Eti Wasomi wa Siku hizi hamna kitu: Ni wasomi au mfumo wa elimu umechoka?

JAMII yetu imewachoka wasomi. Inawasema vibaya! Wasomi hawaheshimiki tena kama zamani. Eti wasomi wa siku hizi ni hamna kitu. Yaani ni Tabula rasa. Ajabu sana. Mtu ametumia karibu nusu ya maisha yake akisoma leo anaambulia kuitwa hamna kitu. Unajua Mungu anawaona?
Kijana mmoja anawatukana walimu kwamba tunazalisha wasomi vihiyo. Acha atukane tu maana mdomo ni mali yake. Anayemtukana mwalimu ni dhahiri hajitambui, maana angejitambua angefahamu kwa nini ualimu ni wito.
Sharti la kuwa mwalimu lazima ujikane mwenyewe na kuubeba msalaba wa wajinga kwa malipo ya kufedheheshwa na kudhalauriwa. Ndiyo! Mwanafunzi akifeli ni uzembe wa mwalimu, akifaulu ni juhudi zake mwenyewe! Na huu ndiyo wito wenyewe. Asiyekuwa nao hawezi!
Imekuwa fasheni hata aliyeshindwa shule kumsema ovyo msomi. Ni kutukana tu. Msanii mmoja wa BongoFleva aliyeishia darasa la nne anasema haoni umuhimu wa elimu kwa sababu kupitia muziki ana kipato kikubwa kuwashinda waliosoma na bado amewaajiri  waliosoma.
Unaibeza elimu, lakini unawatumia wasomi katika kazi zako. Ni sawa na Chichidodo ndege anayesema kinyesi ni uchafu lakini anakula minyoo kutoka kwenye kinyesi hicho. Huyu Msanii ni mpumbavu. Mbona kuna walioacha shule na kukimbilia muziki lakini bado wanahenya?
Hapa ndiyo utajua kila asemaye Bwana Asifiwe atakwenda Mbinguni. Mfalme Suleiman hakukosea aliposema, Hata ukimtwanga mpumbavu kwa mchi kinuni pamoja na ngano, upumbavu wake hautamtoka.
Hata madiwani nao wanasema wasomi hawana kitu. Maskini ya Mungu. Madiwani wengine hata kusoma na kuandika tu ni shida, nao wanabeza. Huku kukaririshwa cha kusema, kunadhalilisha watu kwa kweli. Tembelea Halmashauri uone wakurugenzi wanachofanyiwa na madiwani. 
Ni vitisho na amri za kuudhi tu. Kitendo cha Diwani kumwambia mkurugenzi ni mbabaishaji hivyo afukuzwe kazi ni muujiza kama ilivyo miujiza mingine. Mbiti anakwambia shida ni kwamba watu weusi tunatumia hisia na vionjo zaidi ya akili katika kufikiri ndo maana maajabu hayaishi. Unadhani kwa nini TANESCO imeshindwa kuangaza maisha ya watanzania wote?
Tatizo, wataalamu wanaelekezwa nini cha kufanya na wanasiasa. Yaani ni sawa na fundi cherehani akafanye kazi za upasuaji kwa sababu ana uzoefu mkubwa wa kutumia mkasi. Enyi wajinga, hata lini mtapenda ujinga?Anauliza Mfalme Suleiman.
Lakini pia wasomi wenye nafasi zao serikalini na katika sekta binafsi nao wanasema ovyo kuhusu wasomi wa siku hizi utadhani wao walisomea Mbinguni. Utaskia, vyuo vikuu vya siku hizi vinazalisha mburula.
Ukiwauliza kwa nini wanasema hivyo, watakwambia wasomi wa siku hizi hawajui kiingereza. Yaani wao kigezo cha usomi ni uwezo wa kumudu lugha ya kikoloni. Huu kama si utumwa wa fikra ni nini?
Sasa kuna lugha nyingine za ovyo kabisa. Eti unaweza kusoma sana lakini maisha yakakupiga. Waliofanikiwa katika maisha wanajisifia kwamba mafanikio yao hayakutokana na elimu bali juhudi binafsi. Wanakwenda mbali zaidi na kuiaminisha jamii kwamba kusoma sana ni kujitafutia umaskini. Wengine wanatoa takwimu za ovyo ovyo kwamba hakuna tajiri aliyesoma sana utadhani shuleni tunafundisha utajiri.
Kuyaruhusu mawazo ya namna hii kuendelea kuishi katika jamii ni kuiua jamii. Kwa sababu jamii hiyo itapuuza elimu na hapo majanga yatatokea. Vyuoni hatufundishi utajiri bali tunafundisha ustaarabu.  Hatuwezi wote kuwa matajiri lakini wote tunaweza kuwa wastaarabu. Tumekuwa jamii ya kubeza elimu na wasomi wetu kupitia tungo za kuchekesha, tungo ambazo husambazwa kupitia whatsap kama sehemu ya burudani.
Eti kuna maprofesa 40 walipanda Air Tanzania ili wasafari. Kabla ndege haijaanza kuondoka, lilipita tangazo kama ifuatavyo: Ndugu wasafiri wote, ndege unayotarajia kusafiri nayo imetengenezwa na wanafunzi wa Kitanzania. Baada ya tangazo maprofesa wote waliteremka isipokuwa mmoja alibaki kwenye kiti chake.
Walipomuuliza ni kwa nini hakuondoka akajibu kwa haraka na furaha kuwa: Kama ndege hii imetengenezwa na watanzania, hata kuwaka haitawaka!” Huku kama siyo kuwafedhehesha wasomi wetu ni nini? Tungo kama hizi pengine ndiyo husababisha viongozi wetu nao kuwabeza wasomi. Kiongozi mmoja kauita utafiti uliofanywa na wasomi kwamba ni lamli. Asiye na akili siku zote humbeza mwenzake alisema Mfalme Suleiman.
Angalia utungo huu nao, “Kijana mmoja akaulizwa hivi ukiambiwa upewe milioni kumi za Kitanzania uchome vyeti vyako utakuwa tayari? Kijana akajibu nitakuwa tayari siyo vyeti tu nitachoma mpaka nyumba zote za waalimu na mabweni na kila kitu”.  Hivi tungo kama hii inatufundisha nini zaidi ya kuidhalilisha elimu yetu? Kwamba elfu kumi ina thamani kuliko elimu ya Tanzania! 
Kitendo cha kuibeza elimu yetu kimewafanya watanzania wengi kukosa imani na shule zetu kabisa. Badala yake, shule zetu zimebaki ni kimbilio la walala hoi, huku walala hai wakiishia shule za kimataifa na Ughaibuni. Kuna jamaa aliwapeleka watoto wake Uganda wakarudi wanaongea kiganda. Walirudi ni wajinga zaidi ya walivyokwenda. Alifikiri Uganda nako ni Ughaibuni.  Jamani mbona tunakuwa kama ndege aendaye haraka mtegoni?
Masengenyo haya huwafanya wasomi wajiskie vibaya na kuwa wanyonge. Nadhani kama wasomi hawapaswi kujibu mapigo kwa kila anayewatukana, badala yake kama jamii tuupitie tena mfumo wetu wa elimu upya. Ni ukweli usiopingika kwamba mfumo wetu wa elimu hauwezi kuandaa watu watakaoendani na kasi ya dunia.
Tunatakiwa kuufumua na kuusuka ili uweze kuzalisha wasomi watakaokuwa wakombozi wa jamii, wasomi watakaotoa majibu ya matatizo ya jamii yetu badala ya kuendelea kuwa na wasomi wanaotegemea kuajiriwa na wakati ajira zenyewe hatuna. Juma lijalo nitajadili elimu tuitakayo! Asanteni!



Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU