Mwanadamu na serikali

KWA kawaida vijana hawakumbuki ya kwamba kuna Serikali mpaka labda siku wanapodaiwa  kodi. Hapo hufumbuka macho wakiwaza “Serikali inataka nini nami? ina haki gani initoze kodi? Kwa kweli Serikali itasema mara kwa mara neno katika maisha yako. Afadhali ufahamu kidogo maana ya Serikali na uhusiano ulio nayo.

 Tuone Utawala wa Wazee zamani
Kama ungalizaliwa wakati wa babu zako, maisha yako yangalipangika tofauti na sasa. Zamani watu wote walikaa kama jamaa moja wakilima na kujilisha kwa mavuno ya Shambani. Mzee wa jamaa aliwasimamia watu wake, tena aliamua magomvi. Mashauri makubwa zaidi yalipelekwa kwake, ndiye mkubwa wa Ukoo.

Huyu na wazee wenzake walikuwa Serikali kwa watu wao. Ingawa ukoo ulikuwa sehemu ya kabila, wakubwa wa koo zote hawakushirikiana katika  utawala wa kabila zima, maana kila mmoja alikuwa sawa na wenzake, akishika mamlaka kwa watu wake tu isipokuwa katika shida kubwa kama vita.

Hapo walisaidiana kwa muda. Mpango huo ulikuwa wa kawaida kwa makabila mengi ya Wabantu.  Pengine Kabila moja moja lilitawaliwa na Mfalme, hasa kwa makabila yaliyopenda vita. Lakini hata kwao mashauri ya kila siku yalikatwa na mkubwa wa Jamaa.

Makabila yalikuwa mengi sana. Kila kabila lilitafuta faida yake tu. Mara nyingi halikupatana  na Kabila la jirani. Watu walikaa kwa shingo upande. Walishindwa kwenda mbali kwa hofu ya kukamatwa na adui zao au kuuawa au hata kufanywa watumwa.

Biashara au shughuli za maendeleo hazikuwa na nafasi, wala nchi haikupata nafasi ya kuinuka na kupata maendeleo. Hali kama hiyo kwa sasa hivi haina nafasi. Tumshukuru Mungu kwamba katika maendeleo ya siku hizi imefaa makabila yaunganike katika taifa, kama ilivyotendeka hapa Tanzania na kusimamiwa na Serikali kuu jinsi ilivyo.

Maana ya Serikali
Tunashukuru kwamba Serikali haipunguzi haki za kila mtu, wala kuyachukua madarakaya familia,ya jamaa ,ya kabila ,wala haimchagulii mtu kazi ya kufanya au dini n.k wala haiwazui wazazi kuwapa watoto wao malezi wanavyotaka wenyewe.

Serikali imewekwa kwa ajili ya raia, siyo raia kwa ajili ya Serikali. Kwa hiyo Serikali yafaa ifanye bidii yoyote iwatunze raia zake na kuwapa nafasi ya kuendelea vizuri badala ya kubakia nyuma.

Serikali iwasaidie katika nini?

Wajibu wa Serikali iwe ni kuwasaidia raia wake katika mambo mazuri yote wasiyoweza kuyapata kwa nguvu zao peke yao. Ni wajibu wake kutunga Sheria zitunzazo amani na utaratibu wa nchi ili raia wakae kwa raha, kuweka mapolisi waihifadhi amani hiyo na kuwaadhibu wakosefu wanaozivunja Sheria. Tena kuweka Jeshi la askari walinde mipaka ya nchi yetu na kuwazuia adui wasiishambulie.

Kujenga hospitali na kuweka Sheria za afya kama kuzuia Malaria, kifua Kikuu na Magonjwa mengineyo, kufungua biashara, barabara, njia za gari la moshi, na kufungua mapatano ya biashara  na nchi za kigeni, kusimamia vizuri miundo mbinu yote na njia zote za mawasiliano.

Serikali ina haki ya kutoza ushuru

Kwa kazi zote chache nilizozitaja hapo juu, Serikali inahitaji fedha, nayo hupatikana hasa kwa ushuru na kodi za kila namna. Ni haki ya Serikali kutoza fedha hii, kwa sababu inatumiwa kwa ajili ya raia. Hata Kanisa litakubaliana na Serikali kama inazijali Sheria za maumbile na za Mungu.

Serikali imepata mamlaka kwa Mungu

Jamaa haitoshi ijipatie mafaa yote jinsi ipasavyo, wala haiwezi kulinda amani na kuinua nchi jinsi itakiwavyo. Kwa mambo hayo inahitajika taifa na Serikali kuu kama nyongeza yake. Mungu mwenyewe ametaka taratibu hiyo alipothibitisha Sheria ya maumbile kwa amri zake kumi. Alizitangaza kwa fahari nyingi, ili watu wakiona enzi yake wazidi kuzishika, soma katika kitabu cha pili cha Musa, sura ya 19 na 20 katika Agano la Kale.

Kwa hiyo ndugu msomaji wa makala haya, uwezo wa Serikali wategemea Mungu, na wakubwa wa Serikali wamepata kwake haki yao ya kutawala. Maneno hayo yamethibitishwa  katika maandiko matakatifu. Pilato alipomwambia Yesu, “ Hujui ya kuwa nina mamlaka ya kukusulubisha na mamlaka ya kukufungua? Alijibu, “Hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu kama hungepewa kutoka juu,” Soma Yohane 19: 10-11.

Utii kwa Serikali ni muhimu kwa sababu kuna msingi wake. Mtume Paulo ameandika hivi: “Kila mtu aitii mamlaka ya wenye kutawala, kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu. Basi, anayekataa kuitii mamlaka anashindana na agizo la Mungu, lakini wenye kushindana nalo wajipatia hukumu” Warumi 13:1-2.

Kwa kuwa wakubwa wa Serikali wamepata mamlaka yao kwa Mungu, hawawezi kutawala jinsi wapendavyo, bali imewapasa kuzijali amri za Mungu na kutawala kwa kadiri yake. Haifanyi tofauti kama wamerithi cheo au wamechaguliwa na raia wenyewe. Mwisho watahukumiwa na Mungu.

Mara kwa mara kuna watawala wabaya wasiomtii Mungu. Hao wataadhibiwa na Mungu. Lakini raia wana lazima wawatii ispokuwa huamuru neno lililokatazwa na Mungu, kwa maana wanashika mamlaka kwa haki ijapo wanaishutumu.

Watawala, ambao Mtume Paulo amewaambia wakristo wake wawatii, walikuwa wapagani wenye mazoea mabaya. Yesu amesema. “ Yo yote watakayowaambia yashikeni na kuyatenda, lakini matendo yao msiyafuate” Mt 23:3. Wakristo wa zamani waliwatii hata watawala wadhulumu katika mambo yote ya Serikali, ila walikataa kukana dini au kutenda yaliyokatazwa na Mungu.

Kwa hiyo ni wajibu wetu kuitii Serikali kwa ajili ya Mungu, siyo kwa hofu ya kukamatwa. Ukifikiri, sitalipa kodi nikipata nafasi ya kutolipa, wala sitazishika amri nyingine za

Serikali nikiona njia za kuziepuka, huna maono ya kikristo. Kumbuka kuwa hupatwi na kosa tu unapokamatwa bali kuivunja Sheria kwenyewe ni kosa. Mtume Paulo ameandika hivi. “ Hamna

budi kuinyenyekea Serikali siyo kwa ajili ya adhabu tu, lakini pia kwa ajili ya dhamiri…….. Basi, wapeni wote yawapasayo, kodi astahiliye kodi, Ushuru, astahiliye ushuru, hofu astahiliye hofu, heshima astahiliye heshima “ Warumi 13:5-7.

Kodi na Sheria zote za Serikali zimewekwa kwa ajili ya mafaa ya watu wote. Ndugu yangu unapozivunja hizo unakosa  amri ya 4 ya Mungu inayotudai kuwaheshimu baba na mama, ili upate miaka mingi na heri duniani. Tena na amri kuu ya mapendo, maana unawanyima wenzako haki yao.

Mwandishi ni Padri wa
Kanisa Kuu JIMBO
Katoliki – KIGOMA.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU