Wazazi wana wajibu wa kuchochea miito

ASKOFU wa Jimbo Katoliki Tanga Mhashamu Anthony Banzi amewahimiza wazazi na wana jumuiya kuichochea miito ya vijana wao ya kuwa watawa na mapadri ili isiishie njiani na kutimiza kusudi ambalo Mungu ameweka ndani yao.

Amesema hayo katika ibada ya kutoa Daraja Takatifu la Ushemasi kwa shemasi Gitaga Okindo wa shirika la  Mapendo ambayo imefanyika jimboni Tanga na kuhudhuriwa na watu mbalimbali akiwemo mkuu wa shirika.

Askofu Banzi amesema kuwa, wazazi wana jukumu la kuhakikisha vijana hawaishii njiani katika kutimiza wito wao wa kumtumikia Mungu, wawasaidie ili kusudi la Mungu litimie kwa kuwa tayari ameweka kitu ndani yao.

“Wazazi mpo karibu na vijana wetu hivyo mkiona  mwelekeo wa mtoto ni kuifanya kazi ya Mungu usimwache akaishia njiani, mtieni moyo na kumsisitiza kufanya yanayompendeza Mungu ikiwemo kumpeleka seminari ndogo ili atimize kusudi la kumtumikia Mungu,” amesema Askofu Banzi.

Amesisitiza kuwa, kuwatoa vijana siyo kuwapoteza, ikiwa kijana ana hiyo karama basi apewe ushirikiano na miongozo kwani hapotezwi ila anawekewa hazina Mbinguni kwa kuwa Mungu anamuhitaji ili aifanye kazi yake.

“Mtoto ni zawadi toka kwa Mungu, hivyo anapoihitaji zawadi aliyokupa ifanye kazi yake usiizuie kwa kutoa sababu ambazo hazina mashiko machoni pa Mungu, mpe Mungu cha kwake haupotezi ila unajiwekea hazina mbinguni na matunda yake utayaona,” amesema Askofu Banzi.
Amesema umeshuhudiwa upungufu wa mapadri katika Kanisa lakini wazazi na jamii wakishirikiana kumtia moyo kijana kutimiza wito ambao Mungu ameweka ndani yake, kutakuwa na mapadri wa kutosha.


“Uzalishaji wa mapadri hauridhishi, siyo kama hawapo wenye huo wito, wapo ila baadhi ya wazazi wanawakwamisha vijana wao hivyo wazazi na jumuiya kwa msisitizo mkubwa, tusiwakatishe tamaa badala yake tuwe nao bega bega ikiwemo kuwapeleka seminari ndogo ili watimize wito wao, kwa kufanya hivyo hatupotezi ila tunawekeza kwa Mungu,” amesema Akofu Banzi.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU