Miaka 100 ya upadri Tanzania Bara imewaunganisha waafrika

Askofu wa Jimbo Katoliki Morogoro Mhashamu Telesphor Mkude amesema kuwa kufikia miaka 100 ya upadri tangu kuingia Tanzania Bara, kumeleta mafanikio ya kufahamiana, kuimarishana na kufikiri pamoja katika masuala ya imani kujenga Kanisa la Mungu.
Amesema hayo ofisini kwake hivi karibuni alipokuwa akizungumza na gazeti hili juu ya maadhimisho ya Jubilei ya miaka 100 ya Upadri Tanzania Bara, ambayo kilele chake kitaadhimishwa kitaifa katika Jimbo Kuu Katoliki Dodoma katikati ya mwezi Agosti mwaka huu.
Askofu Mkude amesema kuwa kufuatia jubilei hiyo ya miaka 100, imekuwepo idara maalumu inayohusika na Mapadri nchi nzima, (UMAWATA) ama Umoja Wa Mapadri Wazalendo Tanzania ili kuendeleza na kufwata misingi iliyoachwa na wamisionari, na kukabili yaliyopo kwa sasa ili kujenga imani ya kweli ya Kanisa na sheria zake
Hata hivyo Askofu Mkude amesema moja ya majukumu ya mapadri ni utumishi katika kuratibisha, kuhubiri, kutoa masakramenti, kuongoza waamini, kuelekeza waamini ndani ya Kanisa, hasa jumuiya na makundi mbalimbali katika Kanisa ili viweze kuwa ndani ya mchungaji mmoja
Sambamba na hayo amefafanua kuwa si vyema Kanisa kutawaliwa na Maaskofu na Mapadri pekee.
“Kanisa linapaswa kutawaliwa na walei wenyewe ndani ya Kanisa kwa kupewa maelekezo, kushirikishwa mambo mbalimbali ndani ya Kanisa ili kueneza uinjilishaji wa kina,” amesema Askofu Mkude.
Amesema kuwa wazo la mapadri kuendelea kushirikiana katika mambo ya kiroho, nchi za AMECEA yaani Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Afrika Mashariki na Kati ikiwemo nchi ya Kenya, Uganda, Madagascar, Ethiopia, Malawi, Zambia, Tanzania, Sudan na Somalia.
Hawa ni waafrika ambao wameungana kufanya mambo mbalimbali katika uinjilishaji wa kina kufikisha mwanga wa injili ulimwenguni pote kwa lengo la kuwatumikia watu.
Wakati huohuo Askofu mkude ametoa pongezi kwa waamini kwa jitihada zao za kuwaombea viongozi wa dini, akisema kuwa sala za waamini ni muhimu sana bila sala hizo hawawezi kusimama imara katika imani, kwani mchungaji anapoanguka kiroho anaanguka na watu kadhaa.
“Msichoke kuwaombea viongozi wa dini, kwani sala zenu waamini ni muhimu sana, bila sala hizo hatuwezi kusimama imara katika imani, kwani mchungaji anapoanguka kiroho anaanguka na watu kadhaa,” amesema Askofu Mkude.

Kufikia miaka 100 ya upadri Tanzania Bara, kumeongeza idadi ya Maaskofu na Mapadri waafrika kuwa wengi zaidi na uwepo wa seminari ndogo na kubwa kama kielelezo cha kuendelea kufahamiana zaidi kiasi kwamba uwepo wa seminari hizo humsaidia padri anaposafiri kwenda Jimbo jingine hukutana na mapadri wengine anaofahamiana nao.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU