Mashemasi waige mfano wa mamajusi

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora Mhashamu Paul Ruzoka amewaasa mashemasi na waamini kumpenda Kristo zaidi na kuwa tayari kupeleka Imani ya Kikristo kwa watu wote katika maisha yao pendwa kwa Mungu.
Askofu Mkuu Ruzoka amesema hayo wakati wa adhimisho la Misa Takatifu katika Kanisa la Kiaskofu Tabora wakati wa sherehe ya tokeo la Bwana.
Akitoa mahubiri yake kwa wana jimbo na waamini toka majimbo jirani ambayo baadhi ya mashemasi hao wanatoka, Askofu Mkuu Ruzoka amesema kuwa Mamajusi walitoka sehemu mbalimbali tofauti na bila kutaarifiana na kujikuta wanakutana Bethlehemu kumsujudia na kumwabudu Mwokozi hivyo imani iliwakutanisha.
Aidha Askofu Mkuu Ruzoka amesema imani peke yake ndiyo kitu kilichowafanya Mamajusi hao wavumilie tabu na changamoto walizokutana nazo safarini bila kukata tamaa, bila imani safari yao isingekuwa na mafanikio.
Mashemasi Ignas Akilimali, Francis Kiguli na Fabian Mkama wamefananishwa na Mamajusi ambao baada ya kufika Bethlehemu na kutoa zawadi zao yaani dhahabu, uvumba na manemane walirudi kwa njia nyingine ambapo mashemasi hao walianza safari yao ya malezi kwa njia ya kawaida toka makwao, lakini baada ya kuwa mashemasi wanaanza maisha ya Useja yaani wanaanza safari kwa njia nyingine tofauti na ile waliyokuja nayo awali.
Aidha amesema jamii kwa kawaida inaelewa na kuzoea kuona kijana akifikia umri fulani hana budi kutafuta mwenzi wake na kufunga ndoa kanisani ambapo nderemo na vigelegele hutawala, ila kwa hawa vijana haitakuwa hivyo.
"Mashemasi mnapaswa kumpenda sana Kristo na kujitoa kwake kimwili na kiroho ili awatumie kwa ajili ya kuwapeleka watu kwa Kristo, aliye njia ya ukweli na uzima," Askofu Mkuu Ruzoka  amesema.
“Kama tunavyosoma, Mamajusi hawa baada ya kumuona mtoto na kutoa zawadi zao walirudi makwao na kitu fulani walichokuwa wamepata na kuwa tayari kukipeleka kwa wale waliokutana nao, hivyo basi mashemasi pelekeni habari njema kwa watu wote yaani uwepo wa Kristo katika ulimwengu wa leo.”
Amewatia moyo mashemasi hao na kuwaomba kuwa na moyo mkuu wa kuvumilia changamoto ambazo wanaweza kukutana nazo katika kutekeleza majukumu yao.
“Mamajusi walisikia na kupokea mpango wa Mungu katika ndoto na hawa vijana wanapaswa kuzingatia malezi waliyoyapata wakati wote walipokuwa wanafundwa katika nyumba za malezi.(seminari zao).”


Jimbo Kuu Katoliki Tabora linatarajia kupata mashemasi wengine mapema mwezi Machi mwaka huu ambapo wito umetolewa wa kuendelea kuwaombea mashemasi hao  ili wafanye yote kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mwenyezi Mungu.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU