Kardinali Pengo: Muungano si bahati nasibu

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewataka waamini na wananchi kwa ujumla kutambua kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar si jambo la bahati nasibu.
Kardinali Pengo ameyasema hayo ofisini kwake hivi karibuni alipoitisha vyombo vya habari vya Kanisa Katoliki kuzungumzia pamoja na mambo mengine ongezeko la Parokia mpya jimboni kwake pamoja na mabadiliko kwa Maparoko na Maparoko Wasaidizi katika baadhi ya Parokia jimboni humo.
Asemema suala la Muungano linapaswa kuchukuliwa kwa uzito wa pekee kwa kila Mtanzania hasa waamini Wakatoliki na kwamba kila mwamini anapaswa kutambua kuwa amepewa jukumu na Mwenyezi Mungu kulinda na kuombea Muungano huo.
Kardinali Pengo anasema ni jambo la kushangaza jinsi Mungu anavyotenda mambo yake kwa wanadamu kwani alileta Imani Katoliki kupitia Zanzibar na kwamba baada ya Uhuru Mungu aliwapatia neema watu wake wa pande mbili za Zanzibar na Tanganyika kuungana na kuwa kitu kimoja.
Anasema wakati Kanisa likijiandaa kwa adhimisho la Jubilei ya miaka 150 ya uwepo wa Kanisa Katoliki katika eneo la Afrika Mashariki ifikapo 2018 Zanzibar haiwezi kuwekwa pembeni.
Kuhusu utendaji wa serikali ya awamu ya tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kardinali Pengo anasema hali inaonesha viongozi wa taifa hili wameanza vizuri na kasi yao inaleta matumaini makubwa.
Kardinali Pengo anawaomba wananchi wa Imani zote kumuombea Rais Dakta John Pombe Magufuli kwa Mwenyezi Mungu ili alinde uongozi wake na auimarishe uweze kubaki katika malengo yake ya kuleta maendeleo kwa Watanzania wote.
Anaongeza kuwa ni wajibu wa kila mwananchi kuomba kwa Mungu ili ibilisi asije akawabadilisha mioyo wale ambao wanaonekana ni watetezi wa wanyonge wakaanza kutenda kinyume na matarajio ya wananchi walio wengi.
“Ibilisi ana namna yake ya kufanya vitu mnaweza kushutukia tu mambo yamebadilika wale ambao mnatarajia wawe watetezi wa Watanzania wa chini wanageuka kuwa ndiyo wakandamizaji wakubwa kwa Watanzania wanyonge.” Amesema Kardinali Pengo

Ujenzi wa Nyumba ya Askofu Bagamoyo
Kwa namna ya pekee anawashukuru waamini Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam kwa majitoleo yao ya fedha katika kuhakikisha ujenzi wa nyumba ya Askofu katika jimbo Katoliki tarajiwa unafanyika kwa mafanikio makubwa.
Kardinali Pengo anasema mpaka sasa amefanikiwa kupata michango kutoka kwa waamini mbalimbali kiasi cha shilingi milioni miatatu na kidogo ambazo zimesaidia kuanza kwa ujenzi huo kwa kasi kubwa.
“Naomba kuwashukuru wale wote walioniwezesha kuzipata fedha hizo kwa ajili ya huo mradi” amesema Kardinali Pengo
Amesema katika kuhakikisha ujenzi huo unafanikiwa Jimbo Kuu Dar es Salaam kutoka katika akiba yake limetoa shilingi milioni miambili hamsini na hivyo kufanya idadi ya pesa zilitolewa kwa ajili ya mradi huo kuwa shilingi milioni miatano na hamsini.
Amesema pesa hizo ni nyingi na zimefanya kazi kubwa lakini hazitoshi kukamilisha mradi huo kutokana na gharama za ujenzi kuwa kubwa kwa nyakati hizi hivyo kiasi hicho bado hakitoshelezi kukamilisha mradi huo.
Kutokana na hali hiyo Kardinali Pengo anasema kiasi cha fedha ambacho si pungufu ya milioni mianne bado kinahitajika na hivyo anaendela kuwasihi waamini kujitokeza kwa wingi kutoa michango yao ili kukamilisha mradi huo kwa wakati.
Anasema matarajio yaliyopo ni kwamba mpaka kufika mwanzoni mwa mwaka 2018 ujenzi huo uwe umekamilika ilikusudi ikimpendeza Baba Mtakatifu aweze kulipatia jimbo tarajiwa la Bagamoyo Askofu Mpya katika mwaka huohuo unaotarajiwa kufanyika sherehe za miaka 150 ya Ukatoliki Afrika Mashariki na kwamna ya pekee nchini Tanzania.
Amesema lengo lake la kuzungumzia juu ya mradi huo ni kuomba ukarimu wa waamini kwani Maaskofu wa Baraza Katoliki Tanzania waliamua wazo la kupata Askofu wa Bagamoyo na wazo kumuomba Baba Mtakatifu atengeneze jimbo Katoliki Bagamoyo kwa mwaka 2018 na uhakikishaji wa kuwa na mahali pa kukaa kwa Askofu Mpya ni jukumu la Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Dar es Salaam.
Amesema kwakuweka nguvu pamoja mradi huo utafanikiwa na kwamba anawaombea kwa Mungu ili azidishe ukarimu wao na afanikishe maendeleo ya kila Parokia na pia afanikishe maandalizi ya Jubilei ya miaka miamoja na hamsini ya Kanisa Katoliki Mashariki mwa bara la Afrika ifikapo mwaka 2018.

Atagaza parokia mpya
Aidha Kardinali Pengo ametangaza ongezeko la Parokia sita mpya na hivyo kunalifanya jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam hilo kuwa na jumla ya Parokia tisini na tano kutoka themenini na tisa za awali.
Parokia hizo mpya ni miongoni mwa vigango kumi na moja ambavyo awali vilitangazwa kuwa Parokia teule Januari sita mwaka huu wakati wa utoaji wa daraja takatifu ya Ushemasi kwa Mashemasi wawili wanaotarajiwa kupata sakramenti ya Upadrisho mapema Julai mwaka huu.
Mwadhama anasema anayomategemeo ikimpendeza Mungu ifikapo Julai mwaka huu baada ya Upadrisho wa Mapadri wapya wa Jimbo upo uwezekano wa kupata Parokia nyingine.
Parokia mpya zilizotangazwa na Mwadhama kuwa Mpya ni pamoja na Parokia ya Kijitonyama ambapo Padri Arnold Babu Tarimo wa Shirika la Kazi za Roho Mtakatifu (OSS) ameteuliwa kuwa Paroko wa Parokia hiyo, Parokia ya Mshikamano ambayo itakuwa chini ya uongozi wa Paroko Bartholomew Mrosso Padri wa Shirika la Wamisionari wa Afrika na Parokia ya Mbande ambayo Paroko wake ni Padri Pushpa Raj, Padri wa Shirika la Bikira Maria Imakulata (MMI).
Nyingine ni Parokia ya Msakuzi Mbezi Mwisho ambapo Padri Fulgence Oisso wa Shirika la Rosminiani ameteuliwa kuwa Paroko wa parokia hiyo, huku Padri Wolfgang Michael Tengia wa Shirika la la Wamisionari wa Clareti akiteuliwa kuwa Paroko wa Parokia Mpya ya Michungwani Kimara na Parokia ya sita ni Parokia ya Mtakatifu Rita iliyopo Kimara Temboni ambayo Paroko wake ameteuliwa Padri Constantine Mlelwa ambaye ni Padri wa Shirika la Mt. Agustino.

Mabadiliko ya Maparoko
Katika hatua nyingi Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amefanya mabadiliko ya Maparoko na Maparoko Wasaidizi kwa baadhi ya Parokia za Jimbo Kuu Dar es Salaam amabapo utekelezaji wa mabadiliko hayo unaanza mara moja Mei Mosi mwaka huu.
Katika mabadiliko hayo Paroko wa sasa wa Parokia ya Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Padri Theophile Hostie Bolampeti ameamishiwa katika Parokia ya Manzese kuwa Paroko wa parokia hiyo ambayo awali ilikuwa chini ya uongozi wa Mapadri wa Shirika la Wasionari wa Afrika (White Fathers)
Pamoja na kwamba Parokia ya Manzese sasa inahudumiwa na Mapadri wazalendo, kwa namna ya pekee Kardinali Pengo amewaomba Mapadri wa Shirika la Wamisionari wa Afrika kuendelea kutoa Mapadri Wasaidizi katika Parokia hiyo hadi mwezi Julai mwaka huu.
Padri Joseph Matumaini ambaye alikuwa Paroko wa Parokia ya Magomeni ameteuliwa kuwa Paroko Mpya wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu na anaendelea kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Uchungaji Jimbo Kuu Dar es Salaam.
Mwadhama anasema kwakuwa Padri Matumaini ndiye Mkurugenzi wa Uchungaji jimboni ameona si vyema akae mbali na Mchungaji Mkuu wa Jimbo ambaye ni Askofu.
Hii ni mara ya pili kwa Padri Matumani kushika nafasi ya Uparoko katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu kwani aliwahi kuwa Paroko wa Parokia hiyo ya Kanisa Kuu kati ya mwaka 2002 hadi mwaka 2004 na kabla ya hapo aliwahi kuwa Paroko Msaidizi kanisani hapo kati ya mwaka 1998 hadi mwaka 1999.
Aidha Padri Christian Likoko ameamishwa kutoka Parokia ya Kizinga na ameteuliwa kuwa Paroko Mpya wa Parokia ya Magomeni huku Parokia ya Kizinga ikibaki chini ya uongozi na uangalizi wa Paroko Msaidizi.
“…kule parokiani Kizinga bado hatujapata Paroko lakini yule ambaye amekuwa Msaidizi katika parokia hiyo anashika majukumu siyo tu ya Usaidizi lakini pia ya Paroko hadi hapo itakapoonekana ni lazima ama kuweka mwingine au kumfanya yeye mwenyewe kuwa Paroko” amesema Kardinali Pengo.
Wengine waliamishwa katika vituo vyao vya kazi ni pamoja na aliyekuwa Paroko Msaidizi Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu Padri Asisi Mendonca ambaye sasa ni Paroko Msaidizi Parokia ya Mtakatifu Petro Oysterbay na Padri Edward Sabbas aliyekuwa akihudumu kama Paroko Msaidizi Parokia ya Mtakatifu Petro Oysterbay ameteuliwa kuwa Paroko Msaidizi Kanisa Kuu la Mtakatifu Yosefu.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU