwezi wa Januari. Hata hivyo, kwa wakristo wakatoliki, siku hizo za kipindi cha Krismasi kinaanza tangu jioni ya mkesha wa Noeli hadi Jumapili baada ya Epifania au baada ya tarehe ya 6 ya mwezi wa Januari.
Makanisa mengi, hasa yale ya Amerika Latino yana desturi ya kuendeleza kipindi hiki hadi siku arobaini kikiishia tarehe ya 2 ya mwezi wa Fubruari.
Kwa baadhi ya maeneo, hasa yale yaliyo katika nchi za Ulaya ya Kati, mapadri waliovaa mavazi meupe wanabariki maji ya Epifania, ubani na vipande vya chaki. Chaki hizo zilizobarikiwa zinatumika kwa kuandikia mifupisho ya majina ya wale Mamajusi watatu yaani Kaspari, Melkiori na Baltazari milangoni mwa majengo ya makanisa na nyumba za waamini.
Wakati wa kuandika, padri anatamka maneno ‘Christus mansionem benedicat’ yenye maana kwa lugha ya Kiswahili ‘Kristo aibariki nyumba hii.’
Makanisa ya Kiothodoksi ya Kimashariki na Sherehe ya Epifania:
Jina la sikukuu hii kama inavyosherehekewa na hayo makanisa ya Kiothodoksi ni ‘Teofani’ lenye maana inayokaribiana na ‘Mungu anayeng’ara au ‘Ufunuo Mtakatifu. ’Katika makanisa hayo, siku hii ya Teofani ni moja ya zile siku kubwa za mwaka wa liturujia, ikiwa ni sikukuu ya tatu kwa ukubwa ikitanguliwa na sikukuu ya Pasaka pamoja na ile ya Pentekoste.
Sherehe ya sikukuu hii inafanyika tarehe ya 6 ya mwezi wa Januari. Dokezo la kwanza kabisa kuhusu sikukuu hii lilitolewa na Mtakatifu Klementi wa Aleksandria kama linavyoonekana katika ‘Stromateis, I XXI, 45.’Dokezo hili linawiana na sherehe ya Kuzaliwa kwa Kristo na pia na Ubatizo wake wa tarehe ya 6 ya mwezi Januari.
Iwapo mambo ni hivyo, basi  sherehe hii inawiana pia na yale mazoea ya Kanisa la Kitume la nchi ya Armenia linalosherehekea Kuzaliwa kwa Kristo tarehe ya 6 ya mwezi wa Januari likiitaja sikukuu hiyo kuwa ni ya Kuzaliwa na pia ya Teofani ya Bwana Wetu Yesu Kristo.
Siku hizi, katika makanisa ya Kiothodoksi ya Mashariki kinachosisitizwa zaidi ni ule Mng’aro na Ufunuo wa Yesu Kristo akiwa kama Masiha na pia akiwa kama Nafsi ya Pili ya Utatu Mtakatifu kama ilivyodhihirishwa saa ile alipobatizwa na Yohani mtoni Yordani. Siku hii inasherehekewa kwa sababu,kulingana na  mapokeo, ubatizo wa Yesu mtoni Yordani ulikuwa moja ya nafasi mbili tu ambapo Nafsi zote Tatu za Utatu Mtakatifu zilijionyesha kwa binadamu kwa pamoja.
Mungu Baba alisikika akizungumza katika mawingu, Mungu Mwana ndiye aliyekuwa anabatizwa mtoni Yordani na Mungu Roho Mtakatifu akiwa katika umbo la Hua akishuka kutoka mbinguni.Nafasi nyingine ambapo Nafsi zote Tatu zilijionyesha, ilikuwa ile ya Yesu Kugeuka Sura Mlimani Tabor. Hivyo basi, siku hii takatifu inachukuliwa kuwa ni sikukuu ya Utatu.
Kanisa la Kiothodoksi linauona ubatizo wa Yesu kama ni ngazi ya kwanza ya kuelekea mlimani Kalvari alikosulubiwa. Ili kuthibitisha wazo hili nyimbo zinazoimbwa siku ya kumbukumbu ya Kuzaliwa kwa Yesu zinafanana na zile zinazoimbwa siku ya Ijumaa Kuu.
Desturi za Kiliturujia kuhusu Epifania zinazozingatiwa na makanisa ya Kimashariki:
Mwanzo wa Sherehe: Sherehe za Kiliturujia za mwanzo wa Teofani zinaanza tarehe ya 1 ya mwezi wa Januari na zinahitimishwa kwa sala mwishoni mwa sherehe hizo hapo tarehe ya 5 ya mwezi wa Februari.
Paramonia: Paramonia ni siku ya mkesha wa sherehe ambayo ni siku ya lazima ya kufunga kwa kila mwamini asiyekuwa na matatizo ya kiafya.Waamini hawa hufunga kula chakula siku nzima hadi nyota ya kwanza inapoonekana saa za jioni. Hapo ndipo chakula pamoja na mvinyo na mafuta kinapoweza kuliwa. Katika siku hiyo husherehekewa Saa Takatifu ikiwa na kumbukumbu ya Ijumaa Kuu.
Zile Saa Takatifu hufuatiwa na Liturujia Takatifu ya Mtakatifu Basili inayoziunganisha sala za jioni na Liturujia Takatifu. Wakati ule wa sala za jioni masomo 15 ya Agano la Kale husomwa. Masomo haya yanayoonyesha ishara za Ubatizo wa Kristo husomwa pamoja na sala za antifona maalumu.
Iwapo Sikukuu ya Teofani inaangukia siku ya Jumapili au Jumatu, zile Saa Takatifu husaliwa siku ya Ijumaa inayotangulia. Sala za liturujia za Mtakatifu Yohani Krisostomi hutumika kwa kusali na mafungo hulegezwa kwa kiasi fulani.
Kubariki maji: Makanisa ya Kiothodoksi yanabariki maji siku hiyo ya Teofani. Kwa kawaida tendo hili la kubariki maji hufanywa mara mbili; mara ya kwanza hufanywa jioni ya mkesha wa sikukuu yenyewe kwenye kisima cha maji kilicho ndani ya kanisa na hufanywa tena kwa mara ya pili siku ya sikukuu yenyewe kwenye chanzo cha asili cha maji kilicho karibu na Kanisa.
Chanzo hicho kinaweza kuwa mto, ziwa, bwawa la kuogelea, bandari, ufukoni, gati n.k. Mwishoni mwa ibada padri anatoa baraka kwa yale maji. Kwa utaratibu wa nchi ya Ugiriki, baraka hiyo inatolewa kwa tendo la padri la kuutupa msalaba majini.
Kama uogeleaji unawezekana katika aina ya maji yanayobarikiwa, waamini wanaogelea kujaribu kuupata tena ule msalaba.Mwamini anayefanikiwa kuupata msalaba huo anaurudisha kwa padri anayempa mwamini huyu baraka ya pekee kwa ujasiri aliouonyesha wa kuogelea na kuupata tena ule msalaba.
Maji yanayobarikiwa siku hiyo yanachotwa na waamini na kuyapeleka majumbani kwao. Waamini hawatajibariki tu kwa kujimwagia maji yale bali pia watayanywa.
Kanisa la Kiothodoksi linafundisha kuwa maji hayo ya baraka ni tofauti na maji mengine kwa sababu utaratibu wake wa asili huwa umebadilika kutokana na ile baraka na kwa hivyo huwa hayawezi kuharibika kwa mujibu wa ushahidi wa mwujiza wa Mtakatifu Yohani Krisostomi. Siku hiyo ya sherehe ya Teofani, kwa kufuata desturi za jadi, huwa ni siku ya kuwabatiza waamini walioandaliwa kwa kubatizwa siku hiyo.
Kubariki nyumba: Siku hiyo ya Teofani padre huzibariki nyumba za waamini kwa kuingia katika kila nyumba na kuzungukia sehemu za bustani akizibariki kwa maji yale mapya yaliyobarikiwa.
Baada ya Sikukuu: Sikukuu ya Teofani hufuatiwa na kipindi cha siku 8 cha kutokuwa na ulazima wa kufunga. Jumamosi na Jumapili baada ya Teofani huwa ni siku zinazoambatana na masomo ya pekee ya ibada yenye uhusiano na kile kitendo cha ibilisi cha kumjaribu Kristo. Kwa hiyo huwa kuna mwendelezo kati ya sikukuu ya Teofani na mwanzo wa kipindi cha Kwaresima.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU