Kwa nini wakatoliki huingia kanisani na viatu, na kukaa kwenye viti?

SWALI. Kwa nini sisi Wakatoliki tunaingia kanisani na viatu? Amri ya Mungu ilitoka katika Kut 3:5 mahali tusomavyo ifuatavyo, “Mwenyezi Mungu akamwambia, ‘Usije  karibu! Vua viatu vyako kwa sababu mahali hapa unaposimama ni mahali patakatifu’”. Swali hili nimeulizwa kwa ujumbe wa simu.
Jibu: Musa alipewa amri ya kinidhamu tu. Musa aliagizwa kufanya vile kimwili kuashiria jambo la kiroho. Baada ya kusoma vyema Biblia, Wakristo tumegundua kwamba Mungu ni roho na anapaswa kuabudiwa rohoni.
Imeandikwa katika Yn 4:21-24 hivi, “Yesu  akamwambia, ‘Niamini wakati unakuja ambapo hamtamwabudu Baba juu ya mlima huu, wala kule Yerusalemu. Ninyi Wasamaria mnawambudu yule msiyemjua, lakini sisi tunamjua huyo tunayemwabudu kwa maana wokuvu unatoka kwa Wayahudi.
Lakini wakati waja, tena umekwisha wasili, ambapo wenye kuabudu wa kweli watamwabudu Baba katika roho na ukweli. Maana Baba awataka watu wanaomwabudu namna hiyo. Mungu ni roho na watu wanaomwabudu lazima wamwabudu kwa Roho na ukweli.’”
Kwa neno hili la Mungu (Yesu Kristo), Wakristo tumeelewa vyema kwamba makubasi anayokataa Mungu na tunayopaswa kuyavua kabla ya kumjongea Mungu ni dhambi na siyo viatu na makubasi haya yanayoonekana. Siyo buti hizi au ndala na  yeboyebo hizi za miguuni. Kinyume chake ni dhambi zilizo rohoni mwetu ambamo tunakutana na  Mungu Mtakatifu.
Tunamwabudu Mungu rohoni, basi humo ndimo mnamopaswa kuwa safi kabla ya kumjongea Mungu mtakatifu. Namna ya kuvua viatu na makubasi ya kiroho ni kujongea kwa muungamishi na kuungama dhambi. Ni kukikabili kiti cha Kitubio.
Ndipo tunahimizana kufanya toba (kuungama) kabla ya kujongea sakramenti, kama vile, Kipaimara, Ekaristi Takatifu, Ndoa na Daraja. Kwa jumla tunahimizana kuacha dhambi, ndiyo kuvua makubasi, kabla ya kumkaribia Mungu. Kifupi, ni suala la kuachana na makubasi ya rohoni, yaani dhambi na siyo viatu au makubasi haya ya miguuni. 
Swali 2. Kwa nini tunakaa kwenye viti na siyo kwenye majamvi kama kipindi cha Yesu walivyokuwa wakikaa hekaluni? Swali hili nimeulizwa vile vile kwa ujumbe wa simu.
Jibu: Awali ya yote si kweli kwamba wakati wa Yesu watu walikuwa wakikaa kwenye majamvi. Huku ni kulazimisha mambo ya siku hizi yasomeke kwenye Biblia. Yesu aliishi katika karne ya kwanza B.K.na wakati ule hekaluni na hata kwenye masinagogi hakukuwa kunatumika majamvi kwa ajili ya kukaa waamini. Aidha, hamkuwa na benchi za kukaa. Watu walikuwa wanasali wangali wamesimama.
Lakini hata kama majamvi yangelikuwepo wakati ule, Wakristo hawapo kusudi waige kila kitu cha Wayahudi ijapokuwa Kristo alikuwa Myahudi na alianzia kule kuhubiri. Ukristo ni dini mpya na tofauti na dini ya Kiyahudi. Kama dini mpya ina haki ya kuwa na desturi zake wala si lazima “kukopi” mambo na desturi zote za Wayahudi.
Majamvi ya leo tusiyapeleke kwenye karne ya kwanza B.K. sembuse kabla yake. Wakati ule haya mambo tuliyoyazoea  sasa hayakuwapo kama yalivyo leo. Natoa mifano. Mfano, hakukuwa na karatasi walitumia ngozi za mbuzi au kondoo. Walitumia pia magombo  ya matete yaliyopondwa na kugandishwa kwa aina ya gundi.
Mikeka, mazulia na majamvi yalikuwa nadra mno labda kwa matajiri wakubwa sana. Shida hii ilitokana na viwango vya chini vya sanaa za kufuma na kusuka. Hakukuwa na viwanda. Nguo zilikuwa za kufuma kwa kutumia sufu na manyoya ya mbuzi. Tena ilikuwaa kazi ya mama kufuma kwa mikono. Mama mvivu alimaanisha watu wa familia yake kutokuwa na nguo (rej. Mit 31:10-31).
Majamvi hayakuwako. Magodoro hayakuwako. Vitanda vya mbao na kadhalika havikuwako. Ukisikia godoro au kitanda cha mtu, ilikuwa na joho lake. Majoho ndiyo yaliyotumika kwa wakati mmoja kama mkeka na blanketi. Majoho yalikuwa makubwa. Mtu alipolala alitumia sehemu fulani kutandika chini na upande mwingine kujikunjia kama blanketi.
Ndiyo maana hata Yesu alipokuwa anaingia Yerusalemu walifaulu kumtandikia nguo zao tu na wala siyo mikeka na mazulia (rej. Mk 11:8). Hivi hekaluni sawa na kwenye masinagogi hakukuwa na mikeka yoyote.
Pili, hekaluni na kwenye masinagogi waamini hawakuwa wanakaa. Hekaluni na kwenye masinagogi waamini walikuwa wanasimama. Hivi, kwa ujumla, kusema kulikuwa na majamvi na kwamba watu walikuwa wakikaa ni kuongopa.
Walikokuwa wanakaa walikuwa viongozi wawili (mkuu wa ibada au kwenye sinagogi – mkuu wa sinagogi na msaidizi wake hazzan). Wengine wote walikuwa wanasimama. Ndiyo maana kwenda kusali kulikuwa kunajulikana pia kama “kwenda kusimama mbele ya Bwana (rejea Zab 24:3, 130:3, 134:1 na 135:2). Hivi hakukuwa hata na haja ya kuwa na mikeka.
Nina mashaka. Swali linaonekana kutokea kwenye mazingira ya Waislamu wanaotaka kuonesha kwamba mikeka wanayotumia misikitini inaendana na mambo yaliyokuwa yanatumiwa hekaluni au kwenye sinagoni enzi za Yesu.  “Ulazimishaji” huu wa mambo si sawa.
Kukaa kama kukaa kulikuwa nje ya nyumba za ibada, hususan majumbani mwa watu. Hata kwenye karamu kubwa kubwa watu hawakukaa isipokuwa waliegemeana (kama  kulaliana vile). Mfano wake ni namna walivyoegemeana kwenye karamu ya mwisho.
Kumbe, tangu Ukristo ulipoanza, namna ya kukaa kwenye mikutano ilikuwa huru kwa Wakristo. Ilitegemea tu mila na desturi za watu waliofikiwa na Ukristo. Wapo waliokuwa wakikaa kama Wayahudi kwenye “fomu” na kuegemeana. Wapo waliokuwa wakisimama tu na kadhalika. Matumizi ya benchi yametokea Ulaya. Ulaya walipopokea Ukristo na kujenga makanisa, waamini waliingiza namna zao na desturi zao za kukaa kanisani, kwani ilikuwa huru.
Upigaji magoti uliingizwa baadaye na Mtakatifu Francis wa Assisi baada ya kupata wazo la kupiga magoti kutoka katika safari yake ya Misri. Kule aliwaona watu wakipiga magoti, ndipo akapenda Wakristo wafanye hivyo hivyo mbele ya Ekaristi Takatifu. Hivi ni Wakristo Wazungu walioingiza viti vya kuhamishika (katika basilica) na visivyohamishika ndiyo benchi za kukalia na kupigia magoti.
Lakini, pamoja na hayo yote, Wakristo wanajua bado kwamba mkao wa kanisani ni huru. Haikatazwi, wenye mikeka na mazulia wanaweza kutumia. Wenye vigoda wanaweza kutumia na kadhalika.

Katika yote, tukumbuke bado kwamba Wakristo hawapo kusudi waige kila kitu cha Wayahudi ijapokuwa Kristo alikuwa Myahudi na alianzia kule kuhubiri. Ukristo ni dini tofauti na dini ya Kiyahudi. Wakristo tunatakiwa kumwabudu Mungu na kusali, kwa namna zipi na tungali tumekaa  vipi, bado ni huru. Tunaagizwa tutumie akili tu (rej. Mt 22:34-40).

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU